Habari za Punde

CAMFED yaipigia chapuo Elimu Bure

Mkurugenzi wa Shirika linalojishughulisha na Ufadhili wa Wanafunzi wa kike CAMFED, Bi.Lydia Wilbard akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari(hawapo pichani), kuhusu wanafunzi 9,877  wa kike watakaofadhiliwa masomo yao ya Sekondari mwaka huu 2020, kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi CAMFED, Bi.Jeane Ndyetabura.
Mwenyekiti wa Bodi CAMFED, Bi.Jeane Ndyetabura, akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari (hawapo pichani), kuhusu wanafunzi 9,877  wa kike watakaofadhiliwa masomo yao ya Sekondari mwaka huu 2020, kulia ni Mkurugenzi Mkuu CAMFED, Bi. Lydia Wilbard.

Mkurugenzi wa Shirika linalojishughulisha na Ufadhili wa Wanafunzi wa kike CAMFED, Bi.Lydia Wilbard na wafanyakazi wengine kutoka shirika hilo akiwa kwenye picha ya pamoja na Wawakilishi wa wanafunzi wa kike wanaofadhiliwa na Shirika hilo mara baada ya mkutano na waandishi wa habari leo Januari 27, 2020 Jijini Dar es Salaam

 Picha na Idara ya Habari-MAELEZO.


Na.Mwandishi Wetu-MAELEZO.                                                                                       
Katika kuadhimisha siku ya Elimu Duniani inayoazimishwa kila mwaka tarehe 24 Januari, Shirika lisilo la kiserikali linalojishughulisha na kuwafadhili  wanafunzi wa kike wanaokutana na vikwazo mbalimbali ikiwemo vifaa vya shule, sare za shule na unyanyasaji wa kijinsia CAMFED, limesifu jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano ya kutoa Elimu bure kuanzia shule ya Msingi hadi Sekondari.

Akizungumza katika Mkutano na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bi.Lydia Wilbard alisema kuwa wamekuwa wakifanya kazi kubwa kuwainua watoto wa kike ambao wanapitia katika mazingira magumu ili wapate elimu katika kiwangi kinachostahili,na kwamba kwa sasa kazi yao imekuwa rahisi kutokana na serikali kutoa elimu bure.

“Katika kuadhimisha siku ya elimu duniani CAMFED tumeendelea kupanua wigo katika maeneo mengi zaidi nchini na kuweza kuzifikia shule za sekondari 471 katika halmashauri 32, na programu hii imewezesha wanafunzi 50,000 wa kike kufanikisha masomo yao ya Sekondari”, Alisema Bi. Wilbard.

Aidha katika kutekeleza majuku yao ya kuwasiadia wanafunzi wa kike ili kufikia malengo yao, Bi. Wilbard alisema kuwa CAMFED kwa mwaka huu inalenga kuwasaidia wanafunzi 9,877 kutimiza malengo yao ya kusoma sekondari na tayari kiasi cha Sh. Bilioni mbili zimeshatolewa kuwasadia wanafunzi hao wa kike kulingana na mahitaji ya kila mwanafunzi.

Alisema katika miaka ya nyuma CAMFED ilikuwa na jukumu kubwa la kugharamia mahitaji ya mwanafunzi ikiwemo michango ya shule, Ada na mahitaji mengine ambayo wanufaika wa program hiyo walihitajika kupata lakini baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani na kutoa elimu bure wameweza kusaidia wanafunzi wengi zaidi baada ya jukumu la ada kuchukuliwa na Serikali.

“ Kuondolewa kwa ada ya shule mwaka 2015 imewezesha wanafunzi wengi kupata urahisi wa kusoma shule, lakini kwa wanafunzi wa kike walioko kwenye mazingira magumu wanapata ugumu wa kwenda shule kwa sababu ya kukosa vifaa vya shule, sare na mahitaji mengine ambayo mtoto wa kike anapaswa kuyapata, kwa hiyo elimu bure imepunguza mzigo wa familia duni”, Alisema  Bi.Wilbard.

Aliongeza kuwa CAMFED ambayo hasa inawanafunzi wa kike ambao waliwahi kunufaika na mradi huo wamekuwa wakifanya kazi ya kuelimisha jamii na kuwapa matumaini wanafunzi walioacha shule hatimaye kurejea mashuleni ambapo zaidi ya wanafunzi 5,500 wa kike waliweza kurejea shuleni na kuendelea na masomo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi wa CAMFED, Bi. Jeane Ndyetabura alisema kuwa  Shirika hilo lililkuwa na mfumo maalumu wa kuwatambua wanafunzi walioko kwenye mazingira magumu na kwenye hilo iligundulika kuwa watoto wa kike wanapitia katika hali ngumu Zaidi.

“Tulikuwa na mfumo maalumu ambao ulitutambulisha kuwa watoto wa kike ambao wako kwenye mazingira hatarishi ikiwemo umasikini, uhitaji mkubwa wa kiushauri, kukosa wazazi wote na kuwekwa kwenye malezi mengine ambayo hayaendani na ndoto zao za kupata elimu na sasa CAMFED inafanya kazi kubwa kuwainua popote pale walipo ilimradi tu imekutana nao”, Alisema Bi.Ndyetabura.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.