RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kwamba maonyesho ya Utalii yanayofanyika
Zanzibar ni muhimu kwa Serikali na wananchi kwa kuwa yamelenga kuitangaza
Zanzibar na sekta ya utalii ambayo ndio muhimili mkuu wa uchumi.
Dk. Shein aliyasema hayo
leo huko katika viwanja vya hoteli ya Verde, Mtoni Mjini Zanzibar katika
ufunguzi wa maonyesho ya Utalii Zanzibar ya mwaka 2018 ambayo yalihudhuriwa na
viongozi mbali mbali wakiwemo Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Pili wa rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd,
wadau wa utalii na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali pamoja
na wananchi.
Katika maelezo hayo,
Rais Dk. Shein alisema kuwa Utalii umekuwa ukichangia asilimia 27 kwa Pato la
Taifa na asilimia 80 ya fedha za kigeni zinazokusanywa ambapo muda wanaokaa
watalii nchini umeongezeka ambapo hivi sasa mtalii hutumia wastani wa siku 8
badala ya 6 kama ilivyokuwa miaka 5 iliyopita.
Alifahamisha kwamba
takwimu hizo ni njema kwa Serikali, wanchi, wawekezaji na wadau wote katika
sekta ya utalii kwa kuwa zinabainisha kwamba sekta ya utalii imekuwa ikikuwa
kwa kasi na watalii wanapenda kubakia nchini huku wakiwa tayari kutumia fedha
wanazokuja nazo kufurahishwa na ukarimu wa watu wa Zanzibar.
Rais Dk. Shein alieleza
juhudi mbali mbali za kuimarisha utalii zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali
zikiwemo kuanzisha mpango wa “Utalii kwa wote” ambapo lengo kuu la mpango huo
ni kuhakikisha kwamba sekta ya utalii inawanufaisha wananchi wote wa Zanzibar
na kuimarisha ustawi wa wananchi kwa jumla.
Alisisitiza kuwa juhudi
mbali mbali zinaendelea kuchukuliwa na Serikali za kuendeleza sekta ya utalii
zinaenda sambamba na mikakati na malengo ya MKUZA, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya
mwaka 2015-2020 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa
(SDGs).
Alieleza imani yake
kwamba maonyesho hayo ni njia bora na madhubuti ya kuitangaza Zanzibar pamoja
na fursa mbali mbali zilizopo za kiuchumi kwa wawekezaji ambapo pia, washiriki watazifahamu
fursa zilizopo nchini na haja ya washiriki hao kuzichangamkia.
Alisema kuwa Zanzibar
imejaaliwa na mazingira yanayovutia na ina vivutio vingi vya utalii zikiwemo
fukwe na sehemu za historia pamoja na hoteli nyingi za kisasa ikiwemo Hoteli
hiyo ya Verde.
Rais Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kueleza juhudi kubwa zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha
miundombinu ya barabara kwa kuzijenga upya na kuzifikisha katika maeneo muhimu
ya utalii kwa lengo la kuimarisha sekta hiyo sambamba na shughuli za uwekezaji
na huduma kwa wananchi.
Alieleza historia ya
Zanzibar kwa kubainisha kwamba Zanzibar ilikuwa ni kituo kikuu cha Biashara
katika Afrika ambacho kilikuwa kikiwavutia wafanyabiashara na wavumbuzi kutoka
Mataifa mbalimali ya Ulaya, Asia na Mashariki ya Kati na Mashariki ya mbali.
Aidha, Rais Dk. Shein
aliiagiza Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kuhakikisha kuwa watu
wanaotembeza wageni wawe wamepatiwa mafunzo yanaayostahiki, wawe na vibali na wahakikiwe
kila baada ya muda ili kuhakikisha kwamba hawaharibu historia ya Zanzibar kwa
kuisimulia isivyo au kwa kuzingatia matakwa na utashi wao binafsi.
Dk. Shein alieleza juu
ya dhamira ya Serikali ya kuifikisha Zanzibar katika kiwango cha nchi zenye
uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020 na kubainisha kwamba hivi sasa wawekezaji
wengi wamekuwa wakija nchini kutokana na kuziamini Sera pamoja na mazingira
mazuri yalioandaliwa na Serikali.
Alieleza kuvutiwa na
maudhui ya maonyesho hayo isemayo “Responsible Tourism for a Better and Greener
Tomorrow”,akiwa na maana kwua Utalii anaotilia mkazo uhifadhi wa mazingira kwa
lengo la kuleta mustakbali mwema kwa maisha ya baadae.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza juhudi zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
za kukuza hali ya usalama ndani ya mji Mkongwe wa Zanzibar ambao ndio mafanikio
maarufu ya utalii na urithi wa kimataifa kama ulivyotambuliwa na UNESCO.
Akieleza juu ya
utekelezaji wa mradi mkubwa wa ufungaji wa kamera katika Mji Mkongwe wa
Zanzibar uliofanywa na Serikali aliouzindua tarehe 04 Oktoba, 2018 na
kufahamisha hivi sasa Mji wa Zanzibar na maeneo yake yako katika usalama zaidi
kwa wakaazi wake wawekezaji na watalii.
Kadhalika alifahamisha
kwamba katika malengo na juhudi za Serikali katika utekelezaji wa mradi wa
Huduma za Mji (ZUSP) ambao pamoja na mambo mengine umelenga kuimarisha
upatikanaji wa huduma za mji pamoja na kuyatunza majengo ya urithi wa utamaduni
na mazingira ya asili ya Mji Mkongwe.
Rais Dk. Shein alieleza
azma ya Serikali kulifukia eneo la babari la Gulioni kama alivyofanya mfanya
biashara maarufu Said Baghresa la kufukia bahari katika eneo la Hoteli ya Verde
sambamba na ujenzi wa miji ya kisasa katika eneo la Kwahani na Chumbuni na
kueleza kuwa Zanzibar itabadilika sio muda mrefu na kusisitiza falsafa yake ya
kutofanya kazi kwa mazoea kuwa ni vyema ikachukua mkondo wake.
Katika hafla hiyo, Rais
Dk. Shein alitoa vyeti maalum kwa wadau mbali mbali waliosaidia kuutangaza
utalii wa Zanzibar ndani na nje ya nchi kwa kutumia huduma wanazoziendesha
yakiwemo makampuni mbali mbali, hoteli, Jumuiya na Taasisi.
Mapema Rais Dk. Shen
alitembelea mabanda maalum ya maonyesho yaliyozishirikisha Kampuni mbali mbali
za kitalii, taasisi binafsi na za umma, Kampuni zinazotoa huduma za kitalii,
Jumuiya pamoja na Hoteli za Kitalii.
Nae Waziri wa Habari,
Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shen
kwa juhudi zake za kuimarisha sekta ya Utalii ikiwa ni miongoni mwa utekelezaji
wake wa Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2015-2020.
Waziri Kombo alieleza
kuwa Wizara yake imo katika hatua za kuhakikisha inavuka lengo la kufikia
watalii nusu milioni kwa mwaka na kueleza kuwa lengo hilo litavukwa kwani
alithibitisha kuwa hadi Julai mwaka huu walifikia watalii 263,000 ambapo
wakiendelea na hatua hiyo hadi mwisho wa mwaka huu watafikia watalii 520,000.
Mapema Katibu Mkuu wa
Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale Khadija Bakari Juma alieleza hatua
zilizochukuliwa na Wizara pamoja na wadau wengine wa utalii na wafadhili
wengine katika kufanikisha maonyesho hayo yenye lengo la kuimarisha sekta ya
utalii nchini.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment