Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein, Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Kazi Uwezeshaji Wazee Vijana Wanawake na Watoto Ikulu leo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                          20.10.2016
---
WIZARA ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto  imeeleza haja ya kutambua vyema taarifa na kumbukumbu za wageni wanaokuja kufanya kazi ama kuekeza hapa Zanzibar ambao hutoka nje ya Tanzania ili kuepuka changamoto za kiusalama, ajira na masuala mengineyo ya kijamii. 

Hayo yameelezwa leo na uongozi wa Wizara hiyo, huko  Ikulu mjini Zanzibar katika kikao maalum kati ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na uongozi wa Wizara hiyo ilipokuwa ikiwasilisha Taarifa yake ya  Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara  kwa kipindi cha Julai hadi Septemba katika Bajeti ya mwaka 2016-2017.

Katika maelezo yake, Waziri wa Wizara hiyo Maudline Cyrus Castico alieleza kuwa kuna umuhimu wa kuchukuliwa juhudi za makusudi katika kujua taarifa na kumbukumbu kwa wawekezaji na wafanyakazi wanaotoka nje ya nchi kwa ajili kuepuka changamoto kadhaa ambazo zingeweza kupatiwa uvumbuzi mapema iwapo hatua zitachukuliwa.

Waziri Castico pia, alieleza haja kwa Serikali kuweka mkakati maalum kwa baadhi ya watoto ambao hutembea nyakati za usiku mkubwa ili kuwakinga na matukio mabaya ambayo yanaweza kuwatokezea nyakati hizo.

Aidha, alizieleza  juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara yake katika kuielimisha jamii kupitia vyombo vya habari, juu ya kuepukana na  mambo mbali mbali yenye athari kwa jamii likiwemo suala zima la udhalilishaji hapa nchini.

Waziri Castico alitumia fursa hiyo kwa niaba ya viongozi na wafanyakazi wa Wizara yake kutoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuliongoza Taifa na kusisitiza kuwa uongozi wake umeleta maendeleo endelevu katika nyanja zote za siasa, uchumi, ustawi wa jamii, elimu, miundombinu, utamaduni na maendeleo mengine kwa ujumla.
Sambamba na hayo, Waziri Castico alieleza kuwa Zanzibar imeendelea kuwa na amani na utulivu jambo ambalo linatoa faraja na ni nyenzo kubwa ya kujiletea maendeleo endelevu kwa wananchi.

Uongozi huo, ulieleza jinsi Zanzibar inavyopata sifa kubwa Kimataifa kutokana na kuanzisha Pencheni Jamii kwa wazee kuanzia miaka 70, ikiwa ni miongoni mwa juhudi kubwa za uongozi wa Dk. Shein katika kuhakikisha wazee wanaenziwa, wanatunzwa na wanaendelea kuyafaidi matunda  ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wake alitoa pongezi kwa Wizara hiyo huku akieleza juhudi mbali mbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika suala zima la ajira, uwezeshaji, wazee, vijana, wanawake na watoto.

Dk. Shein alieleza kuwa ni jukumu la kila mwananchi kupiga vita suala zima la udhalilishaji kwa watoto na hata watu wazima wakiwemo wanawake huku akieleza mikakati inayoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kuhakikisha vitendo hivyo vinatokomezwa.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja ya kutolewa elimu kwa wananchi juu ya usalama katika maeneo yao ya  kazi pamoja na nyumba zao wanazoishi ili kuepuka majanga na athari zinazoweza kutokezea huku akieleza umuhimu wa mashirikiano kati ya Wizara hiyo na Mawakala wanaowapeleka vijana kufanya kazi nje ya nchi.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, alitilia mkazo suala zima la kupata taarifa na kumbukumbu sahihi za wageni wanaokuja hapa nchini kwa ajili ya kufanya kazi au kuekeza na kupongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na uongozi pamoja na watendaji wa Wizara hiyo.

Balozi Seif alieleza kuwa Serikali italiangalia kwa mtazamo maalum suala zima la udhalilishaji pamoja na matembezi ya watoto wadogo nyakati za usiku mkubwa  huku akieleza haja ya kuendeleza mashirikiano kati ya Wizara hiyo na Wizara ya Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Nae Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliupongeza uwasilishwaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo na kusisitiza suala zima la taarifa kwa wageni huku akigusia suala zima la viongozi kuwasimamia vyema wafanyakazi wao ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.