Habari za Punde

LINDI WAASWA KUJIUNGA NA VIFURUSHI VYA BIMA YA AFYA

Mkuu wa mkoa wa Lindi Mhe. Godfrey Zambi akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya kuhamasisha wananchi kujiunga na vifurushi vya bima ya afya kupitia mfuko wa Taifa wa Bima ya AFya (NHIF) mkoani humo Desemba 20, 2019.

Na Mwandishi wetu- Lindi
Mkuu wa Mkoa wa Lindi Godfrey Zambi amesema mpango wa vifurushi vya bima ya afya una lengo la kuhakikisha kuwa tunakuwa na Taifa lenye afya na lenye nia ya kuzalisha mali kuelekea uchumi wa kati kwa kuwa tutakuwa na nguvu kazi yenye afya.


Akiongea wakati wa Uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha watanzania kujiunga na vifurushi vya bima ya afya Mkoani Lindi, Mhe. Zambi amesema huu ni wakati kwa watanzania kuchangamkia fursa hiyo ili kuwa na uhakika wa matibabu.

“Niwapongeze sana NHIF kwa kuja na mpango huu, mpango huu ni suluhisho kwa watanzania wengi ambao awali hawakuwa na uwezo wa kujiunga na bima ya afya, leo hii kwa 192,000 tu unakuwa na uhakika wa matibabu kwa mwaka mzima, sasa tunakwenda kutengeneza taifa lenye watu wenye afya kwa ajili ya uzalishaji”-Mhe. Zambi

Aidha, Mhe. Zambi alisema kuwa mpango wa vifurushi hivi ni mzuri kwa kuwa umezingatia Idadi ya huduma muhimu za afya na uhai wa mfuko hivyo watanzania hawana budi kujiunga na mpango huu kwa uhakika wa huduma za afya.

Akiongea wakati wa uzinduzi huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NHIF Bi. Anne Makinda amesema kuwa Bima ya Afya ndio ufunguo wa afya yako na pia ni uhai. Mkuu wa mkoa wa Lindi Mhe. Godfrey Zambi (katikati mwenye suti) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF ) Bi. Anne Makinda na Viongozi wa mfuko huo pamoja na wananchi mara baada ya uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha wananchi kujiunga na vifururshi vya bima ya afya mkoani humo Desemba 20, 2019.

Mhe. Makinda aliongeza kuwa ukishakuwa na Kadi ya Bima ya Afya hiyo ndio pesa yako na dawa yako hivyo watanzania tujiunge na mpango huu kwa faida ya afya zetu.

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo Bw. Bernard Konga alisema kuwa Hatua hii ya uzinduzi wa vifurushi ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya kuhakikisha watanzania wanakuwa na uhakika wa huduma za afya na kupata matibabu kuanzia zahanati hadi Taifa lakini kwa ngazi kanda na taifa mwanachama atapata huduma kwa utaratibu wa rufaa.

Akiongea baada kupata kadi za bima ya afya kwa mpango wa vifurushi Zuberi Bakari Juma amesema kuwa mpango huu ni mkombozi kwake kwani amekuwa akilazimika kutumia zaidi ya milioni moja ndani ya mwezi kwa ajili ya matibabu ya mtoto wake lakini kwa mpango huu ataweza kumtibia mwanae kwa kiwango chini ya hicho kwa mwaka mzima.

Naye Mwasa Jeremiah Jungi Mkazi wa Lindi amesema ameamua kukata bima ya afya kwa mpango wa vifurushi kutokana na urahisi wake tofauti na ilivyokuwa awali na sasa ana uhakika wa huduma za afya.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.