Na Maulid Yussuf WEMA
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe Simai Mohammed Said amefanya ziara kuangalia maendeleo ya ujenzi wa Skuli za kisasa za Mpendae kwa bint Hamrani, Kidongochekundu, Mwanakwerekwe pamoja na Masingini.
katika ziara hiyo Mhe Simai amesema ameridhika na hatua ya awali ya ujenzi unavyoendelea.
Akizungumza katika ziara hiyo Mhe Simai amesema amefarajika kuona jamii imejitolea kusaidia kusafisha maeneo hayo ili kurahihisisha ujenzi huo.
Mhe Simai amewataka Wazazi na Walezi kuwasimamia watoto wao hasa katika Skuli ya Kidongo chekundu kwani mazingira ya ujenzi wa Skuli yapo karibu na Skuli ya maandalizi.
Baadhi ya Wanafunzi hawakusita kutoa maoni yao juu ya ujenzi wa Skuli hizo ambapo wameipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kuamua kuimarisha miundombinu ya Elimu kwani itasaidia matumizi mazuri ya ardhi pamoja na kupunguza mrundikano wa Wanafunzi madarasani.
Ujenzi wa Skuli hizo ni miongoni mwa Ujenzi wa Skuli 10 mpya za kisasa pamoja na madarasa mapya 805 na kufanyiwa matengenezo baadhi ya Skuli 22 za Unguja na Pemba, zinajengwa kwa utekelezaji wa mradi wa UVIKO 19 ambapo fedha zake zimepatikana kupitia mfuko wa IMF.
No comments:
Post a Comment