Habari za Punde

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Mipango Zanzibar Dkt.Saada Mkuya Azungumza na Mkurugenzi Mtendaji,Uendeshaji -- Benki ya Dunia


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango Zanzibar, Mhe. Dkt. Saada Mkuya Salum, ambaye anaongoza Ujumbe wa Tanzania katika Mikutano ya Mwaka ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), kwa niaba ya Waziri wa Fedha wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Uendeshaji wa Benki ya Dunia (World Bank Managing Director for Operations) Bi. Anna Bjerde, kando ya Mikutano ya Mwaka ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), inayofanyika Jijini Marrakech, nchini Morocco, ambapo wamejadiliana kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo maandalizi ya Mkutano wa Kimataifa wa Tathimini ya Muda wa Kati wa Mzunguko wa 20 wa Benki ya Dunia (IDA20 Medium Term Review) utakaofanyika Zanzibar kuanzia tarehe 6 hadi 8 Desemba, 2023, ukishirikisha wajumbe zaidi ya 250 kutoka mataifa takribani 100 duniani.

Bi. Bjerde, ameishukuru Tanzania kwa kufanikisha Mkutano wa Wakuu wa nchi za Afrika, ulioangazia masuala ya Maendeleo ya Rasilimali Watu (Africa Heads of State Human Capital Development Summit), uliofanyika kwa mafanikio makubwa mwezi julai, jijini Dar es Salaam.

Aliahidi kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha Benki hiyo inaisaidia katika kukabiliana na mabadaliko ya tabia nchi.

Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, anayesimamia nchi za Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Bi. Victoria Kwakwa, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Katibu Mkuu-Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango - Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, na Naibu Katibu Mkuu - Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban.





(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha-Marrakech)

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.