6/recent/ticker-posts

Sioni sababu ya kujiuzulu - Waziri Masoud


WAZIRI wa Miundombinu na Mawasiliano, Hamad Masoud Hamad, amesema kwamba haoni sababu ya kujiuzulu nafasi yake kutokana na matatizo yaliojitokeza katika mikataba ya ujenzi wa jengo jipya la kupokelea abiria katika kiwanja cha ndege cha Zanzibar.

Waziri huyo, aliyaeleza hayo jana wakati akijibu suala la Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe, Ismail Jussa Ladhu, aliyetaka kujua kwanini hajiuzulu yeye na viongozi wa wizara yake waliohusika kusaini mkataba huo ambao umeonekana kuwapo kwa uzembe walioufanya wa kuitia hasara serikali na kusababisha kuweka saini mkataba mwengine.


Suala hilo pia liliulizwa na Mwakilishi wa Jimbo la Kiwani Hija Hassan Hija, na Mwakilishi wa Muyuni Jaku Hashimu Ayoub, waliotaka kujua kama kulikuwa na uzembe ndani ya mikataba hiyo.

Akijibu suala hilo waziri huyo alisema suala la kujiuzulu kwa viongozi wa wizara hiyo halipo kwani kilichofanyika kilikuwa hakitokani na viongozi wa wizara hiyo bali ni mapendekezo yaliotokana na wataalamu wa ujenzi na usanifu wa michoro ya jengo hilo.

Alisema hapo awali serikali ilikabidhiwa michoro ya jengo hilo ikionesha kuwapo kwa mikonga miwili, lakini baadae mjenzi alipokabidhiwa aliona kuwa baadhi ya maeneo yamepewa nafasi ndogo kwa kuwa na vyumba vidogo.

Alisema eneo jengine ambalo lilionekana kuwa na tatizo ni kuokana na ujenzi wa mikonga katika kiwanja hicho ingelikuwa midogo kutokana na hivi sasa serikali inaadhimia kupokea ndege kubwa.

Alisema mikonga iliyoainishwa katika michoro ya awali ilionekana ndege ambazo zingeweza kuhudumiwa na mikonga ya kupokelea abiria ingeliwafanya abiria kushuka ndani ya uwanja wa ndege huku ndege ambazo zingeweza kutumia mikonga hiyo zingekuwa ni za mashirika madogo kama Precision.

Alisema kutoka na sababu hizo hivi sasa mabadiliko hayo yatasababisha kuwapo kwa mabadiliko ya ujenzi wa mikonga kutoka minne hadi kufikia mikonga miwili ikiwa ni hatua itayoweza kukifanya kiwanja hicho kuwa na hadhi ya kimataifa.

Kutoakana na hali hiyo waziri huyo alisema haoni sababu ya kuwapo kwa madai ya kutakiwa yeye na watendaji wake kuwa ajiuzulu kwani kilichofanyika ni urekebishaji wa mikataba na hivi sasa kampuni iliyopewa kazi hiyo inaendelea na kazi zake.

Mapema Naibu waziri wa wizara hiyo, Issa Haji Gavu, akijibu suala la msingi la Mwakilishi wa Jimbo la Muyuni Jaku Hashim Ayoub aliyetaka kujua sababu za msingi zilizosababisha kuwapo mikataba miwili yenye gharama tofauti za ujenzi.

Naibu huyo alisema kutokana na mabadiliko ya usanifu ambayo muajiri alitaka kufanyika na ndiko kulikosababisha gharama zake kubadilika kutoka dola za kimarekani 57.5 milioni, na kufikia dola za kimarekani 70.4 milioni zikiwa na lengo la kufanikisha ongezeko za vifaa kwa ajili ya ujenzi huo.

Alisema mradi huo unatarajiwa kumalizika mwezi Januari 2014, na umezingatia takribani huduma zote muhimu za kuhudumia ndege za mizigo ikiwemo mikonga ya kuhudumia ndege.

Alisema hadi hivi sasa tayari serikali imeweza kuwafidia wananchi 60 ambao waliathirika na kuwapo kwa ujenzi huo ikiwa ni hatua ya kuweza kufanikisha ujenzi huo.

Post a Comment

0 Comments