Habari za Punde

Vijana waaswa kutojiingiza katika vitendo vinavyoweza kuvuruga amani

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                                                             5.11.2016
---
MKE wa Rais wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mama Mwanamwema Shein amewataka Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuendelea kuwaelimisha vijana wasikubali kutumika katika vitendo vinavyoweza kuvuruga amani huku akiwataka kuieleza jamii kuwa uchaguzi umekwisha hadi mwaka 2020 ndipo utafanyika uchaguzi mwengine.

Mama Mwanamwema Shein aliyasema hayo leo huko Ikulu ndogo Chake Chake Pemba katika Mkutano kati yake na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar wa Majimbo ya Pemba pamoja na wale wa Viti Maalum.

Katika maelezo yake Mama Shein, aliwataka viongozi hao kutambua kuwa nyazifa zao ni za ulezi na usimamizi wa jamii wanayoizunguka ikiwa ni pamoja na kuwasisitiza vijana kukimbilia katika kazi za halali zitakazowapatia kipato kwani Serikali haina ajira za kutosha kwa wote wanaohitaji.

Aidha, aliwataka viongozi hao kuwaelimisha vijana juu ya madhara ya utumiaji wa dawa za kulevya na kuwataka vijana walioko skuli kuongeza bidii katika masomo yao kwani nchi hii itajengwa na wananchi wenyewe hasa vijana wenye maarifa na ujuzi.

“Kwa kuwa mimi ni mzazi, naguswa sana na hatma ya vijana wetu kuendelea kudanganywa na kudanganyika hivyo tuendelee kuwaelimisha katika majimbo yetu kuwa wakatae kutumika katika vitendo vinavyoweza kuvuruga amani, wajue kuwa uchaguzi umekwisha”,alisema Mama Shein.

Mama Shein alieleza kuhuzunishwa kwake na vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto na kuwataka viongozi hao kuelekeza juhudi zao katika kuwaelimisha vijana na wazazi juu ya mbinu za hadaa na mazingira yanayotumiwa na wabakaji na wadhalilishaji wote kwa jumla.

Hivyo, Mama Shein alieleza haja ya kutoa elimu kwa mtu mmoja mmoja, vikundi pamoja na ngazi za familia na kueleza kuwa Serikali kwa upande wake imeanza kuchukua hatua mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuanzisha kampeni maalum ya kutokomeza vitendo hivyo kupitia Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto kwa kushirikiana na Taasisi mbali mbali.

Pamoja na hayo, Mama Shein alisema kuwa ushindi mkubwa kilichoupata Chama Cha Mapinduzi kwa  wagombea wake wa nafasi mbali mbali za uongozi wa kisiasa katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kielelezo thabiti cha imani ya wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa chama hicho.

Mama Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa kukipatia ushindi mkubwa chama cha CCM kutokana na wananchi wa Pemba kuzikubali Sera za CCM pamoja na kuwakubali wagombea kupitia chama hicho.

Aidha, Mama Shein alisema kuwa miongoni mwa majukumu ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba chini ya uongozi wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein imedhamiria ni kushirikiana na wananchi katika kupambana na umasikini.

Mama Shein alisema kuwa Serikali imeandaa fursa mbali mbali kupitia Wizara zake lakini na viongozi nao wanawajibu wa kuwaunganisha wananchi na kuwahamasisha kuzifuatilia na kuzitumia fursa hizo hasa kwa ajili ya kina mama na vijana.

Alisema kuwa kwa upande wao wakiwa wake wa viongozi wa Serikali wamejiwekea utaratibu wa kuhamasisha na kuongeza nguvu kwa wale ambao tayari wamehamasika katika suala zima la kupambana na umasikini.

Nae Mke wa Makamo wa Pili wa Rais, Mama Asha Balozi aliwaeleza viongozi hao umuhimu wa Umoja wa wake wa viongozi kwa maendeleo ya wananchi wote huku akisisitiza juu ya suala zima la kuendeleza amani na utulivu.

Aidha, alieleza kuwa suala la udhalilishaji ni kubwa sana litakuwa ni kipaumbele katika utekelezaji wa majukumu ya umoja huo pamoja na kueleza haja ya kuunda Kamati Maalum katika Majimbo ili iwe kimbilio kwa wananchi pale linapotokea tatizo la udhalilishaji wa wanawake na watoto ili wapate msaada.

Mjane wa Marehemu Mzee Abeid Amani Abeid Karume, Mama Fatma Karume, alitumia fursa hiyo kutoa historia ya Zanzibar pamoja na kutoa pongezi na shukurani kwa Dk. Shein kwa kuendelea kuiongoza Zanzibar kwa nguvu zake zote na kuendelea kusisitiza kuwa hakuna uchaguzi mwingine hadi mwaka 2020 wala Serikali ya Mpito na kilichokuwepo hivi sasa ni kuijenga nchi na wananchi wake ili kuweza kupata maendeleo.

Nao Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Majimbo ya Pemba walitumia fursa hiyo kutoa pongezi na shukurani kwa Mama Shein kwa nasaha zake pamoja na kuahidi kuyafanyia kazi maazimio ya mkutano huo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.