Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema suala la ukodishwaji wa
visiwa kwa jili ya uwekezaji wa utalii ni njia moja ya kuhakikisha inavitumia
visiwa hivyo kwa kuchangia ukuaji wa pato la taifa pamoja na kuzalisha ajira
kwa vijana
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi Afisi ya Rais - Kazi, Uchumi na Uwekezaji Mhe. Mudrick Ramadhan wakati akijibu maswali ya wajumbe wa baraza la wawakilishi kuhusu adhma ya serikali ya kuamua kuvikodisha visiwa kwa ajili ya uwekezaji wa utalii, katika kikao cha kumi na tisa mkutano wa saba wa baraza la kumi la wawakilishi Chukwani mjini Unguja
Amesema serikali ya awamu ya nane kwa mujibu wa thamini ya serikali katika kuvikodisha visiwa hivyo imeonyesha kuwa uwekezaji huo utainufaisha Zanzibar katika ukuwaji wa uchumi kwa kuingiza fedha nyingi pamoja na kuzalisha ajira nyingi kwa vijana tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo visiwa hivyo vilikuwa vikitumika kwa matumizi ya kawaida ambayo hayakutoa mchango mkubwa kwa taifa
Akizungumzia muda wa kuvikodisha visiwa hivyo kwa wawekezaji kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya mwaka 1992 iliyotungwa na baraza hilo amesema kuwa kila mwekezaji atakaepata fursa ya kuwekeza kwenye visiwa hivyo atakodishwa kwa muda wa miaka thalathini na tatu ikiwa ni awamu ya kwanza ya uwekezaji wake
Pia Waziri Soraga amesema Seriali kwa kushirikiana na taasisi zake imewashirikisha kikamilifu wananchi wanaofanya shughuli zao za kimaisha katika visiwa vilivyopangwa kwa ajili ya kukodishwa ili kutoa uelewa kwa wananchi ambapo serikali imewahakikisha wananchi kuwa wataendelea kufanya shughuli zao katika visiwa hivyo pamoja na kufaidika na uwekezaji huo
Aidha amewashukuru wajumbe wa baraza hilo pamoja na wananchi wote kwa kuendelea kuanga mkono juhudi za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi za kuhakikisha anwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar kufuatia ukodiishwaji wa visiwa hivyo.
No comments:
Post a Comment