Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Amewaahidi Wananchi wa Charawe na Ukongoroni Barabara Yao Itajengwa kwa Kiwango Cha Lami Ndani ya Miezi 12.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                15.08.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewaahidi wananchi wa vijiji vya Ukongoroni na Charawe kuwa ndani ya miezi 12 barabara yao itajengwa kwa kiwango cha lami na kuwataka wawe na subira kwani hatua hiyo ni kutekeleza ahadi yake kwa wananchi wa vijiji hivyo.

Dk. Shein alitoa ahadi hiyo leo katika ziara yake ya kutembelea miradi ya maendeleo sambamba na kuangalia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 inavyotekelezwa katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba, ziara inayoendelea Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja ambapo vijiji hivyo vimo ndani ya Wilaya hiyo.

Akiwa katika kijiji cha Ukongoroni mara baada ya kukagua shamba la kilimo cha midimu alipata fursa ya kuwaeleza wananchi waliofika katika banda wanalohifadhia ndimu zao kuwa kutiwa lami kwa barabara zao hizo za Ukongoroni na Charawe ni utekelezaji wa ahadi ya chama chake ambayo aliahidi yeye mwenyewe.

Dk. Shein alisema kuwa licha ya kuwepo kwa changamoto ya upungufu wa vifaa kwa Idara husika ya ujenzi wa barabara (UUB), juhudi za makusudi zitachukuliwa katika kuhakikisha barabara hiyo inajengwa kwani tayari ndani ya uongozi wa Serikali anayoiongoza imeweza kuijenga kwa kiwango cha kifusi.

Aliwaleleza wananchi hao kuwa Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar imefanya mambo mengi na kuwahaidi kuwa atahakikisha vijiji hivyo vinazidi kupata maendeleo endelevu na kamwe vijiji havitokuwa kama vilivyokuwa hapo siku za nyuma huku akiponmgeza kilimo cha ndimu kinavyoendeshwa hapo Ukongoroni.

Akiwa kijiji hapo, Dk. Shein aliwataka Mawaziri husika ambao wananchi walizitaja changamoto walizonazo kupitia Wizara zao wawahakikishie ni kwa namna gani Serikali kupitia Wizara zao itazitatua changamoto hizo zikiwemo barabara, afya, elimu, kilimo na sekta nyenginezo.

Ambapo kwa upande wa kilimo Waziri husika wa Wizara hiyo Hamad Rashid Mohammed alieleza hatua zinazochukuliwa kupitia mradi wa MIVARF kuwapatia mashine wakulima wa ndimu kwa ajili ya kuzisarifu ili hatimae wapate soko la uhakika.

Nao wananchi wa kijiji cha Ukongoroni kupitia Sheha wao Haji Vuaa Khamis walieleza changamoto zinazowakabili ikiwemo barabara yao yenye urefu wa kilomita 13.7 kutaka kuweka lami pamoja na ile ya Charawe yenye urefu wa kilomita 12.8, pamoja na uhaba wa madaktari.

Nao Mawaziri wasio na Wizara Maalum kutoka vyama vya upinzani walipongeza juhudi za Dk. Shein za kuwapelekea wananchi maendeleo na kuahidi kuwa wataendelea kumuunga mkono kwani maendeleo hayana chama huku wakiwataka vijana kuiheshimu Serikali na kuyathamini Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Mapema Dk. Shein alipokea taarifa ya Mkoa huo huko katika Ofisi za Mkoa wa Kusini Unguja zilizopo Tunguu, Wilaya ya Kati ambapo taarifa hiyo ilieleza mafanikio, changamoto na utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Mkoa huo.

Taarifa hiyo ilitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuongoza kwa busara, hekima na uadili huku wakipongeza hatua zake kwa kufanya ziara hizo kwa ajili ya kuwatumikia wananchi wote wa Zanzibar.

Wakati huo huo, Dk. Shein aliweka jiwe la msingi katika jengo la CCM Tawi la Kaebona  na kueleza kufarajika na ujenzi huo ambapo wanaCCM hao watapata fursa ya kujadili mambo ya chama chao na kuahidi kuliezeka, kuliweka milango, madirisha pamoja na kutoa mtaji kwa mradi wa duka lao wanalolijenga tawini hapo.

Aidha, Dk. Shein aliweka jiwe la Msingi ghala la kuhifadhia mazao ya JKU huko Cheju na kupongeza juhudi zizochukuliwa na kikosi hicho chini la kuahidi kuzitekeleza changamoto zilizoelezwa zikiwemo kuwapatia matreka pamoja na mashine ya kupandia mbegu.

Dk. Shein pia, alikihakikishia kikosi hicho kuwa Serikali anayoiongoza itaendelea kutekeleza azma ya vikosi vya Serikali vilivyoasisi na Rais wa Awamu ya kwanza wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume.

Katika taarifa iliyosoma na uongozi wa JKU katika kambi hiyo ya Cheju iliyoanzishwa mwaka 1976, ilioanzishwa kwa lengo la kuendesha kilimo cha Mpunga wa kutegemea mvua yenye ukubwa wa ekari 85 ambazo 70 zinalimwa mpunga na kunde, 10 kilimo mchanganyiko na 5 kwa ajili ya majengo.

Uongozi huo ulieleza kuwa utekelezaji wa ujenzi wa ghala hilo umetokana na vianzio vya mapato ya miradi ya Kambi na sio ruzuku kutoka Serikalini.

Akiwa Mitakawani, Dk. Shein alipata maelezo juu ya mradi wa maji safi na salama pamoja na kukagua mradi wa kisima cha maji na kuitaka Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja kisima hicho kiwe kimekamilika ili wananchi wa kijiji hicho wapate huduma hiyo ya maji.

Dk. Shein pia, alizindua Mradi wa kisasa wa ufugaji wa nyuki huko Dunga na kupata maelezo kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Kati Mashavu Sukwa juu ya mradi huo ambao Wizara ya Kilimo ulipeleka wataalamu na kuanza kwa mitego mipya 13.

Alioongeza kuwa kwa kila mtego hupelekea kupatikana kwa lita kumi za asali ambapo kila lita moja huuzwa kwa TZS elfu 20 hivyo kwa mara moja mfugaji anapata laki 2 shughuli ambayo anaweza kuifanya mara moja kila baada ya miezi miwili.

Pia, Dk. Shein alipata fursa ya kukagua kazi za ujasiriamali za Baraza la Vijana wa Wilaya ya Kati na kupongeza juhudi zao wanazozichukua katika kuendeleza miradi yao na baadae aliweka jiwe la msingi la jengo la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kati Unguja.

Akitoa salamu zake mara baada ya kuweka jiwe hilo la Msingi, Dk. Shein alipongeza hatua za ujenzi huo zilizofikiwa na Wilaya hiyo na kueleza kuwa jengo hilo la ghorofa moja litamalizwa ili liwe la mfano wake.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.