UMOJA wa Wawakilishi Wanawake Zanzibar (UWAWAZA) umempongeza Mke wa Rais wa
Zanzibar Mama Mwanamwema Shein kwa kushirikiana nao kikamilifu katika hafla ya
kuvunjwa kwa Baraza la Tisa la Wawakilishi hivi karibuni.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wawakilishi
Wanawake Zanzibar (UWAWAZA) ambaye pia ni Naibu Spika wa Baraza la
Wawakilishi Zanzibar Mgeni Hassan Juma
akitoa pongezi kwa niaba ya Umoja huo huko Ofisini kwake Chukwani, Jijini la
Zanzibar alisema kuwa wanampongeza Mama Shein kwa kuujali mwaliko waliompa na
kuweza kushirikiana nao kikamilifu katika hafla hiyo.
Mwenyekiti huyo wa Umoja huo alieleza kuwa
(UWAWAZA) pamoja na viongozi wengine wote wanaume wa Baraza la Wawakilishi la
Zanzibar wamefurahishwa sana na ujio wa Mama Shein katika hafla hiyo adhimu na
kusisitiza kuwa wanatoa pongezi zao za dhati kwa Mama Shein.
Alieleza kuwa Mama Shein amekuwa mstari
wa mbele katika kushirikiana na Wajumbe wa Baraza hilo ukiwemo Umoja wa
Wawakilishi Wanawake Zanzibar (UWAWAZA), ambao amekuwa akiuthamini pamoja na
wajumbe wake wote.
Aliendelea kumshukuru na kumpongeza Mama
Shein kwa ushirikia wake mkubwa katika shughuli mbali mbali za kimaendeleo
zikiwemo za kijamii, kisiasa na kiuchumi Unguja na Pemba.
Aliongeza kuwa Mama Mwanawema amekuwa
akishirikiana nao katika shughuli mbali mbali za kisiasa Unguja na Pemba ikwia
ni pamoja na kushiriki kikamilifu katika kuwanga mkono akina mama katika Umoja
wao wa Wanawake Tanzania (UWT) hapa nchini.
Aidha, alieleza kuwa Umoja huo
unampongeza Mama Shein kwa misaada yake mbali mbali anayotoa kwa jamii na
kusisitiza kuwa Umoja huo unathamini sana michango na misaada yake hiyo anayoitoa
kwa jamii bila ya kujali rangi, dini, jinsia, itikadi wala wapi mtu anatoka.
Mwenyekiti huyo wa (UWAWAZA), kwa niaba
ya viongozi wenziwe wa Umoja huo alimuelezea Mama Shein kuwa alikuwa kiungo
kikubwa sana katika maendeleo ya Zanzibar yakiwemo ya kisiasa kwani amekuwa
akimpa moyo sana Rais Dk. Shein katika shughuli zake mbali mbali za kisiasa.
Sambamba na hayo, Mwenyekiti huyo
alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kumpongeza na kumshukuru Mama
Mwanamwema Shein katika hotuba yake ya kuvunjwa kwa Baraza la Tisa la
Wawakilishi aliyoitoa hivi karibuni huko katika ukumbi wa Baraza hilo, Chukwani
nje kidogo ya Jijini Zanzibar.
Naibu Spika huyo wa Baraza la Wawakilishi
Zanzibar ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja huo wa (UWAWAZA) alisisitiza kuwa
akina mama wamekuwa na mchango mkubwa sana katika maendeleo ya wanaume na
kumuelezea Mama Shein jinsi alivyoshirikiana na Rais Dk. Shein katika kipindi
chake chote cha uongozi.
Alisisitiza kuwa katika uongozi wa Rais
Dk. Shein maendeleo makubwa yamepatikana katika sekta zote za maendeleo
zikiwemo zile za kiuchumi, kisiasa na kijamii na kueleza kuwa kiongozi huyo
ameonesha mfano mkubwa wa kiongozi bora mwenye uongozi uliotukuka.
No comments:
Post a Comment