Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Ajumuika na Wapiganaji wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama Katika Chakula Maalum Alichowaandalia leo Katika Viwanja vya Polisi Ziwani Zanzibar.S


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameungana pamoja na Wapiganaji wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama walioshiriki katika Maadhimisho ya sherehe za kutimiza miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika chakula maalum cha mchana alichowaandalia.

Chakula hicho maalum cha mchana aliwaandalia kutokana na ushiriki wao kwenye sherehe hizo za miaka 56 ya Mapinduzi zilizofanyika Januari 12 mwaka huu 2020 huko katika uwanja wa Amaan, Mjini Unguja.

Hafla hiyo ya chakula maalum ilifanyika leo katika  viwanja vya Polisi Ziwani Jijini Zanzibar, ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu.

Wengine ni Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Said Hassan Said, Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Washauri wa Rais wa Zanzibar.

Aidha, viongozi wengine pamoja na Wakuu wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Maafisa na Wapiganaji na wanahabari kutoka  vyombo mbali mbali vya habari nao walihudhuria.

Katika shukurani zake Rais Dk. Shein kwa Wapiganaji hao zilizotolewa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Ussi Gavu alitoa pongezi kwa Wapiganaji hao kwa kushiriki kikamilifu katika sherehe hizo adhimu za kutimiza miaka 56 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Waziri Gavu alimpongeza Rais Dk. Shein kwa uongoziz wake madhubuti uliopelekea kuwepo kwa salama, amani, umoja na mshikakamno na utulivu mkubwa ambao umezaa matunda ya maendeleo hapa Zanzibar.

Aliendelea kutoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa muendelezeo wake wa  kuwaandalia chakula maalum cha mchana ambao ni utamaduni aliouweka kila mwaka baada ya kumaliza sherehe za Mapinduzi hatua ambayo inaonesha wazi jinsi alivyokuwa na upendo pamoja na imani kubwa na wananchi wote anaowaongoza.

Alieleza matumaini makubwa yaliopo kuwa kila uchao sherehe hizo zitaendelea kuwa nzuri na kuvishukuru Vikosi hivyo kwa kufanikisha sherehe hizo huku akitumia fursa hiyo kuvipongeza kwa kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulinda amani, utulivu na mshikamano uliopo.

Waziri Gavu alitoa shukurani za dhati kwa vikosi hivyo kwa kuadhimisha kwa hali ya juu kilele cha miaka 56 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Sambamba na hayo, Waziri Gavu alieleza kuwa sherehe hizo za Januari 12, 2020 zilivutia sana ambazo zilikuwa ni kielelezo cha kutosha cha Mapinduzi ya Januari 12.1964 yaliyowakomboa Wazanzibari wote ambayo yataendelea kulindwa, kuenziwa na kutunzwa daima.

Nae Mkuu wa Brigedi ya Nyuk Zanzibari, Brigedia Jenerali Fadhil Omar Nondo  ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama alitoa shukurani na pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuvijali na kuvithamini vikosi vya Ulinzi na Usalama.

Alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendeleza utamaduni wake huo aliouweka wa kila mwaka ambapo mara baada ya sherehe za Mapinduzi matukufu huwandalia chakula maalum cha mchana Wapiganaji na Maafisa hao na kula nao pamoja.

Brigedia Jenerali Nondo alitumia fursa hiyo kumkaribisha Rais Dk. Shein pamoja na viongozi na wageni wote katika eneo hilo la viwanja vya Polisi Ziwani na kueleza kuwa hatua hiyo anayoifanya Rais Dk. Shein  inawachochea kuwa na ari ya utekelezaji wa ulinzi wa nchi,  wananchi wake pamoja na kuyalinda Mapinduzi ya Januari 12, 1964.

Pia, Bregedia Jenerali Nondo alieleza namna ya maandalizi ya gwaride yalivyofanyika hadi kufanikisha sherehe hizo na kutoa shukurani kwa Rais Dk. Shein pamoja na Serikali kwa kusaidia kufanikisha maandalizi yote ya gwaride hilo na kutoa pongezi na shukurani kwa niaba ya Wapiganaji wote walioshiriki katika hafla hiyo adhimu.

Ni utamaduni aliouweka Rais Dk. Shein wa kuwaandalia chakula cha mchana Vikosi vya Ulinzi vinavyoshiriki katika gwaride la sherehe za Mapinduzi pamoja na vijana na Wanafunzi ambao hushiriki sherehe hizo kwa kila mwaka.

Hapo kesho Rais Dk. Shein  amewaandalia chakula cha mchana vijana na wanafunzi  walioshiriki katika maadhimisho ya Sherehe za kutimiza miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar hapo hapo katika viwanja vya  Polisi Ziwani Jijini Zanzibar.

Katika hafla hiyo pia, Kikundi cha Taarab ‘Island Super Star’ maarufu Wajelajela kutoka kikosi cha Mafunzo kilitumbuiza kwa nyimbo zake mwanana zikiwemo zile za kuhamasisha kuyaenzi na kuyalinda Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 pamoja na Brassband ya Jeshi la Polisi ambayo nayo ilitumbuiza katika hafla hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.