Habari za Punde

Watumishi wa Afya kuongezwa JNIA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalim (mwenye kitambaa kichwani) akiomgea na Waandishi wa Habari wa vyombo mbalimbali vya habari leo alipotembelea Jengo la Tatu la abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), kukagua namna walivyojiandaa kudhibiti maambukizi ya virusi vya Corona vinavyosababisha homa ya mapafu, vilivyoanzia nchini China.


Na Bahati Mollel,TAA
WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalim amesema wataomba kibali cha kuongeza watumishi wa afya kwa ajili ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), ambapo kumekuwa na abiria wengi wanaotoka nje ya nchi.

Mhe. Mwalim aliyasema hayo leo wakati alipotembelea jengo la tatu la abiria – TB3, wakati wa mchana muda wa kuwasili abiria kutoka nchi mbalimbali Duniani, ikiwa ni moja ya lengo la kukagua utayari wa watumishi wa afya na kiwanja hicho kwa ujumla wa kudhibiti homa ya mapafu inayosababishwa na virusi vipya vya Corona 2019.

“Nimejionea abiria ni wengi sana na wataalam wetu ni wachache inahitajika waongezwe kwa haraka ili waweze kuwahudumia kwani wengi wanawasili kwa wingi kwa ndege za mchana kunakuwa na msongamano usiokuwa wa lazima” alisema Mhe.  Mwalim.

Pia amesema ameweza kukagua maeneo ambayo abiria atakayebainika kuwa na homa hiyo ya mapafu na kugundua kwa sasa chumba kipo kimoja na hakitoshelezi jinsia zote mbili, hivyo anaangalia uwezekano wa kupatikana kwa chumba kingine cha pili.

“Ninaishukuru Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania kwa kushirikiana vyema na Kitengo cha afya cha hapa JNIA, maana wameweza kuweka vifaa muhimu ikiwemo dawa maalum ya kunawa mikono kwa abiria anapowasili tu, na endapo atakuwa na virusi hivyo vinakuwa vimedhibitiwa kwa kiasi fulani,” amesema.

Ila ameagiza sasa kutengwe eneo maalum patakapowekwa vifunika pua na mdomo (masks) kabla ya abiria kutoka eneo la kiwanja cha ndege na baadaye vikatekelezwe kwa moto, kwa kuwa abiria wanakuwa wamesafiri navyo kwa safari ndefu wawapo ndani ya ndege hadi wanapowasili.

Halikadhalika ameagiza fomu maalum za kujua maelezo mbalimbali ya abiria sasa zijazwe ndani yandege ili kuepuka msongamano wa abiria katika eneo wanalotumia kujazia.

Akizungumzia hali ya homa hiyo kwa Tanzania, amesema hakuna mgonjwa aliyegundulika kuwa na virusi hivyo, kwa mipaka yote ambayo inaingiza watu wa mataifa mbalimbali wakiwemo Watanzania wenyewe.

Hatahivyo, Mhe. Mwalim ametoa angalizo kwa wananchi kuwa wakiona dalili za ugonjwa huo ambazo ni kukohoa, homa kali, nimonia, kupumua kwa tabu, kutapika na kuharisha wawahi vituo vya afya kupima afya zao kabla hali haijawa mbaya zaidi kwani virusi vinadumu kwa siku 14 na dalili kuanza kuonekana.

Naye Kaimu Meneja wa TB3, Mhandisi Barton Komba amesema watatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Mhe. Waziri kwa kushirikiana na wadau wengine wanaohusika na abiria yakiwemo mashirika ya ndege na kitengo cha afya kilichopo kiwanjani hapo.

“Kama mlivyoona Mhe. Waziri wa afya amekuja kutembelea na kuja kuangalia miundombinu ya viwanja vya ndege kwa kuwa ni moja ya mipaka japokuwa kuna changamoto za hapa na pale na sisi tutatekeleza, tutaongeza maboresho yote,” Amesema Mhandisi Komba.

Mbali na China ulipoanzia ugonjwa huu nchi nyingine zilizoathirika na homa hii ni pamoja na Thailand, Australia, Marekani, Singapore, Malaysia, Japan, Korea Kusini, Ufaransa, Canada, Vietnam, Ujerumani, Nepal, Sri-lanka na Cambodia. Hata hivyo, kasi ya maambukizi ya virusi vya Corona sasa ni tishio hadi Barani Ulaya.

Corona ni kundi kubwa la aina ya virusi, ambavyo huweza kumuathiri binadamu na wanyama, ukubwa wa maambukizi unahusisha homa za kawaida pamoja na homa kali na wakati mwingine matatizo katika mfumo wa upumuaji.

Namna mtu anavyoambukizwa homa hii ni pamoja na kugusana moja kwa moja bila kinga na muathirika; kushika kwa mkono vifaa vya muathirika na baadaye kushika mdomoni au puani, ambapo virusi husambaa kwa kasi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.