Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Biashara Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                          24.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,  ameupongeza uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kwa kutekeleza vyema majukumu yao na kuutaka kutotumia muda wao mwingi kukaa ofisini na badala yake waende kwa wananchi wakawasikilize changamoto zinazowakabili kwani Wizara hiyo imegusa mambo muhimu katika maisha yao.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2016/2017, Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2017/2018 na Utekelezaji wake kwa  kipindi cha robo ya kwanza ya Julai hadi Septemba, 2017.

Dk. Shein alieleza haja kwa uongozi huo kuyakabili na kuyasimamia majukumu yao na kuueleza uongozi huo kuwa kuwasikiliza wananchi changamoto zao ndio sifa moja wapo kubwa ya uongozi kwani kiongozi ni lazima awasikilize wananchi pamoja na wale wote anaowaongoza.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza suala zima la kuwajibika katika utekelezaji wa kazi zao, kwani kila mmoja ana wajibu wake kazini kwake na katika cheo chake kwa kufuata taratibu, kanuni, sheria na misingi yote ya kazi. “uwajibikaji utakuja kwa kujituma… Pia, ni vyema kufanya kazi kwa kufuata wakati”.alisisitiza Dk. Shein.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa uongozi na wafanyakazi wote wa Wizara ya hiyo kwa kutekeleza vyema majukumu yao na kufanya kazi kwa pamoja hali ambayo imedhihirika baada ya uwasilishaji wa Mpango Kazi wao na kuwataka kuendeleza utamaduni huo.

Alieleza matumaini yake katika usimamizi wa sekta zilizomo katika Wizara hiyo ikiwemo sekta ya ardhi na kusisitiza mashirikiano pamoja na kusaidiana katika kutekeleza majukumu yao ya kazi huku akitoa pongezi kwa hatua zinazochukuliwa katika kupeleka umeme kwenye visiwa vidogo vidogo kupitia Shirika lake la (ZECO).

Dk. Shein alieleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika kupata taarifa za upatikanaji na uhifadhi wa mafuta hapa Zanzibar  kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) pamoja na utaratibu mpya wa ununuzi wa mafuta kwa lengo la kuondosha usumbufu wa nishati hiyo kwa wananchi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alifurahishwa na azma ya Wizara hiyo katika suala zima la Mipango Miji hasa kwa mji wa Zanzibar sambamba na azma ya kurejesha haiba na jina la Uwanja wa Farasi uliopo mjini Unguja ambao hapo miaka ya nyuma uwanja huo ulitumika na kuwa maarufu kwa mchezo wa farasi.

Katika kikao hicho, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd nae alihudhuria na kutumia fursa hiyo kusisitiza haja ya kuwepo kwa uhakika wa upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa Unguja na Pemba.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja ya kuwepo kwa usimamazi mzuri kwa watendaji wa Wizara hiyo kutokana na sekta zake kuwagusa wananchi moja kwa moja.

Nae Waziri wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib alieleza kuwa  Wizara hiyo inaendelea na jitihada zake za kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bora za maji, nishati, Mazingira ya kuishi pamoja na kuimarisha matumizi bora ya ardhi.

Waziri Salama alieleza kuwa kwa upande wa Mkoa wa Mjini Magharibi, utekelezaji wa mradi wa maji safi na usafi wa mazingira ambao unatarajiwa kukamilika ifikapo 2018 umeanza kuonesha mafanikio katika maeneo ya uimarishaji wa miundombinu ya maji unaohusisha ukarabati na uchimbaji wa visima vipya 9, ujenzi wa matangi matatu ya juu yenye jumla ya ujazo wa lita milioni 5 sambamba na ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilomita 68 yenye upana tofauti.

Kwa upande wa program ya usambazaji maji vijijini, Wizara hiyo imo katika hatua za kukamilisha mradi wa uchimbaji visima na usambazaji maji unaofadhiliwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.

Hii ni kwa lengo lakuimarisha huduma za maji katika maeneo makuu matano ambayo ni Chaani, Donge na Kisongoni kwa Mkoa wa Kaskazini Unguja na Kiboje na Miwani kwa Mkoa wa Kusini Unguja.  

Nao uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira ulieleza  kuwa hali ya mifuko ya plastiki hivi sasa ni nzuri licha ya kuwepo kwa baadhi ya watu wachache waliokuja na mbinu mpya za kuuza mifuko milaini ya plastiki ambayo hutumika kwa kufungia bidhaa mbali mbali vikiwemo viungo masokoni lakini hata hivyo waliahidi kupambana na watu hao.

Uongozi huo ulieleza marufuku iliyowekwa kutokana na sheria zilizopo ni kuwa mifuko ya plastiki yenye mikono na isiyo na mikono yote hairuhusiwi kutumika hapa Zanzibar.

Uongozi huo pia, ulieleza kuwa hadi mwishoni mwa mwaka huu itakuwa imeshachimba visima 50 kwa Unguja na Pemba na kueleza kuwa azma ya kuhakikisha huduma ya maji safi na salama inafanikiwa kwa wananchi wote wa Unguja na Pemba.

Pia, ungozi huo uliahidi kuendelea kutoa taarifa kwa wananchi juu ya utekelezaji wa majukumu yake kwa sekta zake zote zilizomo katika Wizara hiyo sambamba na kutoa elimu kwa wananchi.

Wakati huo huo, Dk. Shein alikuna na uongozi wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko chini ya Waziri wake Balozi Amina Salum Ali ambapo Waziri huyo alieleza kuwa thamani ya uzalishaji viwandani katika mwaka 2016-2017 imeimarika na kufikia 4,879 milioni kwa mwaka 2016 ikilinganishwa na milioni 4,170 mwaka 2015.

Aliongeza kuwa ukuaji huo umetokana na kuimarika kwa uzalishaji katika viwanda vya usagaji nafaka, kiwanda cha maziwa cha Azam, Kiwanda cha Sukari Mahonda, usarifu wa matunda na mboga mboga, viwanda vya maji ya chupa pamoja na viwanda vya kokoto na matofali.

Pia, uongozi huo ulieleza majukumu yaliotekelezwa na Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS),  hatua zilizochukuliwa katika utoaji na upatikanaji wa leseni kupitia Baraza la Kusimamia Mfumo wa utoaji Leseni (BLRC) pamoja na majukumu ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali Zanzibar (BPRA).

Nae Dk. Shein kwa upande wake aliupongeza uongozi wa Wizara hiyo kwa kutekeleza vyema majukumu yake pamoja na kuendelea kusimamia vyema masuala ya biashara, viwanda na masoko kwa lengo la kuimarisha uchumi na maendeleo hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.