Habari za Punde

Makala Dkt. Abassi kuendeleza mageuzi Sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo


 Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wakila kiapo cha Uadilifu katika utumishi wa Umma mele ya Katibu Mkuu na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi baada ya kupata Semina elekezi kutoka Ofisi ya Rais, Sekretariat ya Maadili ya Viongozi wa Umma iliyofanyika Februari 07, 2020 jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya kikao kazi cha watumishi wa Wizara hiyo.

Na Eleuteri Mangi-WHUSM, Dodoma
Katika hali ya kawaida mtu anapofanya vizuri hupongezwa kwa kazi nzuri aliyoifanya ndio maana waswahili husema “Chanda chema huvikwa pete”, maana yake mtu anayefanya mema hulipwa mema.

Maneno hayo yanasadifu usemi aliousema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa anawaapisha viongozi mbalimbali February 3, 2020 Ikulu Jijini Dar es Salaam akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Hassan Abbasi Said.

Rais Dkt. Magufuli alitanabaisha utendaji wa Dkt. Abbasi kwa kusema ni mchapakazi anayefanya kazi nzuri ya kuisemea vizuri Serikali bila kuchoka kwa kufuata miongozo mizuri ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe na viongozi wengine kwenye Wizara hiyo.

"Ningependa aendelee kuwa Msemaji wa Serikali, lakini mahali mtu anapotakiwa kupata promosheni usimnyime kwa sababu ni “Motivating Agent” ndio maana tumemteua kuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, na kwa sasa hivi ataendelea kuwa Msemaji wa Serikali mpaka tutakapopata mwingine, na sasa atakuwa anasema akiwa mkubwa zaidi" alisema Rais Magufuli.

Mara baada ya Kuapishwa Dkt. Hassan Abbasi amesema kipaumbele chake ni kufanya mageuzi katika Wizara hiyo kwa kuwa anazifahamu vizuri sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

“Nimeaminiwa tena na Mhe. Rais namshukuru sana ninamuahidi yeye binafsi, Watanzania wote, wadau wa hizi sekta pamoja na wafanyakazi wenzangu pale Wizarani, kwamba tunaenda kuendeleza mageuzi, sio kuanzisha, kwa sababu watangulizi wangu niwashukuru wameanza kazi kubwa, mimi kazi yangu pale itakuwa ni mageuzi katika Wizara ya Habari watu wasubiri mageuzi makubwa.” alisema Dkt. Abassi.

Mara baada ya kwasili wizarani hapo, Dkt. Abbasi alianza kazi kwa kukabidhiwa ofisi na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Ally Possi ambaye alikuwa akikaimu nafasi hiyo baada ya aliyekuwa Katibu Mkuu Suzan Mlawi kustaafu.

“Nimekuta watumishi wazuri sana Wizara hii, nimepata ushirikiano mzuri katika utendajikazi wangu, ni timu nzuri lazima tuiboreshe. Hakika kazi yako ya kuisemea Serikali umeifanya kwa weledi na mapinduzi makubwa sana katika Idara ya Habari ambayo unaendelea kuwa Msemaji wa Serikali, umeipeleka Idara pazuri sana” alisema Dkt. Possi.

Februari 7, 2020 Dkt Abassi alikutana na watumishi wote wa Wizara hiyo waliopo Jijini Dodoma na kubainisha mtarajio yake kwa watumishi hao na kuwahamasisha waendelee kuchapakazi kwa weledi kwa kuzingatia taaluma zao badala ya kuendekeza uvivu, utoro, uchelewaji, majungu, uzandiki na ubazazi.

“Natarajia mtakuwa waadilifu na wazalendo, muipende wizara yenu na nchi yenu na msiruhusu hujuma ya aina yeyote” Alisema.

Natarajia mtakuwa wabunifu katika kazi zenu, mtindo wa kufanyakazi kwa mazoea bila ubunifu hauna nafasi ni vema mtumie taaluma zenu ipasavyo ziwe na tija kwa wadau wetu na nchi yetu” alisisitiza Dkt. Abassi     

Katika kuyafikia malengo ya Wizara na ya Serikali, Katibu Mkuu huyo aliainisha siri sita za kusukuma mbele gurudumu la wizara hiyo kwa kuongozwa falsafa yake ya “Timu Tunatekeleza” inayosimamia kuweka malengo katika kazi na kuyasimamia. Malengo ni dira, bila kuweka malengo huwezi kujua hata unataka kwenda wapi wala utafika lini na kwa njia ipi.

