Habari za Punde

Tume yaombwa kufundisha elimu ya utawala bora nchini Kenya


Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu (kulia) akimkaribisha Kamishna Rose Macharia kutoka Kenya alipofanya ziara katika ofisi za tume jijini Dodoma
Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu akiongea na wageni wake kutoka Kenya waliotembelea ofisi za tume kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya utawala bora na maadili ya viongozi.
Kamishna wa tume, Dkt. Fatma Halfan akisisitiza jambo katika kikao kifupi kilichaofanyika Dodoma baina ya tume na ujumbe kutoka Tume ya Maadili na Kupambana na rushwa nchini Kenya Novemba 22,2019. Kushoto ni Mwenyekiti wa tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu.

Na Mbaraka Kambona
Kamishna wa Tume ya Maadili na Kupambana na Rushwa nchini  Kenya, Rose  Macharia ameikaribisha Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora (THBUB) kushirikiana  nao kufundisha elimu ya maadili ya viongozi katika chuo chao cha taifa cha maadili ili kukuza na kuimarisha utawala bora katika nchi hizo.

Macharia alitoa kauli hiyo katika ziara fupi aliyoifanya katika ofizi za Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora zilizopo Dodoma Novemba 22, 2019.

Akiongea katika kikao baina yake na Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu, Macharia alisema kuwa  wametembelea tume kwa sababu  wanatambua kuwa  hiyo  ni taasisi kongwe katika masuala ya usuluhishi na usimamizi wa utawala bora  na ndio taasisi  ya kwanza barani Afrika  iliyoanzishwa na Mwalimu Julius  Nyerere kwa ajili ya kazi hiyo.

Macharia alieleza kuwa kwa kutambua uimara na ukongwe wa tume katika masuala ya utawala bora ndio maana wameona ni vyema  kuja kujifunza na kutafuta  namna nzuri ya kushirikiana  katika kujenga maadili ya viongozi na utawala unaofaa kwenye jamii zao.

“masuala ya maadili ya uongozi kwetu yalianzishwa mwaka 2011 kwa sheria ya maadili na mapambano dhidi ya rushwa, hivyo  taasisi yetu  bado ni changa,  tumekuja kujifunza kutoka kwenu ili tuweze kushirikiana kwa njia tofauti kuhakikisha nchi zetu zinakuwa na utawala unaofaa”,alisema Macharia

Macharia aliendelea kusema kuwa katika chuo chao wanafundisha masuala ya maadili ya uongozi, hivyo anawakaribisha tume kwenda kushirikiana nao katika chuo hicho kufundisha kwani lengo la chuo hicho ni kukuza maadili ya viongozi.

“Lengo la chuo chetu ni kukuza maadili ya viongozi ili kuwa na utawala unaofaa, siku zote tunasema ni vyema kuzuia kuliko kusubiri jambo liharibike ndio muanze kulirekebisha”, alisisitiza Macharia

Naye, Jaji Mwaimu akiongea katika kikao hicho kifupi alisema kuwa ni kweli tume ni taasisi kongwe sana katika masuala ya utawala bora ambayo ilianzishwa mwaka 1965 na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere wakati huo ikiitwa tume ya kudumu ya uchunguzi kwa lengo maalumu la kusimamia maadili ya viongozi mpaka ilipobadilishwa kikatiba mwaka 2001 kuwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

“Jambo hilo mlilolifanya la kuwa na chuo cha maadili ni maamuzi mazuri, na hivyo sisi sote kwa pamoja tuna mahala pa kujifunza pia kutoka kwenu”, alisema Mwaimu

“Japo sisi tume hatufanyii kazi moja kwa moja masuala ya maadili ya viongozi lakini tumekuwa na ushirikiano mzuri sana na Sekretarieti ya maadili ya viongozi na taasisi ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (PCCB), na mara zote wananchi wanapoleta malalamiko yanayohusu maadili ya viongozi au masuala yanayohusiana na rushwa tumekuwa tukiyaelekeza huko kwani wao ndio taasisi zilizoundwa kusimamia masuala hayo” Jaji Mwaimu alimueleza Kamishna Macharia

Akiongea awali, Jaji Mwaimu alimueleza Kamishna huyo kuwa tume ni Idara huru ya serikali iliyoanzishwa kikatiba na kupewa jukumu la kulinda, kuhifadhi na kutetea haki za binadamu na kusimamia misingi ya utawala bora.

“Mimi na wenzangu tuliopewa dhamana ya kuongoza taasisi hii tutajitahidi kuhakikisha tunafanya kazi zetu kwa weledi mkubwa tukizingatia sheria na taratibu zilizowekwa na nchi”,alieleza Jaji Mwaimu

Naye, Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Dkt. Fatma Halfan alisema katika kikao hicho  kuwa suala  la ushirikiano ni jambo  muhimu, hivyo waendelee kushirikiana, na kuhusu suala la kwenda kufundisha katika chuo hicho cha maadili nchini Kenya ni jambo linalowezekana na wako tayari kushirikiana nao katika kufanikisha hilo.

Aidha, Dkt. Fatma alimueleza Kamishna Macharia kuwa tume ni taasisi ya muungano hivyo wakipata nafasi wasisite kwenda Zanzibar pia ili kujifunza zaidi.

Katika ziara yake hiyo, Kamishna Macharia aliambatana na maafisa kutoka tume hiyo ya Kenya ambao ni Kairishi Marimba, Patrick Owinu na Stella Mbele.

Wengine ni Viongozi waandamizi kutoka Sekretarieti ya Maadili nchini ambao ni Waziri Kipacha na Jasmin Bakari. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.