Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein Alifungua Kongamano la Sita la Diaspora Tanzania Kati Ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni leo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali.Mohamed Shein akihutubia Wanadiaspora wakati wa Ufunguzi wa Kongamano la Sita la Diaspora Tanzania lililofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar.  


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameahidi kwamba atahakikisha anapomaliza muda wake  wa Urais suala la Diaspora limeshakaa sawa kimkakati, kisera pamoja na kisheria kwa upande wa Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Hoteli ya Verde, Mtoni Mjini Zanzibar wakati akifungua Kongamano la Sita la Diaspora.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa anaamini kwamba kutakuwa imeiwekea mazingira mazuri uongozi wa Awamu inayofuata ya Nane katika kulisimamia vizuri suala hilo.

Hivyo, Rais Dk. Shein alimuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ahakikishe kwamba anasimamia kwa karibu utayarishaji na kukamilika kwa rasimu ya sheria ya Diaspora ili iweze kuwasilishwa katika Baraza la Wawakilishi kabla ya mwezi  Mei, 2020.

Aliongeza kuwa kuwepo na kutumika kwa Sera ya Diaspora iliyoizindua rasmi mwaka jana tarehe 09 Mei, 2018 kumerahisisha juhudi zinazoendelea kuchukuliwa hivi sasa za kutayarisha Sheria ya Diaspora na amefurahishwa na matayarisho yaliyofikiwa.

“Katika mazungumzo yangu niliyoyafanya na baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wiki iliyopita, tarehe 7 Disemba, 2019, walinieleza kwamba wao wanapenda inakuwa rahisi kwao kujadili na kupitisha sheria kwa masuala ambayo tayari yameshatungiwa Sera”,alisema Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika kuhakikisha masuala ya kuuimarisha ushirikiano wa Wanadisapora na nchi yao ya asili unakuwa endelevu, aliagiza Ofisi yake kutenga  fedha kila mwaka katika bajeti ya Serikali, kwa ajili ya kufanya makongamano hayo ambapo hapo mwanzo yalikuwa yakitegemea michango ya wafadhili.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake na Wanadisapora kwa kuzipokea vizuri juhudi zinazochukuliwa na Serikali zote mbili za kuanzisha Diaspora kwani wamekuwa wakishiriki vizuri katika kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo.

Kwa upande wa Zanzibar, Rais Dk. Shein alitoa shukurani maalum kwa Wanadispora kwa kuishiriki kikamilifu katika kuimarisha Sekta za Afya na Elimu hasa ikizingatiwa kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba imeweka mkazo katika kuziimarisha sekta hizo.

Alitoa shukurani kwa timu ya Wataalamu ya Wanadiaspora walioshiriki katika kuanzisha masomo ya Uzamivu (PHD) ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), ambapo mafanikio yake yamekuwa makubwa na hivi sasa wanafunzi 39 wanafanya (PHD) ya Kiswahili chuoni hapo.

Rais Dk. Shein alitoa wito kwa Wanadiaspora kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha sekta ya elimu na kusomesha wataalamu wazalendo kama walivyoanza ambapo pia, aliwahimiza Wanadiaspora kila watakapopata nafasi wajiendeleze kwa kupata elimu zaidi hasa katika maeneo ambayo yanahitaji wataalamu.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliwatoa hofu Wanadiapora kwamba Jamhuri ya Muunganao wa Tanzania, ikiwemo Zanzibar iko salama na inaendelea kuwa salama wakati wote hivyo, wasiakhirishe matembezi ya kuja nchini na wala wasitaharuk kutokana na uchaguzi ujao.

Alieleza kwamba mara nyingi katika baadhi ya nchi duniani, uchaguzi huandamwa na changamoto mbali mbali zinazopelekea hali ya amani na utulivu kutetereka hivyo, aliwaeleza katika uchaguzi ujao wa hapa nchini vurugu hazina nafasi.

Aliwaleeza kuwa kwa upande wa Zanzibar imeendelea kupokea wageni kutoka mataifa mbali mbali duniani ambao wao hawana hofu na idadi yao imekuwa ikiongezeka kila mwaka sasa haoni sababu kwa Wanadispaora kuwa na hofu kuja kutembea nchini mwao.

Rais Dk. Shein aliwaeleza Wanadiaspora hao kwamba Serikali zote mbili zitayafanyia kazi mapendekezo na maazimio yatakayopitishwa katika Kongamano hilo alilolizindua.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa nasaha juu ya masuala mbali mbali ikiwa ni pamoja na pale inapotokea hali ya maisha kuwa ni magumu katika nchi wanazoishi, wasione tabu kuja kuendelea na maisha hapa nyumbani.

Vile vile, aliwahimiza kuzitumia vizuri taaluma zao na mitaji waliyonayo katika kuwekeza nyumbani licha ya wengi wao kukumbana na changamoto ya usimamizi wakati wanapowekeza hivyo, aliwataka watafute wasimamizi waaminifu na wenye ujuzi na uzoefu katika mambo wanayoyawekeza ili waepukane na ghilba.

Aliwasisitiza kuzitumia vizuri Ofisi zao za Kibalozi na kutafuta ushauri, nasaha na misaada kila wanapohisi wanauhitaji msaada huo, huku akitoa pongezi maalum kwa Ofisi za Kibalozi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika nchi mbali mbali kwa kufanya kazi kwa karibu na kwa kushirikiana na Wanadiaspora katika nchi hizo.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kuandaa Kongamano hilo.

Mapema akimkaribisha Rais, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu alieleza jinsi ya washiriki wa Kongamano hilo wanavyoongezeka kila mwaka na kumpongeza Rais kwa juhudi alizozichukua katika kuhakikisha sula la Diaspora linaimarika hapa nchini.

Nae Mwenyekiti wa Baraza la Diaspora la Watanzania Duniani (TDC Global) Norman Jasson  alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kuwaletea maendeleo Watanzania wote bila ya kujali itikadi, dini au hali zao za kijiografia.

Alitoa salamu za upendo na pongezi kutoka kwa Balozi Dk. Willibrod Slaa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, nchi za Nordic, Baltic States na Ukraine ambaye ndiye mlezi wa Baraza hilo.

Mwenyekiti huyo alieleza umuhimu wa kuwepo kwa Sera ya Diaspora huku akieleza changamoto inayokikumba vizazi vya Diaspora vyenye nasaba ya Kitanzania ambavyo vimetawanyika duniani kote kutokana na Watazania kuolewa na kuoa mataifa mengine na pia Wataznania wenye kuoa au kuolewa wakiwa tayari wamebadilisha uraia.

Alieleza kuwa kizazi hicho ni muhimu sana kwa taifa hilo hata hivyo, kwa sasa wanakuwa na changamoto moja kubwa ambayo wanapokuwa ughaibuni wanahesabika kama ni wageni na wanaporudi nyumbani Tanzania ambako wazazi wao ndipo walipotokea napo wanakuja kama wageni.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira George Simba Chawene kwa niaba ya Waziri wa Mmabo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamangamba Kabudi alieleza hatua zilizofikiwa katika mchakato wa Sera ya Diaspora kwa upande wa Tanzania Bara.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alipata fursa ya kutembelea maonyesho ya Wajasiriamali mbali mbali katika viwanja vya hoteli hiyo pamoja na sehemu maalum ya jengo la hoteli hiyo.

Katika Kongamano hilo mada mbali mbali zimetolewa na Wanadiaspora ikiwemo mada inayohusu Urejeshaji wa Taka za plastiki iliyotolewa na Johnas Singo Diaspora kutoka nchini Norway.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.