6/recent/ticker-posts

Kuimarisha Sekta ya Afya kwa Kuhakikisha Mahitaji ya Msingi ya Afya Yanaendana na Mpango Kazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO)

 Na.Omar Abdallah -Wizara ya Afya Zanzibar.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Afya Zanzibar imeendelea kutoa vipaumbele katika kuimarisha sekta ya afya kwa kuhakikisha mahitaji ya msingi ya afya yanaendana na mpango kazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO).Hatua hii inalenga kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa mipango ya pamoja kati ya Serikali na Shirika hilo la kimataifa.

Akizungumza katika mkutano wa mashirikiaono  ya Wizara ya Afya Zanzibar na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) wa kujadili vipao mbele vya Afya Zanzibar  Msimamizi wa ofisi ya WHO Zanzibar Dr Nemes Iriya amesema kwa kawaida, mpango kazi wa WHO huandaliwa kwa ushirikiano wa karibu na serikali za nchi wanachama ili kuhakikisha mipango hiyo inaendana na vipaumbele vya kitaifa.

Katika kikao kilichofanyika na wadau wa sekta ya afya wamekutana kupitia mpango wa WHO unaotekelezwa duniani na kuulinganisha na maeneo ya kipaumbele yaliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Wadau wametathmini namna mpango wa kimataifa unavyoweza kuakisi mahitaji halisi ya Zanzibar, ili kuuwezesha kuingizwa kwa ufanisi katika mpango wa pamoja wa utekelezaji.

Aidha, imeelezwa kuwa vigezo vya maendeleo katika sekta ya afya vinapaswa kuendana na mkakati wa Wizara ya Afya pamoja na miongozo ya Serikali, huku baadhi ya vigezo vikionekana kutofautiana na vile vya mpango wa kimataifa.

Kupitia majadiliano hayo, Serikali ya Zanzibar na WHO wamekubaliana kuendelea kufanya kazi kwa karibu katika kuratibu na kuoanisha vigezo hivyo, ili kuhakikisha vinakidhi malengo yaliyopangwa na pande zote mbili.

Mpango huo unatarajiwa kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi, sambamba na kuimarisha uwezo wa Serikali katika kufikia viwango vya kimataifa vya maendeleo ya afya. 

Mkurugenzi Sera mipango  na utafiti Wizara ya Afya Zanzibar  Abdul Latif Khatib Haji  

Amesema Lengo la kikao hicho ni kupitia taarifa kutoka Vitengo na programu husika, ili kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya.

Aidha Amesema Kupitia majadiliano hayo, wizara imepanga kuandaa Mpango Mkakati wa Muda wa Kati ambao utaainisha maeneo ya kipaumbele yatakayochochea uimarishaji wa huduma za afya kwa wananchi. Mpango huo wa miaka miwili unatarajiwa kuanza mnao  mwezi julai 2026 hadi mwaka 2028  kuwa na hatua mahsusi zitakazosaidia kuongeza ufanisi, kuboresha miundombinu, na kuimarisha huduma za afya kwa ujumla.

Wizara inaendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na salama, sambamba na kutimiza dira na maelekezo ya Serikali katika kuboresha sekta ya afya nchini. 

Nae Mkuu wa kitengo cha maradhi yasiombukiza Zanzibar Dr Omar Mohammed Amesema wadau wa Vitengo mbalimbali wamewasilisha maoni yao   miongoni vipaumbele vya sasa ni pamoja na magonjwa yasiyoambukiza (NCDs)  pamoja na huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto.

Maeneo haya yameonekana kuhitaji nguvu ya pamoja kwani yanagusa maisha ya watu wengi, hususan katika jamii zinazokaa mbali na vituo vikuu vya huduma.

Wadau hao wameeleza kuwa changamoto hizi haziwezi kutatuliwa kwa upande mmoja pekee, bali zinahitaji ushirikiano wa sekta mbalimbali pamoja na mashirika ya kimataifa.

MWISHO.

Post a Comment

0 Comments