Habari za Punde

Uzinduzi wa Kitambulisho Kipya Cha Kisasa cha Mzanzibar Mkaazi (Smart Cards) Zanzibar Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni leo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akizindua Kitambulishi Kipya cha Kisasa cha Mzanzibar Mkaazi cha (SMART CARDS) kulia Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Miukoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ.Mhe. Haji Omar Kheri, hafla hiyo imefanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema matumizi ya Vitambulisho vipya vya Mzanzibari mkaazi (smart card) yataiwezesha serikali kuweka na kuhifadhi kumbukumbu za matukio ya watu wote katika Daftari la Usajili na Utambuzi.

Dk. Shein amesema hayo katika uzinduzi wa Kadi mpya za Kielektronik ya Mzanzibari mkaazi, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul wakil Kikwajuni mjini hapa.

Alisema matumizi ya vitambulisho hivyo vitaisaida Serikali, taasisi na watu binafsi kupanga vipaumbele vya utekelezaji wa shughuli mbali mbali zenye mnasaba na huduma za maendeleo ya kijamii.

Aidha, alisema kuwepo kwa mfumo huo wa matumizi ya vitambulisho vipya utaisadia serikali katika kuwatambuwa watu wanaostahiki kupata haki za msingi , kama ilivyobainishwa katika Katiba ya Zanzibar ya 1984.

“Itawezesha kumtambua mtu anaestahiki kupata haki yake kama vile malipo ya pensheni, haki za matibabu, kujiunga na masomo na nyenginezo”, alisema.

Dk. Shein alisema kutokana na vitambulisho hivyo Serikali itapata urahisi  katika suala zima la ukusanyaji wa mapato hivyo kuimarisha huduma muhimu za kijamii, ikiwemo afya, elimu, barabara pamoja na ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Alisema kimsingi Serikali inapaswa kuwa na nyenzo katika udhibiti wa amani na utulivu wa watu wake, hivyo ni dhahiri Vitambulisho vipya vitakavyotumika hivi sasa ni vyenye ubora wa hali ya juu na uwezo  wa kuhifadhi taarifa  nyingi za mtumiaji.

Alieleza kuwa vitambulisho hivyo vimetengenezwa kwa teknolojia ambayo sio rahisi 
kughushiwa, vikiwa na uwezo mkubwa wa kiusalama wa taarifa za mtumiaji, akibainisha kutumika  katika nchi kadhaa duniani.

Rais Dk. Shein alitowa wito kwa wakaazi wote wa Zanzibar waliofikia umri wa miaka 18 kwenda kujisajili katika ofisi za Wakala wa Usajili wa matukio ya Kijamii zilizopo katika Wilaya zote nchini, sambamba na wale ambao bado hawajajiandikisha kufanya hivyo.

Aidha, aliwataka watendaji wanaohusika na utayarishaji wa vitambulisho hivyo, kuwa makini na waangalifu katika utoaji wake.

Vile vile aliwataka Wakuu wa Mikoa kusimamia vizuri taarifa za uhakiki wa watu walioko katika maeneo yao, kuanzia ngazi za shehiya, wadi na Wilaya ili kuhakikisha wanawatambua wananchi wao na taarifa zao zilizo sahihi.

“Ni muhimu mlifanyie mapitio daftari la wakaazi katika shehiya, ambalo ndio msingi wa uthibitisho wa kujua taarifa za utambuzi na makazi ya watu waliomo katika maeneo yenu”, alisema.

Dk. Shein aliwataka wananchi kutambua jukumu la kuisadia Ofisi ya Wakala wa Usajili wa matukio ya kijamii katika kutambuwa wakaazi wa maeneo yao badala ya kuiachia jukumu hilo Ofisi hiyo pekee.

Aidha, aliwataka wananchi kuondokana na tabia ya kutumia njia za mkato katika upatikanaji wa vitambulisho hivyo, akibainisha hatua hiyo imekuwa chanzo cha kuibuwa rushwa.

“Naendelea kukunasihini watendaji wote wa Wakala wa Usajili wa matukio ya kijamii Zanzibar, mfanye kazi zenu kwa uadilifu, uzalendo na mfungamane na misingi ya haki na sheria pamoja na kufuata taaribu zilizowekwa katika kuendesha Ofisi ”, alisema.

Alisisitiza haja ya kulinda na kudumisha amani na utulivu uliopo nchini, akibainisha kuwa ni hazina isiyopaswa kuvurugwa na kusema bila ya kuwepo amani na utulivu nchini, hakutakuwa na meendeleo yoyote yatakayofikiwa,

Alisema kukamilika kwa mradi huo ni miongoni mwa hatua za utekelezaji wa Ilani ay Chama cha Mapinduzi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015-2020, inayolenga kuwapatia huduma bora wananchi.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein aliwakumbusha wananchi umuhimu wa kutembea na Kadi ya Utambulisho wa Mzanaiabari mkaazi mahala popote ndani ya nchi, akibainisha faida kubwa ya jambo hilo.

Mapema, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za mitaa na Idara maalum za SMZ, Haji Omar Kheir aliwataka wananchi wote wenye sifa za kisheria kufika katika vituo vya usajili vilivyopo kila Wilaya nchini.

Alisema vitambulisho vipya vya Mzanzibar mkaazi ndicho kitakachotumika katika upatikanaji wa huduma mbali mbali muhimu kama vile upatikanaji wa leseni, miamala ya fedha, mahitaji katika taasisi za umma pamoja na zile zenye mahitaji ya vitambulisho.

Aidha, alisema Wizara hiyo itaendelea kusimamia utoaji wa elimu kwa wananchi ili kutii sheria ya ukaazi na kupata fursa mbali mbali ziliopo nchini.

Nae, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Usajili na matukio ya kijamii Zanzibar, Dk. Hussein Khamis Shaaban alisema Ofisi hiyo itaendelea na mikakati ya kusajili na kuwapatia vitambulisho wananchi wote wenye sifa za kisheria.

Alisema mfumo wa vitambulisho  vya kielektronic ni ufunguo katika kufikia maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa pamoja na kudumisha ulinzi na usalama katika nchi.
Aidha, alisema Zanzibar inakabiliwa na changamoto kubwa ya uingiaji wa wageni kutoka nje, hivyo kuwepo kwa vitambulisho hivyo ni muhimu kwani kutawezesha kuwatambuwa wageni hao.

Katika hafla hiyo, pamoja na mambo mengine, Dk. Shein alipata fursa ya kutembelea Ofisi za Wakala wa Usajili wa matukio ya Kijamii Zanzibar ziliopo Mazizini na kuangalia vifaa mbali mbali vinavyotumika kutayarishia vitambulisho hivyo.

Aidha,  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za
SMZ Haji Omar Kheri alimkabidhi Dk. Shein Kitambulisho kipya cha Mzanzibari mkaazi , ambapo nae alipata fursa ya kuwakabidhi  viongozi mbali mbali wa serikali , akiwemo Mama Mwanamwema Shein pamoja na Wananchi kadhaa.    
       
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.