Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Maofisa Wadhamini wa Wizara Pemba wakati wa ziara yake, mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Chakechake Pemba.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amewataka Maafisa Wadhamini kisiwani Pemba kufanya kazi ya
kukabiliana na maafa kwenye maeneo ambayo wananchi wameathirika hasa
ikizingatiwa kwamba kazi hiyo haina Afisa maalum bali wote wanatakiwa
kuwajibika.
Rais Dk. Shein
aliyasema hayo leo huko Ikulu ndogo, Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba, wakati
alipofanya mazungumzo na Maafisa Wadhamini wa Wizara za Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar wanaofanya kazi zao Pemba ikiwa ni miongoni mwa ziara yake ya siku
tatu kisiwani humo.
Rais Dk. Shein
aliwasisitiza viongozi hao kuzifanyia haraka tathmini za maafa kwa kila Wilaya
yakiwemo maeneo ya vijijini ili kujua nani anatakiwa kusaidiwa ili shughuli
hizo zifanyike ipasavyo na kwa muda muwafaka.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein aliwataka viongozi hao kuwa mstari wa mbele katika kushirikiana na
Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar ikiwa ni pamoja na kupambana na
maradhi yanayosababishwa na virusi vya Corona.
Dk. Shein aliwapongeza
viongozi hao kwa kufanya kazi nzuri ya kupambana na maradhi yanayosababishwa na
virusi vya Corona kwa kushirikiana na Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa
Zanzibar na kusisitiza kuwa hilo ni jukumu la sekta zote za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar.
Alieleza kuwa jukumu
la kupambana na maradhi yanayosababishwa na virusi vya Corona si la Wizara ya
Afya pekee, bali ni la taasisi zote na kueleza kuwa kazi ya kupambana na
maradhi hayo inafanywa vizuri na viongozi wa Pemba hivyo, ni vyema wakaendelea na
mfumo huo.
Kwa upande wa maafa
yaliyosababishwa na athari za mvua za Masika zinazoendelea, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa mvua ni neema ila kuzidi kwake kiwango ndiko kulikopelekea maafa
hayo ikiwa ni pamoja na kuanguka kwa nyumba za wananchi na kuwataka viongozi
hao kufanya kazi kwa kusaidia kwani hiyo ni kazi ya jamii na wote wanahusika.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliwataka Maafisa hao Wadhamini kutokaa maofisini tu na badala yake
waendee katika maeneo yao ya kazi kwa maslahi ya wananchi na serikali kwa
jumla.
Aidha, alisema
kuwa hali ya nchi ni nzuri na ina
utulivu mkubwa ambapo Serikali zote mbili zinaendelea kusimamia vyema amani na
utulivu pamoja na kulinda mipaka yake na kuvipongeza vikosi vya ulinzi na
usalama kwa kulisimamia hilo.
Aliongeza kuwa
maendeleo yaliopatikana hapa nchini yanatokana na amani na utulivu mkubwa
uliopo hivyo, ni lazima yasimamiwe kwa ari na kasi kubwa na kueleza matumaini yake kuwa amani iliyopo nchini itaendelea kulindwa kwa nguvu
zote.
Rais Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kueleza hatua zinazochukuliwa na Serikali zote mbili katika
kukaabiliana sambamba na kupambana na maradhi yanayosababishwa na virusi vya
Corona.
“Matumaini yetu
maradhi haya yanayosabahishwa na virusi vya Corona yatamaliza kwani juhudi zetu
pia zinahitajika na Mwenyezi Mungu atatusaidia........hakuna dhiki wa dhiki
bali baada ya dhiki ni faraji”, alieleza Dk. Shein
Aidha, Rais Dk. Shein
aliendelea kusisitiza kuwa hofu ni mbaya sana hivyo, aliwataka viongozi hao
kuwaondoa hofu wananchi pamoja na kujiondoa hofu wao wenyewe.
Alisema kuwa katika
kupambana na maradhi hayo hakuna haja ya kuvunjana moyo na wale wote waliougua
na wanaoendelea kuugua maradhi hayo wapewe faraja na wasinyanyapaliwe.
Alieleza kuwa ni vyema
wananchi wakaendelea kumuomba Mwenyezi Mungu kuyapeperusha maradhi hayo
sambamba na kuendeleza juhudi za kupambana nayo.
Aidha, Rais Dk. Shein
alisema kuwa maradhi yanayosababishwa na virusi vya Corona yameleta changamoto
ikiwemo maradhi yenyewe sambamba na changamoto ya kiuchumi hapa nchini na dunia
nzima kwa jumla.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haijatetereka kiuchumi licha ya kuwepo
kwa maradhi hayo na kila lililopangwa linatekelezwa ipasavyo kwa azma ya Serikali ya kuwahudumia wananchi wake wote.
