Na Masanja Mabula Pemba.
JAMII inayoishi na watu wenye ulemavu wa afya ya akili imeushauri kuwapa nafasi watoto wao kushiriki masuala ya Michezo kwani wanaouwezo mkubwa wa kuitanga nchi kupitia sekta ya michezo.
Akizungumza kwenye bonanza la michezo la watu wenye ulemavu wa akili katika viwanja vya Shaame Mata Wilaya ya Micheweni , Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib aliitaka jamii kuwashirikisha katika masuala ya maendeleo.
Alisema Michezo ya watu wenye ulemavu wa akili inatakiwa kupewa kipaombele kwani ni fursa ya kuweza kuutangaza uatalii wa nchi na hivyo kuchangia pato la nchi.
“Wakati umefika kwa jamii kutowabagua watu wenye ulemavu wa afya ya akili kwa kuhakikisha wanawashirikisha katika masuala mbali mbali ya kijamii yakiwemo ya Michezo”alisisitiza.
Aidha alitumia bonanza hilo kutaka jamii kujiepusha na vitendo vya udhalilishaji na unyanyapaa wa watu wenye ulemavu wa akili kwa kuwapa majina yasiyofaa ambapo kufanya hivyo ni kukiuka misingi na haki za utawala bora.
“Sio jambo jema hawa ndugu zetu wenye ulemavu wa akili kuwapa majina yasiyofaa , kufanya hivyo ni kuwadhalilisha kwani wanayohaki ya kushiriki na kushirikishwa katika masuala ya maendeleo”alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahya alisema mabonanza ya Michezo kwa watu wenye ulemavu wa akili yatumike kuwaibua na kuwaunganisha na jamii nyengine.
Alisema watoto wenye ulemavu wa akili wanavyovipaji ambavyo iwapo vitaendelezwa vinaweza kuwa ni chachu ya kuweza kufikia maendeleo ya kweli.
Mwenyekiti wa Olimpiki Maalumu Zanzibar - SOZ- Sada Hamad Ali alisema kila mmoja anatakiwa kuwashiriki katika kuwasaidia watoto wenye ulmavu wa akili ili waweze kutumiza malengo yao haa ya kupata elimu na kushiriki kwenye michezo.
No comments:
Post a Comment