Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Akizungumza na Uongozi wa ZBC na Bodi ya Wakurugenzi wa ZBC Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein,akizungumza na Bodi ya Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC na Uongozi wa Shirika hilo Ikulu Zanzibar.kulia Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee na kushoto Waziri wa Habari Utalii na Mambo ya Kale Mhe. Mahmoud Thabit Kombo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuendelea kuliimarisha Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) ili liweze kwenda na wakati uliopo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipokutana na Uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale, uongozi wa (ZBC) pamoja na Bodi ya Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa lengo la kuliimarisha Shirika hilo.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuwa (ZBC) ni Shirika la Utangazaji ambalo lina historia ya muda mrefu hivyo linapaswa kufanya shughuli zake kulingana na wakati uliopo bila ya kupoteza malengo ya kuanzishwa kwake.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweza kulibadilisha Shirika hilo kwa kununua vifaa mbali mbali vya kisasa vyenye uwezo mkubwa wa kurusha matangazo na utengenezaji wa vipindi na hivyo kuliwezesha Shirika kumudumu ushindani katika tasnia ya habari na mawasiliano.

Aliongeza kuwa juhudi za makusudi zimeendelea kuchukuliwa na Serikali katika kuhakikisha Shirika hilo linaimarika na linarudi katika uhalisia wake kama ilivyokuwa hapo siku za nyuma ambapo taasisi nyingi za habari za ndani na nje ya Tanzania zilijifunza kupitia Shirika hilo kongwe na lenye uzoefu mkubwa.

Dk. Shein amesisitiza haja kwa Shirika hilo kuandaa Mpango wa kuendeleza wafanyakazi wake ili liweze kuendelea kufanya kazi zake kwa ufanisi kulingana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea kukua kwa kasi ulimwenguni.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Shirika hilo kwa kufanikisha vyema Sherehe za Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 mwaka huu ambazo kilele chake kilifanyika huko uwanja wa Gombani Chake Chake Pemba hivi karibuni.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuyaendeleza malengo ya Shirika hilo la (ZBC )ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa, kuelimisha na kuiburudisha jamii.

Alifahamisha kuwa pamoja na kuwa Shirika hilo linapaswa kujiendesha kibiashara pia, ni vyema kuwa na mpango mkakati utakaozingatia malengo pamoja na vipaumbele katika utekelezaji wa shughuli zake.

Akizungumzia maendeleo ya Shirika hilo, Rais wa Zanzibar amesema kuwa (ZBC) imekuwa ikifanya vizuri hasa baada ya kupatiwa vifaa vya kisasa licha ya changamoto ndogo ndogo ambazo zimekuwa zikikabiliana nazo.

Nae Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahamoud Thabit Kombo alitoa pongezi zake kwa Rais Dk. Shein kwa juhudi zake anazozichukua katika kuhakikisha Shirika hilo linaimarika na linazidi kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Waziri Kombo alieleza kuwa licha ya kuwepo baadhi ya changamoto ambazo zinaendelea kufanyiwa kazi Shirika hilo limekuwa likifanya kazi zake vizuri na kuweza kutoa elimu ya televisheni na taarifa mbali mbali kwa jamii.

Nae Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisisitiza haja kwa wafanyakazi wa Shirika hilo kufanya kazi kwa mashirikiano ili kuweza kutekeleza malengo yaliowekwa.

Alieleza kuwa kutokana na wakati uliopo suala la teknolojia sambamba na kuwepo kwa mpango maalum wa kuliendesha Shirika hilo haliepukiki hivyo mashirikiano yanahitajika kati ya wafanyakazi, uongozi wa (ZBC), Bodi ya (ZBC) pamoja na uongozi wa Wizara.

Mapema uongozi wa (ZBC) ulieleza mafanikio na changamoto walizonazo na jinsi zinavyofanyiwa kazi kuzitatua hivi sasa huku wakitumia fursa hiyo  kutoa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa kuliendeleza na kuliimarisha Shirika hilo ikiwa ni pamoja na kulipatia vifaa vya kisasa.

Uongozi huo ulieleza juhudi zinazoendelea kuzichukua katika kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa na kueleza jinsi walivyofanikiwa katika utendaji wao wa kazi ikiwa ni pamoja na kuzalisha vipindi mbali mbali vya redio na televisheni kwa mwaka huu ikilinganishwa na mwaka jana.
  
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.