Habari za Punde

Israel Kutuma Wataalamu Kutafiti Maradhi ya Moyo kwa Watoto


Na Faki Mjaka - Maelezo                    

Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Idd Balozi amesema Israel itatuma timu ya Wataalamu kuja kufanya utafiti wa Ugonjwa wa Moyo ambao umekuwa ukiwashambulia watoto hasa kutoka maeneo ya Pemba na kutafuta njia nzuri za kuweza kukabiliana na tatizo hilo.

Balozi Idd ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasili uwanja wa Kimataifa wa ndege wa Abeid Aman Karume kutoka ziara yake ambapo alizitembelea Nchi za Israel, Cuba na Ras El kheima.


Amesema kuwa Israel imepata mshangao mkubwa kwa kuona kuwa watoto wadogo wengi kutoka Zanzibar wanakabiliwa na matatizo hayo ya ugonjwa wa moyo jambo ambalo si la kawaida kwa hivyo wameona iko haja ya kuja Zanzibar kufanya utafiti juu ya maradhi hayo.

Balozi Seif amesema kuwa mbali ya maradhi hayo Israel imeahidi kutoa nafasi za mafunzo kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji kwani wao wanachuo maalum cha kufundishia suala hilo kutokana na nchi yao kuwa ni jangwa kwa hivyo wanautaalamu wa kutosha.

Akizungumzia juu ya sula la kilimo cha ufugaji wa Samaki amesema kuwa Isarael pia ipo tayari kusaidia Zanzibar kwa wananchi walioanzisha ufugaji wa Samaki na zaidi kisiwani Pemba ili waweze kufanya shughuli hiyo kwa utaalamu zaidi na kujipatia kipato zaidi.

Kuhusu suala la maafa Balozi Seif amesema kuwa Israel ipo tayari kuisadia Zanzibar kwa kuipatia vifaa na mbinu za kuweza kujikinga na maafa na pia kuwasomesha wananchi wa Zanzibar kuhusu masuala hayo na tayari nafasi mbili kwa watu wa Zanzibar wamepatiwa kwenda nchi hiyo mwezi ujao

Kwa upande wa Cuba Makamu wa Pili wa Rais amesema kuwa nchi hiyo imekubali kuongeza madaktari Zanzibar wa maradhi mbalimbali na pia kutoa madaktari watakaoweza kuwafundisha wanafunzi wanaosomea fani hiyo hapa Zanzibar.

Aidha Balozi Seif amesema mbali na kuleta madaktari pia patakuwa na nafasi kwa nchi hizo mbili kubadilishana uzoefu katika fani hiyo kwa kutembeleana.
Mbali na shuguli hizo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alifanyiwa matibabu ya Macho nchini humo ambapo hali yake ipo nzuri na yakuridhisha.

Huko Ras El Kheima alisema kuwa nchi hiyo imeendelea katika ufugaji wa Lulu ambapo Zanzibar inaweza kufaidika katika soko hilo kwa wataalamu kutoka nchi hiyo kuja Zanzibar kuweza kuwafundisha wananchi ili na wao waweze kutoa zao hilo kwa wingi na soko kuu kuwa huko.

Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd aliondoka Zanzibar May 5,2012 kwa kuanzia ziara yake nchini Israel,Cuba na hatimaye Ras El Khaeima na kurejea Zanzibar June 2,2012.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.