Habari za Punde

DPP Yasifia Ushirikiano ZLSC

Na. Haji Nassor - Pemba.
OFISI ya Mkurugenzi wa Mashitaka kisiwani Pemba, imesifia sana ushirikiano uliopo, baina yao na Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ZLSC tawi la Pemba, katika kuwafikia wananchi kuwapatia elimu ya sheria, inayowapa ujasiri wa kudai haki zao.

Kauli hiyo imetolewa na Mwanasheria wa Serikali kutoka Afisi hiyo, Juma Ali Juma wakati akizungumza kwenye kipindi maalumu kilichorushwa na kituo kimoja ya redio, kisiwani Pemba wakiwa na Afis Mipango wa Kituo cha hicho, Khalfan Amour Mohamed.

Alisema ZLSC, mewasaidia sana wao kama ofisi ya DPP, kwa vile wamekuwa wakishirikiana kutoa elimu hata ule wakati, ambao ofisi yao haijapata uwezo wa kwenda vijijini.

Mwanasheria huyo, alisema inatokezea Kituo cha huduma za sheria, kuwa na safari za vijijini, hivyo watendaji wa DPP huangana nao, hivyo kuwaelezea wananchi kazi na majukumu yao.

Alisema, kuwepo kwa ZLSC inaonyesha sasa wananchi baadhi wameshawiva kitaaluma walau kujua haki zao, kutokana na wengine kupata ujasiri wa kufuatilia haki zao ofisini kwao, jambo ambalo, awali lilikuwa gumu.

“Mimi nadhani usirikiano wetu uliopo baina yetu sisi na ZLSC, umezaa matunda sana, maana tunaona wananchi wanapofika hata mahakamani, wanajitetea kisheria sio maneno matupu”,alifafanua.

Hata hivyo Mwanasheria huyo wa serikali, amewataka wananchi kuendelea kuitumia ofisi yao, ili kupata ufumbuzi wa mambo yao ya kisheria, badala ya kusikiliza maneno ya vijiweni.
Nae Afisa Mipango wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ZLSC tawi la Pemba, Khalfan Amour Mohamed, alisema kituo kimekuwa na kazi kubwa ya kuwafikisha taaluma ya sheria wananchi.

Alisema, sasa wananchi kadhaa wamepata uwelewa mkubwa wa kuzifuatilia haki zao kwenye vyombo vya sheria, wakiwa na uthubutu jambo, ambalo hapo awali halikuwepo.

“Sasa wananchi wanauwelewa mkubwa wa kuzitambua haki zao, tofauti na zamani na sasa wakienda mahakamani, DPP au kwenye taasisi nyengine za kisheria, hili tunajivunia”,alisema.

Baadhi ya wananchi walizoungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema taasisi za kisheria lazima ziongeze kasi ya kuwaelimisha wananchi juu ya namna bora kujenga uthubutu ya vyombo vya sheria.

Ali Hamza Haji wa Machomane Chakechake, alisema pamoja na wananchi kupata, uwelewa lakini bado, vyombo hivyo vinakumbwa na harufu ya rushwa.

Kwa upande wake Hassina Hamad Omar, alisema wanawake lazima wajengewe uwezo wa kuvifikia vyombo vya sheria, wanapokuwa wamedhulumiwa haki zao.

Hata hivyo wananchi hao, waliwataka wanasheria kuhakikisha wanavitumia vyombo vya habari kutoa elimu, ili wananchi wazidi kufahamu haki na wajibu wao.


Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka Zanzibar imeanzishwa mwaka 2002, sawa na Kituo cha Huduma za Sheria kilichoanzishwa mwaka 1992 na kuanza kazi zake rasmi kisiwani Pemba, mwaka 2002.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.