Habari za Punde

Mji wa Zanzibar Unakuwa Safi na Kuvutia Ili Kuurejesha Katika Haiba Yake ya Asili na Hatimai Kufikia Lengo la Kuwa Jiji.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akifuatilia maelezo ya ripoti ya Utekelezaji ya Mpango Kazi ya Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, ikiwasilishwa na Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Haji Omar Kheri, katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein,ameeleza haja kwa Baraza la Manispaa Mjini kuweka mikakati maalum katika kuendelea kuuweka Mji wa Zanzibar kuwa safi ili kufikia malengo ya kuufanya mji huo kuwa Jiji.
Hayo aliyasema katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ wakati ulipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Dk. Shein alieleza kuwa mji wa Zanzibar hivi sasa una wakaazi wengi sana hiyo ni kutokana na kuongezeka kwa mahitaji hali inayosababisha kuwepo kwa ongezeko kubwa la taka.

Hivyo, Rais Dk. Shein alieleza umuhimu kwa Ofisi hiyo kuweka mikakati maalum ya kuhakikisha Mji wa Zanzibar unakuwa safi na wa kuvutia ili kuurejesha katika haiba yake ya asili na hatimae kufikia lengo la kuwa Jiji.

Alieleza kuwa mji wa Zanzibar unatambulikana kitaifa na Kimataifa hivyo malengo ya kuufanya mji huo kuwa Jiji yatakapofikiwa hivi karibuni itazidisha hamu kwa wageni kuja kulitembelea kutokana na vivutio vyake mbalimbali vilivyomo ndani yake.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein alieleza juhudi mbalimbali za makusudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha mji wa Zanzibar unaimarika kwa usafi pamoja na kuwa salama kwa kuendeleza miradi kadhaa ukiwemo mradi wa Huduma za Miji (ZUSP).

Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Ofisi hiyo kwa juhudi zake katika Idara zake zote sambamba na mashirikiano yaliopo kwa uongozi pamoja na watendaji wa Ofisi hiyo.

Rais Dk. Shein pia, alisisitiza kuwa ugatuzi umeleta mabadiliko makubwa hivyo ni vyema kwa Ofisi hiyo kuendelea na mikakati yake ili kufikia malengo yaliokusudiwa.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake na juhudi zilizochukuliwa na Wizara husika zilizopewa kazi za kupeleka huduma za jamii katika kijiji cha Mgonjoni huku akieleza hatua zitakazochukuliwa katika kurekebisha barabara ya kuelekea kijijini huko baada ya mvua kuleta athari.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi wake huku akisisitiza haja ya utekelezaji katika suala zima la ugatuzi katika sekta zake zilizogatuliwa ikiwemo sekta ya afya, elimu na kilimo.

Nao Washauri wa Rais kwa upande wao walipongeza utekelezaji wa Mpango kazi huo na kusisitiza haja kwa Ofisi hiyo kupitia Mabaraza yake ya Manispaa kuendelea kusimamia vyema masuala ya usafi hasa katika mji wa Zanzibar.

Aidha, walieleza umuhimu wa kuangalia taratibu nzima za uendelezaji wa masoko makuu kutokana na kuonekana kuwa masoko hayo yamezidiwa na mahitaji ya wananchi wanaofuata huduma likiwemo soko la mboga Mombasa, soko la Darajani na soko la Mwanakwerekwe.

Mapema, Waziri wa Wizara hiyo Haji Omar Kheri akiwasilisha muhtasari wa Mpango kazi huo alieleza kuwa Serikali za Mikoa zimeendelea kudhibiti na kuitafutia ufumbuzi migogoro ya ardhi iliyopo kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zinazohusika na masuala ya ardhi.
Alieleza kuwa katika kipindi ha miezi tisa iliyopita idadi ya migogoro ya ardhi ilioripotwa ni 119 kati ya hiyo migogoro 57 sawa na asilimia 48 ya migogoro yote ilioripotiwa tayari imepatiwa ufumbuzi.
Aliongeza kuwa Serikali za Mikoa na Wilaya na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kushirikiakana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali zimefanya juhudi kubwa ya kuihamasisha jamii katika suala zima la uandikishaji wa wanafunzi wa maandalizi na msingi.
Pamoja na hayo, Waziri Kheri alisema kuwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa ma Idara Maalum za SMZ imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto.
Katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato katika Serikali za Mitaa, alisema kuwa Ofisi kwa kutumia wataalamu wa ndani imesimamia kwa kuhakikisha kila Manispaa, Baraza la Mji na Halmashauri zinakusanya mapato kutoka vyanzo vyake vya mapato katika mfumo wa kielektroniki.
Hivyo, alisema kuwa hadi kufikia Machi 2019, Halmashauri zote zimeunganishwa katika mfumo wa pamoja na ukusanyaji mapato na kuanza kutumia mashine maalum za kukusanyia mapato katika maeneo ya maegesho, masoko na vituo maalum vya ukusanyaji wa ada zitokanazo na maliasili zisizorejesheka.
Aidha, alisema kuwa katika kuimarisha taarifa za usajili wa matukio ya Kijamii, Ofisi imesimamia zoezi la uandikishaji wa vitambulisho vipya vya Mzanzibari Mkaazi ambalo lilifanyika katika Shehia zote 388 za Zanzibar.
Sambamba na hayo alieleza kuwa Ofisi imeendelea kuzifanyia matengenezo makubwa barabara za ndani katika kiwango cha lami, barabara zenye urefu wa kilomita 2.98 zimefanyiwa matengenezo kwa kiwango cha lami.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.