Naibu Waziri
wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella Manyanya, akisisitiza jambo
kwenye kikao na wawakilishi wa Umoja wa Wabanguaji Wadogo wa Korosho
Tanzania(UWWKT) kilichofanyika kwenye hoteli ya Lindi Sea View. Pembeni ya
Naibu Waziri ni Mkuu wa Wilaya ya Lindi, mhehsimiwa Shaibu Ndemanga, Mkurugenzi
Mkuu wa SIDO Profesa Sylvester Mpanduji na kulia ni Mwenyekiti wa UWWKT Tumpale
Magehema
Mwenyekiti wa Umoja wa
Wabanguaji Wadogo wa Korosho Tanzania (UWWKT) Bi. Tumpale Magehema akisoma
risala mbele ya Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, mhandisi Stella
Manyanya alipofanya kikao na baadhi ya wanachama wa umoja huo mjini Lindi.
Baadhi ya
wanachama wa Umoja wa Wabanguaji Wadogo wa Korosho Tanzania (UWWKT)
wakimisikiliza mgeni rasmi (hayupo pichani) Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara
na Uwekezaji, mhandisi Stella Manyanya. Umoja huo wa wabanguaji wadogo wa
korosho umeonesha nia ya kubangua korosho iliyonunuliwa na serikali.
Naibu Waziri
wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, mhandisi Stella Manyanya(katikati walioketi)
kwenye picha ya pamoja na wawakilishi wa wanachama wa Umoja wa Wabanguaji
Wadogo wa Korosho Tanzania (UWWKT). Wengine walioketi kuanzia kushoto ni
Mkurugenzi Mkuu wa SIDO, Profesa Sylvester Mpanduji, Mkuu wa Wilaya ya Lindi,
Shaibu Ndemanga, Mwenyekiti UWWKT Tumpale Magehema na Mkurugenzi Mtendaji wa
ANSAF, Audax Rukonge.
Na Mwandishi Wetu
Uamuzi
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, kununua
korosho za wakulima na kuzibangua nchini umepongezwa na Umoja wa Wabanguaji
Wadogo wa Korosho Tanzania (UWWKT).
Akisoma
risala mbele ya Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella
Manyanya, Mwenyekiti wa umoja huo Bi. Tumpale Magehema amesema uamuzi wa Rais
Magufuli una nia ya kuwapa ajira wanachama wake wapatao 2881, jambo ambalo ni
la kupongezwa.
Licha
ya kutoa ajira Bi. Tumpale ameueleza uamuzi huo wa kijasiri uliofanywa na Rais
Magufuli utaongeza ari ya kufanya kazi na kuchochea ukuaji wa uchumi hasa
kwenye mikoa inayolima korosho kwa wingi.
Akitoa
taarifa kwa mgeni rasmi, Katibu wa umoja huo Bw. Audax Mkongi, alimueleza mhandisi
Manyaya kuwa umoja huo ni asasi mwamvuli ya kitaifa ya wabanguaji wadogo yenye
jumla ya vikundi 183 kutoka wilaya tisa za mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na
Morogoro. Baadhi ya wilaya hizo ni Ulanga, Tandahimba, Kisarawe, Liwale na
Ruangwa.
Kwenye
taarifa yake Bw. Mkongi amesema tangu umoja huo uanzishwe mwaka 2015
umefanikiwa kumiliki mashine za kubangua korosho ghafi kwa kutumia mkono 117,
mashine za kutumia miguu 317, mashine za kuchemshia (boiler) 23, mashine za
kupanga madaraja 12, mashine za kukaushia (oven) 12, na za kufungashia 14 zenye
uwezo wa kubangua korosho ghafi kg 25,370 kwa siku.
Kwa
upande wake mgeni rasmi kwenye hafla hiyo iliyofanyika kwenye hoteli ya Lindi
Sea View, Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Stella Manyanya
ameupongeza umoja huo kwa ari na nia ya kuunga mkono juhudi za serikali ya
awamu ya tano ya uchumi wa viwanda.
Licha
ya kuupongeza umoja huo, mhandisi Manyanya pia amewahakikishia ushirikiano
kutoka wizara yake na kwa kuanza
serikali inaandaa utaratibu wa kuutumia ili kuingia nao mikataba ya kubangua
korosho iliyonunuliwa na serikali msimu huu.
Wakati
huo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO), Profesa
Sylvester Mpanduji amesema taasisi yake itaendelea kushirikiana na Taasisi ya
Utafiti wa Kilimo Naliendele pamoja na wadau wengine wa korosho kutoa mafunzo
kwa wajasiriamali wadogo na wa kati ili kuongeza thamani na ubora wa zao hilo
ambalo linaongoza kwa kuliingizia taifa fedha za kigeni.
No comments:
Post a Comment