Habari za Punde

Waziri Mhe.Ummy Ataja Fursa za Mikataba ya Kimataifa.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza wakati wa Semina kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya Mazingira iliyofanyika leo Februari 10, 2021 katika Ukumbi wa Msekwa jijini Dodoma. Kushoto ni Naibu Waziri wa Ofisi hiyo Mhe. Mwita Waitara na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Mhe. David Kihenzile.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Mhe. David Kihenzile akizungumza wakati wa Semina kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya Mazingira iliyofanyika leo Februari 10, 2021 katika Ukumbi wa Msekwa jijini Dodoma.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mwita Waitara akifafanua jambo wakati wa Semina kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya Mazingira iliyofanyika leo Februari 10, 2021 katika Ukumbi wa Msekwa jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu  (wa pili kulia), Naibu Waziri katika Ofisi hiyo Mhe. Mwita Waitara (wa kwanza kulia) na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi  Joseph Malongo wakimsikiliza Mbunge wa Buchosha Mhe. Erick Shigongo (kushoto) mara baada ya kumalizika kwa Semina kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya Mazingira iliyofanyika leo Februari 10, 2021 katika Ukumbi wa Msekwa jijini Dodoma. 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu amesema changamoto za uharibifu wa mazingira hazitambui mipaka ya kijiografia, kiutawala, mifumo ikolojia, bioanuai na rasilimali nyingine za mazingira zinavuka mipaka ya nchi moja hadi nyingine.

Waziri Ummy ameyasema hayo hii leo Jijini Dodoma wakati Ofisi yake ikitoa Semina kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya Mazingira ambayo Tanzania ni mwanachama na Ofisi ya Makamu wa Rais inaratibu utekelezaji wake.

Amesema uharibifu wa mazingira katika upande mmoja wa dunia unaweza kuleta athari kubwa sehemu mbalimbali duniani ikiwa ni pamoja na Tanzania, hali inayopelekea kuanzishwa kwa Mikataba ya Kimataifa inayohusu masuala mbalimbali ya hifadhi ya mazingira, kwa lengo la kuweka juhudi za pamoja kukabiliana na changamoto zinazojitokeza na kuendelea kuhifadhi mazingira kwa pamoja kama urithi wa dunia kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

“Ndugu zangu nchi yetu si kisiwa kinachojitegemea tumekuwa tukiunga mkono juhudi hizo kwa kuridhia Mikataba hiyo na itifaki zake, hususan mikataba ile ambayo tunaona kuwa ina maslahi kwa Taifa letu na si kikwazo katika ustawi wa maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii kwa Taifa” Waziri Ummy alisisitiza.

Waziri Ummy amezitaja fursa zipatikanazo kutokana na kuridhia kwa Mikataba hiyo kuwa ni pamoja na upatikanaji wa fedha za utekelezaji wa miradi ya hifadhi ya mazingira na ustawi wa jamii; fursa za ubadilishanaji wa uzoefu na utaalamu katika masuala mahsusi yanayohusu hifadhi ya mazingira.

Fursa nyingine ni pamoja na upatikanaji wa nyenzo na teknolojia mbalimbali zinazochangia katika juhudi za hifadhi ya mazingira na mbinu bora za uzalishaji katika kujiletea maendeleo endelevu duniani.

Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Mhe. David Kihenzile ameishauri Serikali kuangalia namna bora ya kuondoa matumizi ya Zebaki kwa wachimbaji wadogo kutokana na athari zake kwa binadamu kupitia Mkataba wa Minamata.

Katika Semina hiyo Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira wamejengewa uwezo katika Mkataba wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabia Nchi; Mkataba wa Hifadhi ya Bioanuai; Mkataba wa Minamata Kuhusu Zebaki; Mkataba wa Kudhibiti Kuenea kwa Hali ya Jangwa na Ukame na Mikataba ya Kimataifa ya Udhibiti wa Taka Hatarishi ambayo yote inaratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.