Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                          8.08.2016
---
VIKAO vya kujadili mipango ya Utelekezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015- 2020 viliendelea tena jana Ikulu mjini Zanzibar chini ya Uenyekiti wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.
Katika vikao hivyo vya jana Rais alikutana, kwa nyakati tofauti, na viongozi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto, Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi pamoja na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji.
Akivifunga vikao hivyo kwa nyakati tofauti, Mheshimiwa Rais alisisitiza umuhimu wa viongozi wa Wizara hizo kusimamia kwa karibu Wizara zao na kuweka uwiano halisia wa majukumu ya ofisi zao Unguja na Pemba kwa kufanya ziara za kikazi mara kwa mara kisiwani Pemba wakiwa na malengo maalum yanayoeleweka.
Alibanisha kuwa kwa kufanya hivyo wizara zitaweza kupata picha kamili ya utekelezaji wa majukumu ya wizara zao na kurasihisha majadiliano ya ripoti za tathmini ya utekelezaji wa kazi za wizara maarufu ‘Bangokitita’ vinavyofanyika kila baada ya robo mwaka.
Akizungumza katika kikao cha wizara yake, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Balozi Ali Karume alimshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna anavyofuatilia utendaji wa wizara jambo ambalo linazidi kuwapa viongozi ari na kuweza kufanya kazi kwa kujiamini zaidi na kufanya maamuzi stahiki na kutenda kazi zao kwa ufanisi.
Kwa upande wake Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Hamad Rashid Mohamed alimhakikishia Mheshimiwa Rais kuwa jukumu alilomkabidhi kuongoza Wizara hiyo atalitekeleza kwa umakini lakini ameishauri serikali kuongeza bajeti ya kilimo hadi kufikia asilimia kumi ya bajeti ya serikali ili kwenda sambamba na utekelezaji wa Azimio la Maputo.
Kuhusu kujitosheleza kwa chakula ambapo serikali imeweka lengo la kuzalisha asilimia 80 ya mahitaji ifikapo mwaka 2020, Waziri huyo alisema utekelezaji wa lengo hilo unaweza kufikia mapema zaidi endapo kuwatakuwa na ushiriki wa kweli wa sekta binafsi katika sekta ya kilimo.
Mapema Dk. Shein alikutana na uongozi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto na kusisitiza haja kwa Wizara hiyo kuendelea kuzisaidia familia zinazoishi katika mazingira magumu.
Katika maelezo yake Dk. Shein alisisitiza kuwa Wizara hiyo ina kila sababu ya kuendelea kuzisaidia familia hizo sambamba na kutoa taarifa kwa Serikali ili taratibu zaidi ziendelee kuchukuliwa.
Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja kwa viongozi wa Wizara hiyo kufanya ziara za mara kwa mara Unguja na Pemba ili kujua shughuli na harakati za kiutendaji katika Wizara hiyo.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Wizara hiyo kutokana na juhudi inazozichukua katika kuhakikisha inatekeleza vyema majukumu yake huku akiwasisitiza viongozi wa Wizara hiyo kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu zaidi.
Nao uongozi wa Wizara hiyo ulieleza jinsi unavyoendelea na juhudi za kuhakikisha inasimamia miongozo ya kazi, kupunguza tatizo la ajira kwa vijana, kuwawezesha wananchi kiuchumi sambamba na kuimarisha maendeleo ya Wanawake, Wazee, Vijana na Watoto.
Vikao hivyo vinatarajiwa kuendelelea hapo kesho.
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.