Siri nyingine ni kuweka malengo makubwa, kutekeleza malengo hayo na sio maneno matupu, kuwa na mawasiliano madhubuti ndani na nje ya wizara ili kuyafikia malengo hayo, kuwa na ushirikiano baina ya menejimenti, watumishi na wadau wa taasisi pamoja na kuamini nguvu ya Mungu katika kufikia malengo tunayojiwekea kwa kuwa yapo mambo ambayo yanazidi uwezo wa mwanadamu na hapo nafasi ya Muumba ni ya muhimu.

Awali akimkaribisha Katibu Mkuu Dkt. Abbasi kuongea na watumishi hao Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Macelline Patrick alisema lengo la kikao hicho ni kutambulishana pamoja na kutoa ahadi ya uadilifu kwa viongozi na watumishi kwa Kiongozi na Mtendaji Mkuu wa Wizara.

Pia aliongeza kuwa Wizara hiyo ina idadi ya watumishi 224 ambao miongoni mwao wapo Makao Makuu jijini Dodoma na wengine wapo jijini Dar es salaam pamoja na Chuo cha Maendeleo ya Michezo cha Mallya kilichopo mkoani Mwanza.

Kwa upande wake Katibu wa Chama cha Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini (TAGCO) Abdul Njaidi amesema kuwa wamefurahishwa na uteuzi wa Dkt. Abbasi kushika wadhifa Katibu Mkuu kwa kuwa ataendelea kuwa nao katika tasnia ya Habari.

“Ataifanya TAGCO iende hatua za juu zaidi kwa sababu anaijua, siku zote amekuwa akisimamia taaluma na kutaka watu wafanye kazi kwa matakwa ya taaluma zao ili kufikia malengo ya Serikali ya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo 2025” alisema Njaidi.

Aidha, Baada ya kuteuliwa na Rais Ijumaa Januari 31, 2020, baadhi ya wadau wa sekta ya habari wakiwemo Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini pamoja na Wizara na Taasisi mblimbali walitoa pongezi na maoni yao kupitia jukwaa la “WhatsApp” kuhusiana na uteuzi huo.

Baadhi waliandika pongezi zao kwa Katibu Mkuu Dkt. Abassi ambapo Theodos Komba anasema “Hongera Dkt., Mungu aendelee kukubariki katika utekelezaji wako wa majukumu mapya. Tunafuraha kuwa tunaendelea kuwa pamoja”; Nteghejwa Hosea anasema “Hongera Dkt., Mungu ataendelea kukuongoza hata hapo unapoenda sasa;”

Wengine waliotoa maoni yao ni Mtamike Omary anasema “Hongera Dkt., Mwenyezi Mungu azidi kukujaalia hekima na busara nyingi zaidi wakati wote wa uongozi wako, hakika umekuwa nahodha bora sana kwetu;” Peres Muhagaze anasema “Hongera sana Dkt. Hassan Abbas!! Umeitumikia Serikali na Umma kwa ueledi wa hali ya juu ukiwa Mkuruggenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na  Msemaji Mkuu wa Serikali, umeacha alama, tunakuombea ufanye zaidi katika ofisi yako mpya ya Katibu Mkuu wa Wizara na kuendelea ili  kutimiza adhma yako ya ndani ya kuwatumikia Watanzania katika masuala mbalimbali. Mwenyezi Mungu akutangulie katika maukumu mapya”

Aidha, pongezi hizo kwa Katibu Mkuu Dkt. Abassi pia zimetolewa na Wizara na Taasisi mbalimbali ikiwemo Wizara yake anayoiongoza, Wizara ya Maji, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Kampuni ya Magazeti ya serikali Tanzania (TSN) na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA).

Akiwashukuru wadau hao kupitia jukwaa hilo kwa kumpongezi zao, Katibu Mkuu Dkt. Abassi anasema “Team, Kimsingi sina la kusema kwa imani hii kubwa ambayo Mhe. Rais ameendelea kuniamini. Namhuskuru sana sana na zaidi nawashukuru wote kwa salaam.

Ni faraja kwamba bado tuko wote katika sekta ya Habari. Tuanzie hapo tulipoishia. Hii ni Wizara iliyobeba soft power zote za nchi. Nawatakia kasi na utekelezaji mwema wa pale tulipoishia. Nitabaki kuwa mlezi wenu mujarabu. Hakika mmenilea, mmenishauri, mmenisikiliza, mmenivumilia na tumepiga kazi, basi na kazi iendelee. Nyie ni TeamTunatekeleza Tuendelee na kazi Mungu Awabariki.”