Akitolea mfano ujio wa
watalii ambao husaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha uchumi kwa kuingiza
asilimia 80 ya fedha za kigeni, Rais Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa haupo na
kile kilichokuwa kikipatikana hakipo lakini Serikali ipo na inaendelea kufanya
kazi zake kama kawaida.
Aliongeza kuwa
Serikali haijafunga mikono na inafanya kazi na inakwenda vyema na shughuli
zinafanywa na kila mmoja anapata haki yake ya msingi. “tunaendelea na shughuli
zetu na serikali inaendelea kufanya shughuli zake za maendeleo”.
Aidha,Dk. Shein
alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar inaendelea na ujenzi wa jengo
jipya la uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume (Terminal III), na wajenzi wake
wanaendelea kulipwa na miradi yote ya Maji na Usafi wa Mazingira (ZUSP) Unguja
na Pemba inaendelea vizuri sambamba na ujenzi wa maduka makubwa Michenzani
ambayo yanatarajiwa kukamilika hivi karibuni.
Aidha, alieleza kuwa
miradi yote ya ujenzi wa barabara, mipango uya ujenzi wa bandari ya Mpiga Duri,
bandari ya mafuta na gesi Mangapwani sambamba na ujenzi wa Uwanja wa ndege wa
Pemba iko pale pale ambapo katika bajeti ijayo ya fedha imepangwa kuanza utekelezaji
wa ujenzi wa uwanja huo wa ndege wa Pemba.
Rais Dk. Shein
aliongeza kuwa Mipango ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu 2020 uko pale pale na Tume
ya Uchaguzi itatangaza tarehe wakati utakapofika.
Alieleza kuwa wapo
baadhi ya wananchi waliodhania kuwa uchaguzi umeaghirishwa jambo ambalo halipo
na kusisitiza kuwa uchaguzi upo na utatangazwa na Tume husika wakati
utakapofika ndani ya mwaka huu mnamo mwezi wa Oktoba.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alisema kuwa bado Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajiweza na kwa
yeyote aliyekuwa na nia ya kuisaidia anakaribishwa lakini bila ya kuiwekea
masharti Serikali kwani haiko tayari kusaidiwa kwa masharti.
Aidha, Rais Dk. Shein
aliwaeleza viongozi hao kuwa miezi iliyobaki kabla ya uchaguzi mkuu mwaka huu
ni miezi ya kuzidisha utendaji wa kazi na sio kufanya kazi kwa mazoea na
kuwataka kufanya kazi kwa juhudi na maarifa pamoja na kuwasimamia wale wote wanaowaongoza.
Dk. Shein alisisitiza
kuwa Bajeti ijayo ni lazima ifanywe vizuri kwa kusimamia kwa kasi mipango itakayopangwa
na Serikali na kuwataka viongozi hao kuondoa muhali na kujuana katika utendaji
wa kazi kwani kwenye kazi hakuna udugu wala urafiki.
Aliongeza kuwa katika
kazi hakuna muhali na kusisitiza kuwa asiyefanya wajibu wake ipasavyo
ashughulikiwe kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za kazi bila ya kuwaonea
wafanyakazi.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein aliwakata viongozi hao kusimamia kazi na kuondokana na tabia ya
kulaumiana na kushutumiana na badala yake wafanye kazi kwa kushirikiana kwa
azma ya kufikia malengo yaliokusudiwa.
Aliwataka viongozi hao
kujenga utaratibu wa kuambizana ukweli katika vikao vyao na kuvitumia vikao
hivyo kama ni sehemu ya usuluhishi wa changamoto zinazojitokeza katika maeneo
yao ya kazi kwani huo ndio utawala bora.
Aliwataka viongozi hao
kuzifahamu Sheria za Utumishi wa Umma sambamba na Kanuni zake huku akiwataka
kuendelea kuwa wamoja na kuwa na mapezi miongoni mwao.
Rais Dk. Shein
aliwataka viongozi hao kusimamia maadili ya viongozi wa Umma ikiwa ni pamoja na
kupambana na rushwa na uhujumu wa uchumi.
Rais Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kuwakumbusha viongozi hao maagizo ya muda mrefu aliyoyatoa
ambayo yamechelewa kutekelezwa katika maeneo mbali mbali kiswani humo na kutoa
muda maalum yawe tayari yamekamilika.
Aliongeza kuwa hakuna
mbadala wa kazi hivyo, aliwataka viongozi hao kufanya kazi kwa bidii, maarifa
na ubunifu mkubwa ili Zanzibar iendelee kupata maendeleo endelevu.
Nao viongozi hao
walitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa hatua yake hiyo ya kufanya mazungumzo
nao na kuahidi kuwa maelekezo aliyowapa watayafanyia kazi sambamba na kuzidisha
kasi ya uchapaji kazi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment