Habari za Punde

Nyumba yateketea kwa moto Chukwani

Baadhi ya kuta  za ghala la kuhifadhia vitu vya thamani zilizoungua na moto uliosababishwa na hitilafu ya umeme huko Chukwani  nje kidogo mwa jiji la Zanzibar JanuarI 30,2023
Muonekano wa  Vitu vilivyoteketea na moto  katika ghala la kuhifadhia fenicha uliosababishwa na hitilafu za umeme huko Chukwani  nje kidogo mwa jiji la Zanzibar JanuarI 30,2023

 Mkuu wa Operesheni na Huduma za Kibinadamu,kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar  Haji Faki Hamduni  pamoja na maofisa wake wakifika katika nyumba iliotokea ajali ya moto kwa kuwafariji huko Chukwani  nje kidogo mwa jiji la Zanzibar JanuarI 30,2023 .

 Na Khadija Khamis – Maelezo  Zanzibar  30/01/2023

Nyumba moja imeteketea kwa moto katika maeneo ya chukwani  nje kidogo na mji wa Zanzibar na vitu kadhaa vimeungua na hadi sasa haijajulikana  gharama ya vitu hivyo.

Akizungumza na waandishi wa Habari Mkuu wa Operesheni na Huduma za Kibinadamu, kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar  Haji Faki Hamduni  Alisema chanzo cha moto huo ni hitilafu ya umeme iliyoanza kwenye kisambazaji cha umeme  (Main switch) iliopo katika ghala la kuhifadhia vifaa vya nyumbani.

Amewataka wananchi kuchukua tahadhari hasa katika kipindi hichi cha kiangazi chenye upepo na joto kali na kutoa taarifa mapema  katika taasisi husika mara tu  wanapoona hitilafu ya umeme ili kuweza kunusurika watu na mali zao .

Nae Mkaazi wa nyumba hiyo Abdulhabib Abrahman Said amesema amesikitika na kumshukuru Mwenyezi  Mungu kwa yote yaliyotokea kupata mtihani huo ambao haukuutegemea kutokea.

Alisema  wakati alipotoka nyumbani kuelekea katika harakati zake za Maisha, hakuona  ishara  yeyote ya hitilafu ya umeme na ndani ya nyumba hiyo mlikuwa hamna mtu mwengine.

‘Wakati nipo kituoni nikisubiri dalala akapita jirani yangu na vespa akaniambia wewe vipi mbona uko huku kwako kunaungua moto ndio nikashtuka na kurudi nyumbani na kufika tu nilipiga mayowe kuwaita majirani kuja kunisaidia, kwani ilikuwa asubuhi mapema  majira ya saa 12:45 watu bado hawajatoka nje “alisema Abdulhabib.

Akizungumzia thamani ya vitu vilivyoteketea alisema hawezi kujuwa thamani yake kwa haraka  kwa vile kulikuwa na vitu vingi vya thamani ikiwemo vitanda viwili vya futi sita kwa sita, viti, meza ya kulia ,sofaseti,  mashine ya kufulia, kabati milango miwili na vitu vingine ambavyo hakuweza kuvikariri kwa haraka .

Nae Sheha wa Shehia ya Chukwani Sleiman Mohamed Mwinyi amewataka wananchi wake ikitokea tatizo lolote hasa la moto wapige namba 114 ya Kikosi cha Uokozi na  Zimamoto ili kupatiwa msaada wa haraka .

Hata hivyo Sheha huyo alimpongeza  mfanyakazi wa shirika la umeme kwa kitendo cha ushujaa alichokifanya kutoa msaada wa haraka kukata nyaya za umeme ili kunusuru  athari ya moto kusambaa Zaidi.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.