Dkt. Abbasi anakuwa Katibu Mkuu wa 26 kuingoza Wizara hiyo akitanguliwa na Makatibu Wakuu 25 tangu nchi yetu kupata Uhuru mwaka 1961 ambapo mnamo mwaka 1964 Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwl. Julius Nyerere aliunda Wizara ya Habari na Utalii ilidumu hadi 1971 ilipoundwa Wizara ya Habari na Utangazaji. Mwaka 1980 Serikali iliunganisha majukumu ya sekta ya Habari na Utamaduni na kuunda Wizara ya Habari na Utamaduni.

Aidha, mwaka 1984 majukumu ya sekta ya Habari na Utamaduni yalihamishiwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Makamu wa Pili wa Rais na na mwaka 1995 hadi 2005 majukumu ya Sekta ya Habari yapohamishiwa tena Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, Sekta ya Habari, Utamaduni na Michezo ziliunganishwa pamoja na kuunda Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo na baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Serikali iliunda Wizara Mpya ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo. Mwaka 2016 Serikali ya Awamu ya Tano iliunda Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michzo ambayo inafanya kazi hadi sasa.

Makatibu Wakuu waliohudumu katika Wizara hii ni pamoja na Bw. A. K. Tibandebage, Bw. B. J. Mkate, Bw. Bernard Mulokozi, Bibi Zahra Nuru, Dkt. Ben Moses, Bw. Daniel Mloka, Mhandisi Paul Mkanga, Bw. Paul Sozigwa, Bw. Wilfred Mwabulambo, Bw. Silvano Adel, Bw. Elly Mtango, Bibi Rose Lugembe, Bw. Raphael Mollel, Bw. Silvanus Odunga, Bw. Abubakari Rajabu, Bw. Kenya Hassan, Bw.  D. Sepeku, Bw.  Raphael Mhagama, Bibi Kijakazi Mtengwa, Dkt. Florens Turuka, Bw.  Sethi Kamuhanda, Bibi Sihaba Nkinga, Prof. Elisante Ole Gabriel na Bibi Suzan Mlawi.    

Dkt Hassan Abbasi Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, ameshika wadhifa wa Mkurugenzi wa Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali tangu Agosti 5, 2016 hadi kuteuliwa kwake kushika wadhifa huo Januari 31, 2020 na kuapishwa Februari 03, 2020 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Alizaliwa wilayani Korogwe, Tanga mwaka 1978 na kupata elimu yake ya msingi katika Shule ya Msingi Hale kati ya mwaka 1988 na 1994. Alimaliza akiwa mmoja wa wanafunzi waliofanya vizuri mkoani humo na kujiunga na Sekondari ya wanafunzi wenye vipaji maalum ya Tabora Wavulana (Tabora School) mwaka 1995 kwa masomo ya sekondari. 

Kati ya mwaka 1997 na 1998 alihamia katika Sekondari ya Azania, Dar es Salaam ambapo alimaliza kidato cha nne na kati ya mwaka 1999-2001 alijiunga na Shule ya Sekondari Lindi kwa masomo ya kidato cha tano na sita.

Kati ya mwaka 2002 na 2006 alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo alichukua shahada ya kwanza ya sheria (LL.B). Akiwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu pia aliajiriwa kama mwandashi wa habari wa kujitegemea katika kampuni ya Business Times na baadaye kushika nafasi mbalimbali kuanzia mwandishi mwandamizi, mhariri msaidizi hadi mhariri Mkuu katika magazeti ya Majira na Kulikoni.

Mwaka 2005 akiwa bado mwanafunzi, alichaguliwa kuwa Mhariri Mkuu wa Jarida liitwalo “Nyerere Law Journal” linalochapishwa na Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Kati ya mwaka 2007 na 2008 alihudhuria masomo ya uandishi wa habari ndani na nje ya nchi ikiwemo makao makuu ya Reuters, London, Uingereza na Chuo Kikuu cha Maine nchini Marekani.

Mwaka 2010 aliajiriwa Serikalini akiwa Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano katika Mpango wa Afrika Kujitathmini Kiutawala Bora (APRM) tawi la Tanzania, programu iliyoko chini ya Wizara ya Mambo ya Nje, ambapo kabla ya mwaka 2014 alikuwa Meneja Mawasiliano katika Ofisi ya Rais, Kitengo cha Matokeo Makubwa Sasa (BRN).

Aidha, ana taaluma ya Sheria ambapo ana hadhi ya Wakili wa Mahakama Kuu tangu mwaka 2011, Dkt. Abbasi pia ana diploma ya uzamili katika usimamizi wa mahusiano ya kimataifa (PGD-MFR) kutoka Chuo cha Diplomasia cha Msumbiji na Tanzania, Kurasini, shahada ya uzamili katika mawasiliano kwa umma (MA Mass. Comm., SAUT) na shahada ya uzamivu katika mawasiliano kwa umma (Ph.D Mass. Comm., SAUT).

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.