Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Shein Azungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchini Mhe. Kangi Lugola.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amezipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Idara za Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha Zanzibar inaedelea kuwa salama.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokutana na uongozi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulioongozwa na Waziri wa Wizara hiyo Kangi Alphaxard Lugola uliofika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais ambapo viongozi wengine waliofutana na Waziri Lugola ni Meja Jenerali Jacob Gideon Kingu, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara Kailima Ramadhan.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliueleza uongozi huo kuwa Zanzibar iko salama hali ambayo imeweza kuwapelekea wananchi wake waendelee kuishi kwa amani na utulivu mkubwa.

Rais Dk. Shein alisema kuwa hatua hiyo inatokana na juhudi kubwa zinazoendelea kuchukuliwa na vikosi vyote vya Idara zilizomo katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi likiwemo Jeshi la Polisi, Uhamiaji pamoja na Idara ya Vitambulisho vya Taifa.

Alieleza kuwa kupungua kwa vitendo vya uhalifu kwa asilimi 34 pamoja na makosa madogo kwa asilimi 57 kwa kipindi cha Januatri hadi Oktoba mwaka huu, kumeonesha wazi kuwa mafanikio makubwa yanaendelea kupatikana katika kudumisha amani, utulivu na usalama hapa Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa kazi imefanywa vizuri sana hadi kufikia hatua hiyo ya mafanikio na kueleza imani yake kubwa aliyonayo kutokana na uongozi wa Wizara hiyo ambao umeanza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Alieleza kuwa viongozi hao wameingia na rekodi nzuri hatua ambayo imepelekea kuendelea kuimarika kwa hali ya utulivu amani na usalama kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kuzitumia vyema Idara zake katika kutekeleza majukumu yao kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili malengo ya waasisi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yaweze kufikiwa.

Dk. Shein aliueleza uongozi huo juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilizozichukua katika kuhakikisha vitendo vyote vinavyohatarisha amani na usalama vinadhibitiwa ipasavyo kwa kuandaa mikakati maalum ili wananchi na mali zao pamoja na wageni wanaoitembelea Zanzibar wakiwemo watalii wanakuwa salama kwa kuweka vifaa maalum vya kisasa vya ulinzi.
  
Rais Dk. Shein alisema kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba sifa njema ya Zanzibar kuwa ni sehemu salama yenye utulivu inabakia na inakuwa ya kudumu na inaendelea kuwa ni kichocheo cha kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi katika nyanja zote ikiwemo sekta ya utalii.

Alieleza kuwa Serikali imeamua kuweka vifaa hivyo kwa lengo la kuimarisha usalama katika mji wa Zanzibar kwani vinauwezo mkubwa wa kuwabaini wahusika wa matukio mbali mbali kwa haraka na ufanisi mkubwa pamoja na kuyabaini matukio ya magendo ya bidhaa kadhaa kwa kuwepo ulinzi katika maeneo ya baharini na angani kupitia vifaa hivyo maalum vya kisasa.

Mapema Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Alphaxard Lugola alimueleza Rais Dk. Shein mikakati maalum iliyowekwa na Wizara yake katika kuhakikisha ulinzi, amani na usalama inakuwa ya kudumu hapa Zanzibar.

Waziri Lugola alimueleza Dk. Shein kuwa kwa kipindi cha muda wa kuanzia Januari hadi Oktoba mwaka huu matukio ya uhalifu hapa Zanzibar yamepungua kwa asilimia 34 na makosa madogo yamepungua kwa asilimia 57 ukiwemo ukiwemo udhibiti wa dawa za kulevya.

Waziri Lugola alitoa shukurani kwa Dk. Shein kwa kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaendelea kuishi kwa amani, utulimu na usalama mkubwa na kumuhakikishia kuwa vikosi vyake vya ulinzi vinasimama imara ili dira ya Zanzibar ya kudumisha amani  inafikiwa.

Aidha, Waziri Lugola alieleza kuwa bado changamoto ya magendo wanaendelea kupambana nayo kwani anatambua kuwa magendo yanahujumu mapato na uchumi wa Serikali.

Alisema kuwa Idara zilizomi katika Wizara hiyo ambazo ni za Muungano zimekuwa zikifanya juhudi kubwa katika kutekeleza majukumu yake likiwemo Jeshi la Polisi, Uhamiaji na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Waziri huyo alieleza kuwa Idara ya Uhamiaji imekwua ikifanya kazi kubwa ya kuwadhibiti wageni wanaoingia nchini na wanaotoka ili waingie na kutoka kihalali pamoja na kutumia pasi za kusafiria kwa njia ya elektroniki, visa na vibali vya kazi.

Aliongeza kuwa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), ina kazi kubwa ikwia ni pamoja na kuwatambua wananchi, kuwasajili sambamba na kuwatambua wageni wanaokaa kihalali sambamba na kwuapatia wakimbizi vitambulisho kwa wale waliotimia kuanzia umri wa mika 18. Alieleza kuwa tayari hadi Oktoba mwaka huu Mamlaka hiyo imeshasajili wananchi wapatao 652,000 na asilimia 90 wameshapatiwa vitambulisho vyao vya Taifa hapa Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.