Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Atembelea Kampuni ya Telecom Haromous

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Djibouti                                                                    8.05.2017

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ametembelea Kampuni ya simu ya ‘Djibouti Telecom Haramuos’ na kupongeza jinsi kampuni hiyo inavyofanya kazi zake ndani na nje ya nchi hiyo.

Katika ziara yake hiyo mjini Djibouti, Dk. Shein alipata maelezo juu ya uendeshaji wa Kampuni hiyo inayojumuisha mkonga wa mawasiliano kupitia katika bahari pamoja na maeneo ya nchi kavu kwa nchi mbali mbali zikiwemo za Afrika ya Mashariki.

Akipata maelezo kutoka kwa uongozi wa Kampuni hiyo, alielezwa kuwa zaidi ya nchi 90 zimekuwa zikifaidika na mkonga wa mawasiliano kutoka kampuni hiyo zikiwemo Ausralia, nchi za Asia, Ulaya na Afrika.

Huduma za mtandao huo kwa mujibu wa maelezo ya uongozi wa Kampjni hiyo ,zina mchango mkubwa wa maendeleo ya kiuchumi na wa kijamii kutokana na kurahisika kwa mawasiliano ya kimtandao katika shughuli mbali mbali zikiwemo za biashara, elimu, na afya.

Hata hivyo, uongozi huo wa ‘Djibouti Telecom Haromous’ ulimueleza Dk. Shein kuwa Kampuni yao bado inaendelea kupanua soko lake na tayari imeshaanza hatua za mashirikiano na nchi mbali mbali zikiwemo nchi zilizokuwa hazipitiwa na bahari kama Rwanda na nchi nyenginezo.

Mapema katika Ofisi za Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa mjini Djiboti mkutano maalum wa kubadilishana mawazo kati ya viongozi waliokuwemo katika ziara hiyo ya Dk. Shein,kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar walipata fursa ya kubadilishana mawazo juu ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano katika sekta za maendeleo na viongozi wenzao wa Djibouti.

Kwa upande wa viongozi wa Tanzania, walieleza haja ya kukuza ushirikiano na uhusiano kati ya Tanzania na Djiboti hasa katika miradi ya maendeleo na kueleza kuwa ziara hiyo itawezesha kujua mikakati na kujifunza mbinu mbali mbali na baadae kufanyiwa kazi.

Aidha, viongozi hao walitumia fursa hiyo kueleza hatua za makusudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika ujenzi mpya wa miundombinu ya mawasiliano, bandari.

Pamoja na hayo viongozi hao kwa pamoja walitoa rai kwa vuiongozi hao wa Djiboti kwa kuwaalika wawekezaji na wafanyabiashara wa Djiboti kuja kuitembelea Tanzania ikiwemo Zanzibar sambamba na kuekeza miradi yao.

Pia, viongozi hao walieleza juhudi zinazochukuliwa katika kuimarisha sekta ya utalii hasa ikizingatiwa kwamba sekta hiyo ina mchango mkubwa kwa Zanzibar na Tanzania kwa jumla kutokana na mchango wake katika uchumi.

Nao viongozi wa Djibouti walieleza kufarajika kwao kwa ziara ya Dk. Shen nchini humo, na kueleza kuwa ziara hiyo itakuwa mwanga mkubwa katika kuazisha ushirikiano  wa kiuchumi na kijamii sambamba na kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Djibouti na Tanzania.

Viongozi hao walieleza kuwa nchi yao iko katika usalama mkubwa hivi sasa na ndio imekuwa chachu ya maendeleo wanayoyapata ikiwa ni pamoja na kuwa kivutio cha wawekezaji kutoka ndani na nje ya bara la Afrika.

Viongozi hao wajibuti wakiwemo Mawaziri wan chi hiyo walieleza kuwa Djibouti na Tanzania ina maeneo mengi ya kushirikiana hasa kwa kuzingatia kufanana kwa mazingira ya nchi mbili hizo.

Pamoja na hayo, viongozi hao walieleza mikakati yao ya kuimarisha uchumi wa nchi yao ikiwa ni pamoja na hatua za kupanua soko nje ya nchi yao pamoja na mashirikiano na nchi nyengine ambayo yamepelekea kushirikiana katika kuekeza miradi kadhaa ambapo nchi kama Ethiopia imekuwa ni miongoni mwa nchi hizo.

Viongozi hao kwa pamoja walieleza haja ya kuwepo kwa ziara za mara kwa mara kwa pande zote mbili ili kuweza kukaa pamoja na kujadili namna ya kuendeleza na kukuza ushirikiano katika sekta za maendeleo na uchumi.  

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.