Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Mabalozi wa Wilaya ya Dimani Kichama.


MAKAMO Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar Dk.Ali Mohamed
Shein amewaeleza viongozi wa CCM wakiwemo Mabalozi kuwa njia pekee ya kuendeleza amani, utulivu na mshikamano ni kuwepo kwa uongozi wa CCM madarakani.

Dk. Shein aliyasema hayo katika mkutano kati yake na Mabalozi wa CCM wa Wilaya ya Dimani Kichama, mkutano uliofanyika katika ukumbi wa CCM Mkoa wa Mjini uliopo Amani mjini Unguja huku akitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa ushindi kwa CCM.

Katika hotuba yake alieleza kuwa amani, utulivu na umoja ndio Sera kubwa ya CCM na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kusisitiza kuwa amani inadumi zaidi pale inaposhughulikiwa na CCM, kwani viongozi wake wamekuwa wakiisisitiza amani na kuitekeleza kwa vitendo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa wapo viongozi wamechaguliwa na wananchi lakini wamekuwa wakiwapiga chenga wananchi waliowachagua na hawaendi katika maeneo waliochaguliwa kwenda kuwatumikia wananchi hao ikiwa ni pamoja na kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza kuwa iwapo hawana uwezo wa kuzitatua changamoto hizo ni vyema wakawaeleze viongozi husika wakiwemo viongozi wa ngazi za juu wa chama chao.

Dk. Shein alisisitiza haja kwa viongozi wa CCM wakiwemo Wabunge, Wawakilishi na Madiwani kuwaeleza wananchi mafaniko ya Serikali yao yaliyopatikana yakiwemo kuimarika kwa huma za jamiio zikiwemo elimu, afya, biashara, mazigira na  nyenginezo.


Aliwaeleza viongozi hao wa Wilaya ya Dimani kuwa ni lazima kanuni na maadili ya chama hicho yafuatwe hasa pale unapokaribia uchaguzi mkuu ili wawe wamoja kwa vitendo na kujidhatiti katika kuiletea ushindi CCM.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kulitafutia ufumbuzi tatizo la maji tokea awamu ya kwanza ya uongozi wa SMZ, ambapo hali ya matumizi ilikuwa ndogo kutokana na idadi ya watu wakati ule na ilivyo hivi sasa.

Alieleza kuwa changamoto kubwa iliyopo hivi sasa ni kupungua kwa maji katika vyanzo vya maji hasa kwa vianzio vinavyotoa maji kwa mji wa Zanzibar na kusisitiza kuwa tayari Serikali imeanza kulichukulia hatua suala hilo.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaweka mtandao mpya wa maji katika mji wa Zanzibar na ule mkongwe utafumuliwa kwani tayari visima kadhaa vimeshachimbwa na baadhi yake vimeshawekewa vifaa na bado vifaa vyengine vimeshaagiziwa hivi karibuni vitawasili.

Alirejea kauli yake ya kulitafutia ufumbuzi tatizo la kutuama kwa maji katika eneo la Mwanakwerekwe ambapo alieleza kuwa eneo hilo litajengwa ili maji yaende na yakienda yatoke pamoja na kuwekwa mabomba makubwa kuelekea baharini na kusisitiza kuwa fedha zipo zipatazo Dola milioni 33 za mkopo kutoka Benki ya Dunia.

Aidha, alieleza kuwa sehemu ya Pili ya Mradi wa Huduma za Jamii Mjini (ZUSP) ambapo sehemu ya pili ni barabara yenyewe kujengwa upya na kuinuliwa na kwa eneo la Kibondemzungu barabara nayo itainuliwa na kujengwa njia mbili ya kwenda na kurudi. Pia, alieleza kuwa barabara ya Kiembesamaki nayo itainuliwa.

Hata hivyo, aliwataka Mabalozi kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha wananchi juu ya usafi wa mazingira kwa lengo la kupambana na maradhi mbali mbali.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dk. Abdalla Juma Mabodi alieleza majukumu ya Mabalozi na kusisitiza kuwa Mabalozi ni jeshi kubwa katika kuipatia ushindi na kueleza kuwa Wilaya ya Dimani hakuna makundi ya CCM bali wote ni wamoja.

Mabodi alisisitiza kuwa ni vyema kwa viongozi wa Chama kueleza mafanikio yaliopatikana kutokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM pamoja na kwenda kwa wananchi kuwa kusikiliza changamoto zinazowakabili.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi Mohammed Rajab Soud alizipongeza juhudi za Rais Dk. Shein na kutumia fursa hiyo kueleza kuwa wanasikitishwa na baadhi ya watendaji ambao wanafanya kazi kinyume na matakwa ya Serikali na wananchi.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Dimani Hussein Ali Mjema (Kimti) alimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa vitendo pamoja na kusimamia vyema amani na utulivu kuahidi kuendelea kushirikiana nae.

Nao Mabalozi wa Wilaya ya Amani katika taarifa yao iliyosomwa na Balozi Mwanakheir Idd Ramadhan  walimpongeza Rais Dk. Shein pamoja na Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk. John Magufuli kwa kusimamia kwa nguvu Ilani ya CCM  na hatimae kupata maendeleo makubwa na kupunguza kero kwa wananchi.

Walieleza kuwa CCM ndio mtetezi wao na ndio sauti yao kwani ndio chama kinachotetea haki ya ukweli na ndio chama wanachokiona kinachosimamia na kudumisha amani na utulivu.

Walieleza kuwa ushindi wa CCM unatokana na wanaCCM wenyewe pamoja na wananchi wanaokiunga mkono chama hicho kutokana na Sera zake lakini pia Mabalozi ndio nguvu kazi ya CCM kwa kuwahamasisha wananchi kujiandikisha katika daftari la kudumu laMpiga kura.

Sambamba na hayo, Mabalozi hao walieleza changamoto zilizopo katika Wilaya hiyo ya Dimani ikiwa ni pamoja na uhaba wa maji safi na salama, ubovu wa barabara za ndani,uhamiaji na ujenziholela, kilio cha Mwanakwerekwe na Kibondemzungu, kucheleweshwa kwa ugawaji wa viwanja kwanajili ya kujenga kwa maeneoya Fumba na Bweleo na nyenginezo.

Hata hivyo, Mabalozi hao walimuhakikishia Makamo Mwenyekiti huyo kuwa wataimarisha umoja na mshikamano ndani ya Chama chao na kufanya kazi kila inavyowezekana ili CCM ipate ushindi mkubwa na kuweza kuendeleza amani na utulivu.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.