Habari za Punde

ZSTC Yatimiaza Miaka 50 Tangu Kuanzishwa Kwake Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC) hafla hiyo ya maadhimisho hayo imefanyika katika viwanja vya Hoteli ya Kitalii ya Verde Mtoni Zanzibar.   


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameitaka Wizara ya Biashara na Viwanda pamoja na uongozi wa Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC), kufanya utafiti wa mimea na mazao ya kibiashara, ili kuyaongezea thamani na kuimarisha uchumi wa taifa.

Amesema utafiti unapaswa kufanyika ili kupanua wigo wa matumizi ya bidhaa zinazozalishwa, ikiwemo karafuu.

Dk. Shein amesema hayo jana katika viunga vya Hotel Verde iliyoko Mtoni mjini hapa, katika maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Shirika la ZSTC.

Maadhimisho  hayo yaliwashirikisha viongozi wa Serikali, wafanyakazi pamoja na wadau mbali mbali wa mazao ya biashara yatokanayo na kilimo, ikiwemo wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Alisema wakati umefika kwa ZSTC kuwa na kitengo maalum kitakachojitegemea na kufanya kazi za utafiti, kwa kushirikiana na Wizara za Kilimo, maliasili, mifugo na uvuvi na taasisi nyenginezo za utafiti, ikiwemo COSTECH ili kuziongezea thamani ya bidhaa zinazotengenezwa.

Alisema mafuta yatokanayo na mimea hiyo, hususan karafuu ni nyenzo kuu ya kiwanda cha makonyo, na kubainisha haja ya kuendelezwa mazao mengine ya biashara yatakayoleta tija kwa Taifa.
“Napenda kutowa wito maalum kwenu uongozi wa Wizara Biashara na Viwanda pamoja na ZSTC kutilia maanani suala la kufanya utafiti ili kupanua wigo wa matumizi wa mazao tunayozalisha , sote tunaelewa karafuu ina matumizi mengi ikiwemo utenegenzaji wa dawa za meno,dawa za tiba lakini pia huongeza ladha katika sigireti, wakati mafuta yatokanayo na mimea  hutumika kwa masaji na kuongeza ladha ya chakula”, alisema.
         
Alipongeza juhudi zinazoeendelea kuchukuliwa na Shirika hilo katika kuwahudumia vyema wakulima wa karafuu pamoja na kuwahamasiha katika kilimo cha mazao ya viungo, hivyo  akaitaka Wizara ya Biashara na Viwanda kusimamia dhamira ya Serikali ya kuitaka ZSTC kufanya biashara nyengine na kujiimarisha.

Dk. Shein alipongeza juhudi zilizonyika za kukiimarisha kiwanda cha uzalishaji wa mafuta ya makonyo na mime mingine kiliopo Wawi Pemba, kwa kupata Mwekezaji na kuongeza uzalishaji, hatua aliyosema inaendeleza sekta ya uwekezaji pamoja na ukuaji wa sekta ya viwanda.

Aidha, Dk. Shein alipongeza mafanikio makubwa yaliopatikana katika uimarishaji wa zao la Karafuu, hatua aliyosema inatokana na mageuzi makubwa ya Shirika la ZSTC.

Alieleza kuwa uamuzi huo wa Serikali ulitokana na Ilani ya CCM (2010-2015), kwa kubadilisha muundo na mfumo wa uendeshaji wa shirika pamoja na sera ya malipo kwa wakulima wa zao hilo.

“Mnamo mwaka 2011 Serikali ilitunga sheria mpya ya ZSTC namba 11 ya mwaka 2011, inayoipa mamlaka makubwa zaidi ZSTC kulisimamia,kulihudumia,kuliimarisha na kuhakikisha zao hilo linapata maendeleo endelevu kwa maslahi ya wakulima wetu”, alisema.

Alisema  miongoni mwa mafanikio yaliopatikana kutokana na hatua hiyo ni pamoja na kuimarisha na kulinda ubora wa Karafuu za Zanzibar, kuongeza kiwango cha uzalishaji, sambamba na upandaji wa mikarafuu mipya.

Alibainisha kuwa utafiti wa ‘Zanzibar Woody Biomass Survey’, uliofanyika Novemba, 2013 umeonyesha mafanikio makubwa ya kiwango cha mikarafuu kuongezeka hapa nchini hadi kufikia 6,554,587, huku mikarafuu 2,700,000 iliyopandwa ikiainishwa kustawi na kuanza kuzaa.
    
Aidha, Dk. Shein alisisitiza ahadi ya serikali ya kuendelea kuwanufaisha wakulima wa zao hilo kwa kuwalipa asilimia themanini ya bei ya soko la Dunia, katika mazingira yote, iwe kupanda bei ama kushuka.

Alisema Serikali itaendelea na juhudi zake za kuwaondolea usumbufu wakulima katika usafirishaji wa zao hilo kuelekea vituo vya ununuzi kwa kuimarisha miundo mbinu ya barabara.

Alisema tayari Serikali imetowa agizo kwa kwa shirika la ZSTC, Wizara inayoshughulikia miundombinu, Ardhi na Kilimo kuchukuwa hatua za kuanzisha barabara zinazokwenda kwenye maeneo inayolimwa kwa wingi mikarafuu kisiwani Pemba.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alitowa wito kwa uongozi wa  ZSTC kuhakikisha inautumia ipasavyo muundo mpya wa Utumishi wa Shirika katika upandishaji wa madaraja (promotion) ya wafanyakazi, sambamba na kulitaka kubuni utaratibu wa kuwazawadia wafanyakazi wake (bonus) pale wanapofanya vizuri na kuvuka malengo waliyowekewa.

Mapema, Waziri wa Biashara na Viwanda Amina Salum Ali, alisema wakati Shirika la Biashara likiadhimisha miaka 50 ya kuanzishwa kwake, kuna umuhimu wa kufanya tathmin na kupanga mikakati mipya ya kuliendeleza, sambamba na kuwa na kauli moja na wadau wa biashara ya karafuu Duniani kote.
Alisema katika kipindi hicho, Shirika limepata mafanikio makubwa na hivyo kuwa na uwezo mkubwa wa kuchangia utoaji wa huduma za kijamii pamoja na kuimarisha uchumi wa taifa.

Nae, Mwenyekiti wa Bodi ya ZSTC, Kassim Ali alitowa pongezi kwa awamu zote saba za Uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa kulishughulikia vyema zao la karafuu pamoja na mazao mengine ya viungo, na hivyo kuleta ustawi wa kiuchumi.

Shirika la ZSTC lilianzishwa kwa sheria ya mashirika ya umma namba 1 ya mwaka 1968, likiwa miongoni mwa mashirika ya mwanzo ya serikali kuanzishwa baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.