Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Shein Mgeni Rasmin Sherehe za Wafanyakazi Mei Mosi Kisiwani Pemba Kesho.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kesho anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), zinazotarajiwa kufanyika Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Katika maadhimisho hayo, Dk. Shein anatarajiwa kupokea maandamano ya wafanyakazi wa sekta za umma na sekta binafsi ambapo pia, salamu mbali mbali zitatolewa zikiwemo kutoka Shirika la Kazi Duniani (ILO), Jumuiya ya Waajiri Zanzibar (ZANEMA), salamu za Waziri, Mkuu wa Mkoa, risala ya wafanyakazi na hatimae, Rais atatoa zawadi na kuwahutubia wafanyakazi.

Kila ifikapo Mei Mosi ya Kila mwaka, Zanzibar huungana na nchi nyengine duniani katika kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani ambapo hapo mwaka jana maadhimisho hayo yalifanyika katika kiwanja cha Mpira Mahonda, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Kauli mbiu ya mwaka huu katika maadhimisho hayo inasema ‘Njia Pekee ya Kukuza Uzalishaji na Kuimarisha Huduma ni Kujadiliana na Kujali Ushirikishwaji”.

Katika hotuba zake mbali mbali anazotoa Rais Dk. Shein amekuwa akisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na utaratibu wake wa kuzilinda haki za wafanyakazi na kuimarisha maslahi ya wafanyakazi hatua kwa hatua.

Katika hotuba yake ya kuzindua Baraza la Nane la Wawakilishi tarehe 11 Novemba mwaka 2010 Rais Dk. Shein alieleza bayana mtazamo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba kuhusu wafanyakazi ambapo alisema “Rasilimali moja kubwa ya nchi ni wafanyakazi ambapo ndio msingi wa kujenga uchumi na maendeleo yote ya nchi”.

Aidha, katika kutilia mkazo suala la umuhimu wa kushirikiana na vyama vya wafanyakazi alisema kuwa “ Maslahi bora ya wafanyakazi popote ni ajenda yetu na tutahakikisha mashirikiano na chombo chao ‘Shirikisho la vyama huru vya wafanyakazi’ na kukuza mahusiano mema”.
Kama inavyofahamika kuwa wafanyakazi ni muhimu katika maendeleo ya Taifa lolote lile kwani ni rasilimali inayotegemewa katika kuzalisha mali na kunyanyua uchumi wa nchi.

Kwa kutambua hilo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikichukua hatua mbali mbali kujenga mazingira mazuri kwa wafanyakazi ili waweze kuzalisha zaidi na kuongeza pato la Taifa.

Siku hii ya Mei Mosi inatokana na historia ya maandamano yaliyotokea  Chicago nchini Marekani mnamo mwaka 1886 ambapo zaidi ya wafanyakazi 300,000 waliandamana wakidai haki zao za msingi.
  
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.