Habari za Punde

Mapishi ya Kizanzibari - Makala


 

MAPISHI YA KIZANZIBARI

 

Adeladius Makwega-DODOMA

 

Mara nyingi nilikuwa mvivu wa kula chakula kwa akina pangu pakavu tia mchuzi kutokana na namna mapishi yake yalivyokuwa yanapikwa, kidogo ilikuwa sijayazoea. Si kwamba mapishi haya yalikuwa mabaya la hasha bali mapishi mengi yalikuwa katika namna nisiyozoea.

 

Mapema mwaka huu 2022 ulianza kwa neema kwa siha yangu kwani walikuja wapikaji wapya, nilijulishwa kuwa wanatokea huko Zanzibar bila ya kufahamu kama walikuwa Wagunya, Washirazi au Watumbatu.

 

Wenzangu waliniambia kuwa ndugu hawa wanapika vizuri sana.

 

“Kichungu huonjwa ”

 

Waswahili husema hivyo, lakini leo mwanakwetu mimi nakwambia, hata kitamu huonjwa pia.

 

Kwa hiyo nilisogelea genge(Mkahawa) la Kizanzibari na kuanza kula. Mapishi haya yalikuwa matama mno, mwanakwetu nilijinoma mno.

 

Chakula chao kilikuwa na kipimo kikubwa na huku wakiweka Nyama, Maharage, Dagaa na Kisamvu.

 

Kisamvu hichi kiliungwa vizuri huku wakikiwekea pilipili kwa mbali.

 

Kwa kuwa walikuwa wananiletea chakula hicho niliwauliza namna wanavyounga Kisamvu chao.

 

“Tunakichemsha, kikiiva tunakitia nazi, kinawekwa maziwa, kinawekwa karanga na kinawekwa viungo vingine kama chumvi, vitunguu maji na vitunguu swaumu kwa kiasi.”

 

Wakati ninaambiwa mapishi haya, moyoni nilisema kuwa haya kweli mapishi ya Kizanzibari na yalikuwa yamekamilika kweli kweli. Nikasema Wazanzibari Kidogo wanaweza kupika kama Binti Mkomangi (bibi yangu mzaa baba).

 

Kila siku niliendelea kula chakula hiki huku nikiogopa kulishwa LIMBWATA LA KIZANZIBARI maana Binti Mkomangi aliniambia kuwa ukiwa mwanaume usipende kula sana vyakula vya wanawake mbalimbali, vingine huwa haviliki, ukionja tu hauwezi kuviacha milele.

 

“Usipende kula vyakula vya wanawake mbalimbali, vingine huwa haviliki, ukionja tu, hauwezi kuviacha milele.”

 

Niliyakumbuka maneno hayo ya Binti Mkomangi mara mbili mbli kwangu kwani mwaka 2004 wakati nakwenda Isimani-Iringa kuanza kazi bibi aliniambia kuwa Wahehe, Wakinga na Wabena wana LIMBWATA lao linalofahamika kama LITAMBULILA kwa hiyo niwe makini sana.

 

Nikiwa Iringa akina Segito, Semuyala,Semdeke, Sechaula, Semlelwa walinipikia vyakula lakini sikuweza kuvionja kuogopa Litambulila. Lakini sasa mapishi ya Kizanzibari yamenivutia mno nikawa nakula kila siku tangu Januari hadi Machi 2, 2022. Nikiwa naliogopa limbwata la Zanzibari huku sifahamu linaitwaje?

 

Siku ya Jumatano ya Majivu, nilifika kwa akina pangu pakavu tia mchuzi, nikatulia tuli na ilipofika saa sita juu ya alama dada wa Kizanzibari alikuja na chakula chake kuniletea.

 

Nilimjulisha kuwa leo kidogo nina dharura.

 

Binti huyu alijisikia vibaya mno, akitambua kuwa sasa amempoteza mteja wake, nilimwambia kuwa usiwe na shaka mimi bado ni mteja wako lakini leo nina jambo langu.

 

Alipokuja nilipo alikuwa na kikapu chake kikubwa kilichojaa mikeba ya plastiki yenye vyakula, alikaa katika kiti na kuanza kutoa machozi.

 

Binafsi ni muda mrefu kumuona mtu analia jirani yangu, hata mimi hulia sana lakini si hadharani, nikiwa na jambo langu huingia chemba na kutoa machozi yangu, nikitoka nje nanawa uso wangu na kuendelea na maisha kama kawaida.

 

Alipoanza kulia nilijiwa na shaka mno, hapa inakuwaje? akija mtu akimuona binti huyu analia si nitaonekana nimemdhulumu kitu, lakiani nikasema namuachia Mungu jambo hilo.

 

Alilia kwa dakika kama tatu hivi, nilimpa maji akanawa. Nikamuuliza kulikoni?

 

“Ninapokuwa na jambo moyoni mwangu linaniumiza huwa ninalia, nikimaliza kulia jambo hilo huwa limetoka moyoni.”

 

Alisema binti huyu kutoka Zanzibar.

 

Nilimuuliza swali lingine mbona kando ya Mikahawa yenu kuna makambi mengi ya ujenzi huko hakuna wateja?

 

Alisikitika tu akasema kaka kwenye makambi haya hakuna wateja na wala hakuna watu. Mwanzoni tulitarajia kuwa kuanza kwa ujenzi huu makambi haya yangeongeza wateja lakini sasa hakuna.

 

Binti huyu huku hasira yake ikiwa inapoa ya kupoteza wateja nilimchokoza nikamwambia sasa si ukawashitakie kwa Mama Samia kuwa makambi hayana watu ili wakija upata wateja.

 

Binti huyu alicheka sana, akasema we waache tu, nitafanya hivyo, umenipa hekima kubwa.Binti huyu aliondoka na kikapu chake cha chakula kurudi mkahawani.

 

Mwanakwetu tangu siku hiyo binti huyu wa Kizanzibari nilipompa hekima ya kuwashitakia sijamuona tena.

 

Swali ni Je amekwenda kushitaki?

 

Mie sifahamu.

 

Nakutakia siku njema.

 

makwadeladius@gmail.com

0717649257


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.