Habari za Punde

Mhe Hemed akagua Miradi ya Ujenzi wa masoko ya Mwanakwerekwe na Jumbi usiku


 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amefanya ziara ya Usiku  kukagua Miradi ya Ujenzi wa masoko ya Mwanakwerekwe na Jumbi Wilaya ya Magharibi “B” kujionea maendeleo ya miradi hiyo.

Mhe. Hemed amesema hatua iliyofikia katika ujenzi wa masoko hayo ni ya kuridhisha ambapo amewataka wakandarasi na washauri elekezi kuongeza kasi ya ujenzi ili kukamilika kwa wakati uliopangwa na ubora wa hali ya juu .

 

Amesema mategemeo ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi kuwa masoko hayo yakamilike mwishoni mwa mwaka huu ili wafanyabiashara waweze kuyatumia kwa shughuli za kujipatia kipato cha kila siku.

 

Aidha amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa miongozo anayoitoa katika miradi hiyo pamoja na upatikanaji wa fedha kwa wakati bila ya ucheleweshaji hatua ambayo inawapa moyo wakandarasi kuwa na kasi ya ujenzi huo.

 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kuwa lengo la kujenga masoko hayo ni kuwawekea mazingira mazuri wafanyabiashara na wananchi ili waweze kufanya biashara zao kwa  usalama wa  afya zao na kuepuka kufanyabiashara katika maeneo yasiyo rasmi.

 

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewaagiza Wakurugenzi wa Manispaa kuhakikisha wanatoa elimu na maelekezo kwa wafanyabiashara juu ya namna bora watakavyoyatumia masoko hayo na kuacha kufanya biashara pembezoni mwa barabara kwani Serikali imetumia gharama kubwa kuyajenga masoko hayo hivyo umakini unahitajika katika kuyatumia na kuyatunza masoko hayo.

 

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa  na Idara maalum za SMZ Mhe. Massoud Ali Moh'd amesema ziara hiyo ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar inaongeza ari na hamasa ya kufanya kazi kwa ustadi wa hali ya juu ili kufiki malengo ya Serikali kuwawekea mazingira mazuri wafanyabiashara.

 

Ameeleza kuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amekuwa akishahuri na kutoa miongozo inayochangia kuharakisha umalizikaji wa ujenzi wa mradi wa masoko hayo.

 

Kwa upande wake msanifu majengo na  mshauri elekezi kutoka Wakala wa Majengo Zanzibar Mhandisi Shadya Fauz Muhamed amemueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa tayari wakandarasi wapo hatua za mwishoni za  kumalizia ujenzi huo na tayari vizimba vimeshaanza kujengwa.


Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)

18/10/2023

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.