Habari za Punde

Rais Dk Hussein Mwinyi atembelea Soko la samaki la Kimataifa la Kasenda Wilayani Chato

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe Dk. Hussein Ali Mwinyi akitembelea Soko la Kimataifa la Dagaa Kasenda akiwa katika ziara yake Mkoani Geita Wilaya ya Chato na (kushoto kwa Rais) Waziri wa Uvuvi na Mifugo Mhe. Mashimba Ndaki na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa ziara yake ya kulitembelea soko la samaki la Kimataifa la Kasenda Wilayani Chato, amejifunza mambo mengi ambayo wananchi wa Zanzibar wanaweza kuanzishiwa ili na wao wakaweza kuuza bidhaa zao za uvuvi na kupata tija.

Rais Dk. Hussein Mwinyi ameyasema hayo leo wakati akiwasalimia wananchi na viongozi wa Kitongoji cha Kasenda  na vijiji vya jirani Wilayani Chato, Mkoa wa Geita mara baada ya kulitembelea soko lao la samaki la Kimataifa la Kasenda ambapo aliungana pamoja na Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa amefurahishwa na hatua hiyo kwa kuanzisha soko la Kimataifa kama hilo hasa ikizingatiwa kwamba hata kwa upande wa Zanzibar wapo wafanyabiashara kama hao wa dagaa wanaouza bidhaa hiyo huko Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Zanzibar imeanza Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambapo vyama vimeungana na kuunda Serikali kwa kupitia  Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho ndio chama chake na Chama cha ACT Wazalendo chama cha  Maalim Seif Sharif Hamad.

Aliongeza kwamba wananchi wa Zanzibar wamo katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hivi sasa tofauti za kisiasa zimeondolewa kwani wameona umuhimu wa kuunganisha watu na hivi sasa Wazanzibari wote wamekuwa wamoja na wako tayari kuchapa kazi ili wajiletee maendeleo.

Rais Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais Magufuli kwa kusimamia na kuhakikisha hilo limewezekana kwa upande wa Zanzibar kwani yeye kama Mwenyekiti wa (CCM) alikuwa tayari kushirikiana naye katika kuhakikisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa inaundwa na kuweza kuunga mkono juhudi hizo.

Alifahamisha kuwa baada ya kukamilisha Serikali, Zanzibar imekuja na Sera ya uchumi wa buluu ambapo hivi sasa uchumi utajikita na mambo yanayohusiana na bahari ambapo moja katika kazi hizo ni uvuvi, ufugaji wa samaki, utalii pamoja na  utafutaji wa mafuta na gesi asilia.

Alisema kwamba Sera hiyo mpya italeta maendeleo makubwa hasa ikizingatiwa kwamba hivi  sasa wananchi wa Zanzibar wameona haja ya kuachana na malumbano ya kisiasa.

Rais Dk. Mwinyi aliwatakia kila la heri wananchi wa Chato katika kufanikisha uendelezaji wa soko lao hilo kwa miundombinu mipya inayotarajiwa kuwekwa huku akisisitiza kwamba Watanzania wote ni ndugu  hivyo aliwakaribisha wananchi wa Mkoa wa Geita kuja Zanzibar huku akisisitiza kwamba juhudi za kuimarisha biashara zitaendelezwa ili kuwasaidia wananchi kujikwamua kimaisha.

Katika ziara hiyo ya kulitembelea soko hilo la Kimataifa la Kasenda Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi alishiriki ambapo pia, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad alipata fursa ya kuwasalimia wananachi.

Mapema, Waziri wa Mifugo na Uvuvi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mashimba Ndaki alisema kuwa sekta ya uvuvi kwa Tanzania Bara ni moja wapo ya sekta zinazochangia katika kukuza uchumi na kupunguza uamasikini.

Alisema kuwa uzalishaji wa samaki katika Mkoa wa Geita umekuwa ukiongezeka kila mwaka ambapokatika wmaka 2015 kiasi cha tani 18,535.05 za samaki zikiwa na thamani ya TZS Bilioni 76.9 zilivunwa ikilinganishwa na tani 21,188.03 zilizovunwa mwaka 2019 zikiwa na thamani ya TZS Bilioni 102.7.

Aliongeza kuwa katika mwaka 2020 jumla ya mazao ya uvuvi tani 5,755 yenye thamani ya TZS Bilioni 7.3 yalisafirishwa nje ya nchi.

Alisema kuwa soko la Kasenda lina ukubwa wa mita za mraba 11,322 na lilianzishwa mwaka 1995 ambalo ni la pili kwa ukubwa kati ya masoko yote ya samaki yaliopo Ukanda wa Ziwa Victoria ambapo pia, soko hilo lilipandishwa hadhi mnamo mwaka 2017.

Sambamba na hayo, Waziri Ndaki alisema kuwa biashara ya samaki katika soko hilo inahusisha masoko ya ndani ya nchi na yale ya nje ya nchi katika nchi za Rwanda, Uganda, Burundi, Congo DRC, Zambia na Malawi.

Alisema kuwa mazao makuu yanayosafirishwa kwenda nje ya nchi kupitia soko hilo ni dagaa wa ziwa Victoria, furu na sangara waliokaushwa kwa chumvi (kayabo) ambapo biashara kati ya nchi hizo inachangia kuiingizia Serikali mapato kupitia mrahaba wa mauzo ya samaki nje ya nchi.

Aliongeza kuwa soko hilo linanufaisha watu wapatao 12,528 ambao hufanya shughuli zao katika maeneo yanayozunguka Wilaya ya Chato Ukanda wa Ziwa Victoria wakiwemo wafanyabiashara. Huku akieleza mikakati ya kuliboresha soko hilo.

Mapema Waziri wa Nishati Medard Kalimani ambaye pia ni Mbunge wa Chato alimueleza Rais Dk. Mwinyi pamoja na Makamo wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad hatua zinazochukuliwa katika kuimarisha biashara hiyo ya samaki Wilayani humo.

Waziri Kalimani alisema kuwa siku hii ni ya kihistoria ambapo italipa hadhi zaidi soko hilo la Kimataifa kutokana na kutembelewa na viongozi hao kutoka Zanzibar huku akimpongeza Rais Magufuli kwa kuendelea kulipa hadhi soko lao hilo.

Aidha, Waziri huyo alieleza matumaini yake kwamba ziara hiyo itazaa mahusiano na mashirikiano ya kibiashara kati ya wafanyabiashara wa soko hilo na wale wa Zanzibar pamoja na wananchi wa Zanzibar kuweza kutumia samaki hao kutoka soko hilo.

Mapema Rais Dk. Mwinyi pamoja na Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad walipata maelezo kutoka kwa Mwenyekiti wa soko hilo Suleiman Mohammed Said na kumueleza kwamba soko hilo ni la pili katika ukanda huo baada lile la Kirumba Mwanza. 

Mwenyekiti huyo alieleza jinsi ya shughuli za soko hilo zinavyokwenda na kueleza maeneo wanayouza samaki wao ndani na nje ya Tanzania huku wakieleza furaha zao kwa kufikiwa na ugeni huo kutoka Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.