Naibu Waziri Ofisi ya Makamu
wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Hassan Chande (Kushoto) akipata
maelezo kuhusu za uchimbaji wa makaa ya mawe na hifadhi ya mazingira kutoka kwa
Bw. Edward Mwanga Meneja wa Mgodi wa TanCoal ulipo Mbinga. Katikati ni Mkuu wa
Wilaya ya Mbinga Bi. Aziza Mangosongo
Bw. Ryan Wienard Mkurugenzi
wa Ruvuma Coal Ltd akitoa maelezo ya shughuli za uchimbaji makaa ya mawe mgoni
hapo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad
Hassan Chande na ujumbe wake. Naibu Waziri Chande yuko Mkoani Ruvuma kukagua
uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.
Na Lulu Mussa Ruvuma
Serikali imesema uwekezaji
wowote ni lazima uzingatie Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 na Kanuni zake
ikiwa ni pamoja kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira kwa kuwa ni takwa la
Kisheria.
Hayo yamesemwa leo Wilayani Mbinga na Naibu
Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Hassan Chande
mara baada ya kufanya ziara ya kukagua migodi ya uchimbaji wa Makaa ya mawe ya
Tancoal Ltd na Ruvuma coal.
Katika ziara hiyo Naibu Waziri Chande ametoa
siku 14 kwa Mgodi wa Tancoal kudhibiti maji taka katika mabwawa yao pamoja na
kudhibiti vumbi ambalo limekuwa kero kwa wakazi wa maeneo ya jirani.
"Mazingira ndio uhai wetu, tuyatunze na
tuyalinde kwa gharama yoyote ile" Chande alisisitiza.
Chande ameshuhudia ukataji wa miti kwa kiwango
kikubwa katika migodi hiyo na kuwaagiza migodi yote miwili kuandaa mpango wa
muda mfupi wa upandaji miti ili kurejesha uoto wa asili.
Aidha, Naibu Waziri Chande ameagiza migodi hiyo
ya makaa ya mawe kuhakikisha wanaanda na kutekeleza mpango madhubuti wa
kurejesha ardhi katika hali ya awali mara baada ya shughuli za uchimbaji
kukamiika ikiwa ni pamoja na kupanda miti kwa wingi.
"Upandaji miti uwe ni utamaduni wetu, hapa
mgodini miti mingi imekatwa, wekeni mkakati wa kuirejesha kipindi cha
mvua" Chande aliagiza.
Katika hatua nyingine Waziri Chande amemuagiza
Meneja wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Kanda ya Kusini
Bw. Jamal Baruti kufanya kaguzi za mara kwa mara ili kuhakikisha masuala ya
Uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira yanakuwa endelevu.
Akiwasilisha taarifa ya Wilaya ya Mbinga Mkuu wa
Wilaya hiyo Bi. Aziza Mangosongo amesema jitihada na mikakati mbalimbali
imechukuliwa katika kudhibiti vitendo vya uchafuzi na uharibifu wa mazingira
unaosababishwa na shughuli za uchimbaji wa madini kwa kufanya ufutiliaji na
usimamizi wa mara kwa mara kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya
mwaka 2004.
Uchimbaji, uchakataji na uuzaji wa madini ya
makaa ya mawe Wilayani Mbinga zilianza mwaka 2012 kupitia Kampuni ya TanCoal
Energy Ltd na siku za hivi karibuni kumekuwa na ongezeko la Kampuni nyingi
zinazojikita katika utafiti na uwekezaji kwenye sekta ya madini.
No comments:
Post a Comment