Habari za Punde

Akinamama Washajiishwa kujiunga na vikundu vya ushirika Kaskazini Pemba


NA/ ASHA BAKARI --- PEMBA

Wajasiriamali wa kikundi cha ushirika  cha Tekeleza waliopo Mavungwa Shehia ya Mbuzini Mkoa wa Kaskazini Pemba, wamesema kutokana na hali za kimaisha zilivyo hivi sasa ni kheri kwa akina mama kushiriki katika vikundi mbalimbali vya ushirika kwani manufaa ni makubwa kiasi ambacho hata 
baadhi ya wanaume wanaweza kupata msaada kutoka kwa wake zao.

Wajasiria mali hao waliyaeleza hayo mbele ya Waandishi wa habari waliofika katika ushirika huo kwa lengo la kuwatembelea na kutazama mafanikio na changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo katika uendeshaji wa shughuli zao.

Walisema  kupitia ushirika wa  Tekeleza, ambao ndio kituo kikuu cha ushirika Mavungwa, wamefanikiwa  kufungua miradi yao mbalimbali na hivi sasa wanaiendeleza  vizuri na hali za kiuchumi zinazidi kuimarika.

Bi Sharifa Khamis,  ambae ni Mwanachama wa kikundi hicho kilichojikita zaidi katika ufugaji na kilimo, alisema   kupitia Tekeleza amefanikiwa kupata elimu ya ujasiriamali na kuamua kuifanyia kazi na hadi sasa ameshafungua mradi wa kufuga bata mzinga akishirikiana na wananchi wengine .

''Nashuruku tunapata pesa , hali sio kama mwanzo, sasa naweza kujipatia mahitaji muhimu katika maisha , nimeshanunua makabati yangu ya kuwekea nguo na cherahani'', alisema mama huyo.

Akielezea mafanikio zaidi aliyayapata, alisema jambo kubwa na la msingi mpaka hivi sasa anamudu kuwasomesha watoto wake kwa kuwalipia ada za Skuli na huduma nyengine jambo ambalo alisema kwake ni faraja kubwa.

Mwanachama mwengine ambae anaonekana kufurahia uwepo wa kikundi cha Tekeleza, Bi Lela Seif Khamis, alisema mara tu ulipokuja mradi wa kujifunza mambo mbalimbali ya ujasiriamali katika kikundi hicho  aliungana na wenzake kutekeleza majukumu ya kikundi huku akipokea taaluma tofauti zilizokua zikimletea mwanga katika maisha.

Alisema kutokana na upeo wa maarifa waliokua wakipatiwa hivi sasa ameshajiwezesha mwenyewe na hali za kimaisha zinakwenda vizuri tofauti na ilivyokua awali.

''Sasa naweza kumlipia mwanangu kila mwaka shilingi 15,000/= za Skuli, nimenunua friji nauza juisi, nimejenga banda nauza uji  , nilikua sina uwezo wowote kipindi cha nyuma lakini hivi sasa mambo yanakwenda vizuri , maana muda mwengine hata mumewangu huchachiwa na akataka nimuazime chochote na nikampatia '', alisema Lela.

Lela, alieleza  ukiachilia mbali mafanikio hayo lakini pia hivi sasa anaona ndoa yake ipo salama kwani ikitokea mume amekosa, chakupika hakikosi ndani ya nyumba na akirudi chakula tayari wanakula na mambo yanaendelea kama kawaida.

Kwa upande wake,  Katibu wa kikundi cha Tekeleza   Muhammed Bakar Omar, alisema  lengo la kikundi chao ni kuondosha utegemezi wa kimaisha kwa wananchi  na kila mmoja awe na nyenzo ya kujipatia kipato katika maisha.

Alifahamisha kituo chao cha Tekeleza ni katika mradi wa ASSP  ambao umelenga kuwakomboa wananchi kiuchumi na hadi hivi sasa harakati za kuwaelemisha zinaendelea vizuri ikiwamo katika sekta ya Kilimo na ufugaji.

'' Tunawafundisha mbinu bora za kilimo na ufugaji , yoyote atakaekuwa tayari nasi huwa tayari kumwelekeza na kisha anaona matunda yake'' ,alisema katibu huyo.

Katibu huyo, alieleza ingawa mafanikio ni mengi katika kikundi hicho kama vile kutoa wanachama wengi ambao wanajitegemea lakini pia wanakabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile ukosefu wa pesa za kumalizia jengo pamoja na kutokuwepo kwa huduma ya umeme ambayo ni muhimu sana kutokana na kazi zao.

Hivyo aliwaomba wadau wa maendeleo na washirika wengine kujitokeza kusaidia katika utatuzi wa changamoto hizo ili yale malengo yaliyokusidiwa yafikiwe kwa wepesi zaidi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.