Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mette
N. Dissing-Spandet (kulia) akijadiliana jambo
na Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu katika Maktaba ya
THBUB alipokuwa akioneshwa mazingira ya ofisi hizo ambazo zilijengwa kwa msaada
wa Denmark.
Afisa wa THBUB, Omary Limu (kushoto)
akimuonesha Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mette N. Dissing-Spandet baadhi ya tuzo katika maktaba hiyo ambazo tume ilizipata
kufuatia ushiriki wake katika matukio
mbalimbali nchini na nje ya nchi.
Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mette
N. Dissing-Spandet akiongea na Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu
katika mazungumzo yaliyofanyika kwenye ofisi za THBUB jijini Dar es Salaam
mwishoni mwa juma.
Na
Mbaraka Kambona,
Balozi
wa Denmark nchini Tanzania, Mette N. Dissing-Spandet, ameieleza Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora (THBUB) kuwa wataendelea kufanyakazi kwa karibu na
tume kufuatia mahusiano mazuri ya muda
mrefu yaliyojengeka baina ya Denmark na
Tanzania.
Dissing-Spandet
alitoa ahadi hiyo katika mazungumzo yaliyofanyika kwenye ofisi za THBUB jijini
Dar es Salaam mwishoni mwa juma baina yake na Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu
Mathew Mwaimu.
Alisema
kuwa Denmark itaendelea kufanya kazi na THBUB na itaendelea kuisaidia
kutekeleza majukumu yake ya kuhamasisha, kutetea na kulinda haki za binadamu
nchini.
“Denmark
imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na THBUB kwa muda mrefu sasa, na tupo tayari
kuendeleza ushirikiano wetu, tumeweza kufanya kazi kwa karibu kutokana na
mahusiano mazuri ya muda mrefu baina ya nchi zetu mbili”, alisema Dissing-Spandet
Kwa
mujibu wa Balozi huyo, alisema kuwa ni
muhimu katika nchi yoyote kuwa na taasisi kama THBUB kwa kuwa zinasaidia nchi
katika kuhamasisha uzingatiwaji wa masuala ya haki za binadamu na misingi ya
utawala bora.
Mwenyekiti
wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu alionesha kuridhishwa kwake na ushirikiano
ulipo baina ya tume na Denmark na kusema kuwa ushirikiano huo umesaidia sana tume kuweza
kutimiza majukumu yake kwa kiasi kikubwa.
“Tunashukuru
kwa jitihada zenu za dhati za kutuunga mkono, Denmark mmekuwa washirika wa
mwanzo kabisa kuisaidia tume, na kupitia msaada wenu tume iliweza kujenga jengo
hili la Haki House ambalo ndio tumekuwa tukilitumia kama ofisi zetu...Ahsante
sana”, Jaji Mwaimu alimshukuru Balozi huyo
Kamishna
wa THBUB, Nyanda Shuli alisema katika kikao hicho kuwa moja ya mipango ya THBUB
mwaka huu ni kufanya ufuatiliaji wa uchaguzi mkuu utakaofanyika baadae mwaka
huu, na kwamba mpaka sasa wameshaanza kufuatilia mchakato wa daftari la mpiga
kura.
“Miongoni
mwa mipango yetu mwaka huu wa uchaguzi ni kuwa na mikutano ya majadiliano na
wadau mahususi ikiwemo Jeshi la Polisi, Vyama vya Siasa na Tume ya Uchaguzi ili
kukumbushana umuhimu wa kuwa na uchaguzi wa amani nchini”, alieleza Shuli
Ziara ya Balozi huyo kwa tume ni ya kwanza
ambayo ililenga katika kufahamiana na kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya
THBUB na Denmark katika kuimarisha uzingatiwaji wa haki za binadamu na misingi
ya utawala bora nchini.
No comments:
Post a Comment