Habari za Punde

Uzinduzi wa Boti ya Kilimanjaro VIII "Falcon of the Sea"

 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameziomba Kampuni za Bakhresa kupitia sekta ya usafirishaji kuboresha usafiri wa baharini kwa kuanzisha safari maalumu za Pemba – Unguja - Tanga kwa safari za haraka na kila siku.

Alisema Wananchi wa Pemba wamekua na shida ya muda mrefu ya usafiri wa baharini, aliomba wawekewe usafiri wa uhakika ili kuwapunguzia usumbufu huo.

Dk. Mwinyi alitoa ombi hilo alipozindua boti mpya ya kisasa ya Kilimanjaro VIII kwenye viwanja vya Hotel Verde, Mtoni Wilaya ya Mjini.

Alisema, wakati Serikali  ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendeleza jitihada za kuitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto ya usafiri salama na wa uhakika kwa Unguja – Pemba, kipindi hiki kampuni ya Azam iendelee kuwapunguzia usumbufu wa usafiri wananchi wa visiwa hivyo.

“Ombi langu kwenu ni kwamba, tuna uhaba mkubwa wa usafiri wa Unguja na Pemba, ninaomba kwa sababu mumeongeza vyombo basi kuwe na safari maalumu za Unguja na Pemba, wananchi wa Pemba wangependa kutumia muda mfupi, vyombo wanavyotumia sasa vinachukua muda mrefu sana na pia havipo siku zote, tunaomba Azam mtusaidie kupunguza hili tatizo wakati Serikali inajipanga kufanya kwa upande wake”

Alisema, safari za Unguja, Pemba na Tanga ni muhimu kwa kutoa huduma kwa wanachi.

Aidha, Dk. Mwinyi alieleza Serikali inathamini mchango wa sekta binafsi katika utekelezaji wa mipango ya serikali ya maendeleo na ukuzaji wa uchumi.

Alitumia fursa hiyo kuzihakikishia kampunzi za Bakheresa kupata ushirikiano kutoka Serikalini ili miradi waliyowekeza kuona inaleta faida kwao na nchi kwa ujumla.

Katika hatua nyengine Rais Dk. Mwinyi aliziagiza, Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar (ZMA) washirikiane na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini ya Tanzania Bara (SUMATRA), kuongeza ufanisi na kuhakikisha usalama wa vyombo vya usafiri wa baharini unaendelea kuwepo.

Pia alisema Serikali kwa awamu zote za uongozi, imejitahidi kuimairisha miundombinu na mazingira mazuri kwa kutoa huduma bora za usafiri wa baharini pamoja na wajibu wa kusimamia usalama wa abiria na mizigo kwa vyombo vinavyotumia usafiri huo.

Dk. Mwinyi, aliwanasihi wananchi kuacha kutumia vyombo vya usafiri wa baharini visivyozingatia usalama wao na kuacha kutumia bandari bubu kwani kunahatarisha maisha yao na ni kinyume cha sheria.

Akizingumzia ufinyu wa bandari ya Malindi, Rais Dk. Mwinyi alieleza Serikali imechukua jitihada kuimarisha eneo kupunguza msongomano wa abiria kwa kuipatia ufumbuzi wa kudumu changamoto hiyo kwa kutekeleza mradi wa Ferry Terminal katika eneo la Maruhubi kwa kujenga kituo kipya cha kisasa kwa ushirikiano wa Serikali na Sekta binafsi. 

Aidha, Dk. Mwinyi alieleza bandari ya Malindi baada ya shughuli za mizigo kuhamia bandari ya Mangapwani itatengenezwa upya ili iendane na dhamira ya Serikali ya kuufanya Mji Mkongwe na maaneo yake kuwa sehemu maalum ya kuendeleza Sekta ya Utalii.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi na Uwekezaji, Mudrik Soraga alisema Serikali imejipatia mafanikio makubwa kwenye sekta ya uwekezaji na kufanikiwa kuleta wawekezaji wenye mitaji mikubwa ya zaidi ya dola za Marekani 373.5 na tayari imesajiliwa.   

Naye, Mkurugenzi wa Azam Marine, Abubakar Azizi amesema kampuni zao zimewekeza mtaji mkubwa wa zaidi ya dola za Marekano milioni 120 ili kuwafikishia huduma bora Watanzania pamoja na wageni wanaotembelea nchini kupitia sekta zake za biashara.

Alisema boti ya Kilimanjaro VIII “The Falcon of sea” inauwezo wakuchukua abiria hadi 11, 000 kwa siku, ina madaraja ya VIP, Royal na daraja la kawaida.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.