Habari za Punde

Misaada Mbalimbali Iliyotolewa na Chuo Kikuu Cha "Houkeland University Hospital" Imekwenda Sambamba na Dhamira ya Serikali.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Ujumbe wa Madaktari kutoka Nchini Norway wa Chuo Kikuu cha "Houkeland University Hospital " ukiongozwa na Katibu Mtendaji Mr. Eivind Hamsen,kushoto wa kwanza.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohammed Shein amesema misaada mbali mbali iliyotolewa na Chuo Kikuu ‘Houkeland University Hospital’, imekwenda sambamba  na dhamira ya muda mrefu ya Serikali ya kutoa huduma bora za tiba ya akili kwa wananchi wake.

Dk. Shein amesema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, alipozungumza na ujumbe wa Madaktari wanne kutoka chuo kikuu cha ‘Houkeland University Hospital’ cha nchini Norway, ukiongozwa na Katibu Mtendaji Eivind Hamsen.

Alisema kwa nyakati tofauti Serikali kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo imekuwa ikifanya kila juhudi kuhakikisha inaimarisha upatikanaji wa huduma za tiba ya akili katika Hospitali yake iliopo Kidongochekundu mjini hapa na kuondokana na dhana iliyojengeka miongoni mwa jamii kuwa eneo hilo ni ‘jela’ ya wagonjwa hao.

“Serikali imekuwa ikifanya kila juhudi kuimarisha Hospita hiyo, ili ionekane ni kituo cha tiba ya akili, sio tena jela ya wendawazimu kama ilivyokuwa ikitambulika mara baada ya kuanzishwa kwake”, alisema.

Alisema juhudi hizo ziliambatana na uanzishaji wa sera mpya  na sheria za uendeshaji wa hospitali hiyo, zikilenga kuleta mageuzi makubwa katika suala la upatikanaji wa huduma bora kwa wagonjwa.

Alisema tayari kuna mafanikio makubwa yaliofikiwa, katika upatikanaji wa huduma za tiba ya akili, huku mkazo ukielekezwa kukiimarisha zaidi.

Katika hatua nyengine  Dk. Shein alisema Zanzibar imepata mafanikio makubwa katika sekta ya Afya, kwa kuiimarisha Hospitali kuu ya Mnazi mmoja, Hospitali za Wilaya pamoja na vituo vya Afya Unguja na Pemba, kwa kuvipatia vifaa vya kisasa na mafunzo kwa madaktari wake.
“ Kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo tumeimarisha Hospitali kuu ya Mnazi mmoja na zile zilioko Wilayani, huduma mbali mbali zinapatikana kwa urahisi na bila ya malipo yoyote; kama vile MRI,  watu wamekuwa wakitoka nje ya Zanzibar kufuta matibabu hapa”, alisema.

Nae, Kiongozi wa ujumbe huo kutoka ‘Houkeland University Hospital’ COE Elvind Hamsen, alisema wameridhishwa na juhudi kubwa zilizochukuliwa na Serikali katika kuiendeleza Hospitali hiyo, sambamba na huduma bora zinazotolewa na wafanyakazi wake.

Alisema Chuo hicho kitaendeleza ushirikiano uliopo ili kuimarisha upatikanaji wa huduma kwa maslahi ya jamii ya Wazanzibari.

“Hatuhesabu kiwango gani cha fedha zimetumika, bali tunazingatia vipi upatikanaji wa huduma zitakavyoimarika”, alisema Hamsen.

Aidha, kiongozi huyo alimhakikishia Rais wa Zanzibar kuwa Chuo hicho kitasaidia uanzishaji wa Hospital kuu ya kisasa, inayotarajiwa kujengwa katika eneo la Binguni, Mkoa Kusini Unguja.

Chuo kikuu cha Houkeland University Hospital, kimekuwa na mradi wa kuisaidia Hospital ya Wagonjwa wa Akili, Kidongochekundu kupitia Nyanja mbali mbali ikiwemo kuboresha kitengo cha Pathology,ecology  pamoja na kutoa mafunzo mbali mbali kwa watendaji katika masuala ya tiba ya akili.


Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.