Habari za Punde

Dk Shein Ahudhuria Mazishi ya Marehemu Makamu Mwenyekiti wa UWT Zanzibar Bi. Asha Bakari Makame Kianga Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                            22.1.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein  leo ameongoza mazishi ya marehemu Bi Asha Bakari Makame aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

Mazishi ya Marehemu Bi Asha Bakari Makame yalifanyika huko Kianga, Wilaya ya Magharibi ‘B’, Mkoa wa Mjini Magharibi kwa heshima zote za Chama Cha Mapinduzi, ambapo viongozi mbali mbali wa vyama na serikali walihudhuria  akiwemo Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.

Wengine waliohudhuria ni Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dk. Mohammed Gharib Bilal pamoja na Rais wa Zanzibar mstaafu Dk. Amani Abeid Karume na wananchi.

Mapema asubuhi, Alhaj Dk. Shein alifika nyumbani kwao marehemu huko Jangombe, mjini Unguja kwa ajili ya kutoa mkono wa pole kwa wana familia pamoja na kumuombea dua marehemu.

Baada ya hapo Alhaj Dk. Shein alishiriki katika dua maalum (hitma) pamoja na sala  ya kumsalia Marehemu Bi Asha Bakari Makame iliyofanyika huko Masjid Noor Mohammad, Mombasa kwa Mchina mjini Unguja.

Akisoma wasifu wa Marehemu, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema kuwa Marehemu Bi Asha Bakari Makame alizaliwa Disemba 12 mwaka 1949 huko Mtambwe, Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Kwa mujibu wa maelezo ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Marehemu Bi Asha alipata elimu ya msingi huko huko kijijini kwao Mtambwe na baadae alijiunga na Skuli ya Sekondari ya Fidelcastro huko Kisiwani Pemba hadi Kidato cha nne ambapo baada ya hapo alienda nchini Bulgaria kwa ajili ya kujiendeleza kwa elimu ya Diploma ya Siasa na Utawala.

Vuai alieleza kuwa tokea uhai wake, Marehemu Bi Asha Bakari Makame, akiwa skuli na baada ya kumaliza skuli alikuwa akijishughulisha na Umoja wa Vijana wa Chama Cha Afro Shirazi Party (ASP) na baadae alijiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pale kilipoanzishwa mnamo mwaka 1977.

Katika uhai wake Marehemu Bi Asha Bakari Makame, aliwahi kushika nyadhifa  mbali mbali ndani ya Chama Cha Mapinduzi pamoja na Serikali ikiwemo Naibu Waziri, Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo ambapo pia, aliwahi kuwa Waziri wa Wanawake na Watoto.

Marehemu Bi Asha Bakari, alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Umoja wa Wanawake (UWT) Taifa mnamo mwaka 1983 na baadae alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Umoja huo nafasi aliyoendelea nayo hadi kufa kwake.

Naibu Vuai katika akisoma wasfu huo wa Marehemu alisema kuwa marehemu Bi Asha  katika maisha yake alikuwa muumini wa kweli wa Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 pamoja na kuwa muumini wa kweli wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliofanyika mwaka 1964.

Marehemu Bi Asha Bakari Makame, katika kipindi chake chote alichotumikia chama cha CCM pamoja na serikali alikuwa kiongozi muaminifu, muadilifu, mchapakazi na asiyeyumba katika masuala ya msingi.

Naibu Vuai alisema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinatoa mkono wa pole kwa ndugu na jamaa wote wa marehemu. Nao wanafamilia walitoa shukurani Kwa wale wote waliohudhuria mazishi hayo.

Marehemu ameacha watoto watatu, wakiwemo wawili wa kike na mmoja wa kiume Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahala pema peponi. Amin.

Rajab Mkasaba, Ikulu

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.