Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe Zungu Ikulu Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Azzan Zungu, alipofika Ikulu Jijini Zanzibar. Kujitambulisha na kufanya mazungumzo. 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akimsikiliza Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Azzan Zungu alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha leo 14-2-2020.


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amemuhakikishia kumpa mashirikiano makubwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira Mussa Azzan Zungu ili aweze kutekeleza vyema majukumu yake hasa yale yanayohusu Muungano.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira Mussa Azzan Zungu ambaye ameteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ili kushika wadhifa huo.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alimueleza Waziri huyo kuwa yeye mwenyewe pamoja na viongozi wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Mawaziri wake watahakikisha wanampa mashirikiano makubwa Waziri huyo ili aweze kutekeleza vyema kazi zake.

Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa miongoni mwa majukumu yake makubwa aliyonayo moja wapo ni kuhakikisha jitihada za waasisi wa Taifa hili Hayati Mzee Abeid Amani Karume na Hayati Julius Kambarage Nyerere za kuleta Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zinaendelezwa na zinadumishwa.

Aliongeza kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umeleta mafanikio makubwa hasa ikizingatiwa kwamba walioungana ni wananchi wa pande mbili ambao wana udugu wa asili na historia ya muda mrefu.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza matarajio yake makubwa aliyonayo kutokana na utendaji kazi na uzoefu alionao Waziri huyo ukiwemo uzoefu wa utumishi Serikalini  pamoja na ule wa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pamoja na hayo Rais Dk. Shein alieleza kuwa mapenzi udugu wa wananchi wa pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni vyema ukaimarishwa na kudumishwa sambamba na kuendeleza mashirikiano yaliopo ya kihistoria.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira Mussa Azzan Zungu alitoa shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwa kupata uteuzi huo ambao aliahidi kuufanyia kazi kwa ufanisi pamoja na kuutendea haki.

Waziri Mussa Azzan Zungu ambaye alikuwa amefuatana na Mkurugenzi wa Muungano Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, alimueleza Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha umoja, mshikamano, upendo na udugu uliopo kati ya Serikali, wananchi na viongozi wa Zanzibar na Tanzania Bara unadumishwa na kuendelezwa kwa manufaa ya Taifa lao.

Sambamba na hayo, Waziri  Mussa Azzan Zungu alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha changamoto ndogo ndogo zinazowasumbua wananchi hususan wafanyabiashara zinafanyiwa kazi changamoto ambazo husababishwa na baadhi ya watendaji.

Alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha anaendeleza na kuzidisha mashirikiano yake na viongozi wakiwemo Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuhakikisha majukumu yake anayatekeleza vyema kwa azma ya kupata mafanikio katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Waziri Mussa Azzan Zungu ambaye pia, ni Mbunge wa Ilala aliteuliwa na Rais John Magufuli mnamo Januari 23 mwaka huu wa 2020 kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira huku aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo George Simbachawene akiteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani.

Waziri George Simbachawene amechukua nafasi ya Kangi Lugola ambaye uteuzi wake ulitenguliwa na Rais John Pombe Magufuli.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822  
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.