Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza wakati wa hafla ya kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini ili kuwawezesha kumiliki makazi bora, katika hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mshamu Ali Munde (Mb), amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za fedha likiwemo Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) ili kuiwezesha sekta ya fedha kupata mikopo yenye gharama nafuu, hatua itakayosaidia jamii ya kipato cha chini kumiliki makazi bora.
Mhe. Munde amesema hayo Jijini Dar es Salaam, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akizindua rasmi huduma ya mikopo midogo ya makazi jijini Dar es Salaam, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora.
“Serikali inaunga mkono mipango kama hii inayolenga kukabiliana na changamoto za makazi, hasa kwa wananchi wa kipato cha chini ambao hukumbwa na vikwazo vikubwa zaidi vya kupata mikopo rasmi kwa kutokuwa na rehani inayohitajika kutokana na kipato chao kuwa kidogo au kisicho rasmi” alisema Mhe. Munde.
Alisema kuwa huduma hizo zinaunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza upatikanaji wa nyumba bora na nafuu zinazokidhi matarajio ya wananchi wa kipato cha chini, na kusaidia Serikali katika kuwahudumia wananchi wake katika sekta ya makazi.
Wakizungumza wakati wa uzinduzi huo rasmi wa huduma ya mikopo midogo ya makazi, Mkurugenzi Mtendaji wa TMRC, Bw. Elibariki Ndossi, amesema lengo kuu ni kuwawezesha Watanzania kupata makazi bora huku Mkurugenzi wa Mikopo ya Nyumba kutoka Habitat for Humanity Tanzania, Bw. Daniel Mhina, akiweka wazi kuwa kupitia mradi huo wananchi hawatalazimika kuwa na dhamana isiyohamishika ili kupata mkopo.
Walisema kuwa hatua hiyo inafuatia utafiti uliofanywa na taasisi hizo, unaoonesha kuwa ni takribani asilimia 3 tu ya Watanzania wanaopata huduma za mikopo ya nyumba, hali inayochangiwa na wengi kushindwa kumudu masharti na viwango vya mikopo hiyo.
Tangu kuanzishwa kwa TMRC mwaka 2010, taasisi hiyo imechangia uwezeshaji wa mikopo ya nyumba kutoka shilingi bilioni 76.7 hadi kufikia shilingi bilioni 745 mwaka 2025.

0 Comments