Mkurugenzi wa Shirika linalojishughulisha na Ufadhili
wa Wanafunzi wa kike CAMFED, Bi.Lydia Wilbard akifafanua jambo kwa Waandishi wa
Habari(hawapo pichani), kuhusu wanafunzi 9,877
wa kike watakaofadhiliwa masomo yao ya Sekondari mwaka huu 2020, kushoto
ni Mwenyekiti wa Bodi CAMFED, Bi.Jeane Ndyetabura.
Mwenyekiti wa Bodi CAMFED, Bi.Jeane Ndyetabura,
akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari (hawapo pichani), kuhusu wanafunzi
9,877 wa kike watakaofadhiliwa masomo
yao ya Sekondari mwaka huu 2020, kulia ni Mkurugenzi Mkuu CAMFED, Bi. Lydia
Wilbard.
Mkurugenzi wa Shirika linalojishughulisha na Ufadhili
wa Wanafunzi wa kike CAMFED, Bi.Lydia Wilbard na wafanyakazi wengine kutoka
shirika hilo akiwa kwenye picha ya pamoja na Wawakilishi wa wanafunzi wa kike
wanaofadhiliwa na Shirika hilo mara baada ya mkutano na waandishi wa habari leo
Januari 27, 2020 Jijini Dar es Salaam
Picha na Idara ya Habari-MAELEZO.
Na.Mwandishi Wetu-MAELEZO.
Katika kuadhimisha siku ya Elimu Duniani
inayoazimishwa kila mwaka tarehe 24 Januari, Shirika lisilo la kiserikali linalojishughulisha
na kuwafadhili wanafunzi wa kike wanaokutana
na vikwazo mbalimbali ikiwemo vifaa vya shule, sare za shule na unyanyasaji wa
kijinsia CAMFED, limesifu jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano ya kutoa Elimu
bure kuanzia shule ya Msingi hadi Sekondari.
Akizungumza katika Mkutano na Waandishi wa Habari
Jijini Dar Es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bi.Lydia Wilbard alisema
kuwa wamekuwa wakifanya kazi kubwa kuwainua watoto wa kike ambao wanapitia
katika mazingira magumu ili wapate elimu katika kiwangi kinachostahili,na
kwamba kwa sasa kazi yao imekuwa rahisi kutokana na serikali kutoa elimu bure.
“Katika kuadhimisha siku ya elimu duniani CAMFED
tumeendelea kupanua wigo katika maeneo mengi zaidi nchini na kuweza kuzifikia shule
za sekondari 471 katika halmashauri 32, na programu hii imewezesha wanafunzi
50,000 wa kike kufanikisha masomo yao ya Sekondari”, Alisema Bi. Wilbard.
Aidha katika kutekeleza majuku yao ya kuwasiadia
wanafunzi wa kike ili kufikia malengo yao, Bi. Wilbard alisema kuwa CAMFED kwa
mwaka huu inalenga kuwasaidia wanafunzi 9,877 kutimiza malengo yao ya kusoma sekondari
na tayari kiasi cha Sh. Bilioni mbili zimeshatolewa kuwasadia wanafunzi hao wa
kike kulingana na mahitaji ya kila mwanafunzi.
Alisema katika miaka ya nyuma CAMFED ilikuwa na jukumu
kubwa la kugharamia mahitaji ya mwanafunzi ikiwemo michango ya shule, Ada na
mahitaji mengine ambayo wanufaika wa program hiyo walihitajika kupata lakini
baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani na kutoa elimu bure wameweza
kusaidia wanafunzi wengi zaidi baada ya jukumu la ada kuchukuliwa na Serikali.
“ Kuondolewa kwa ada ya shule mwaka 2015 imewezesha
wanafunzi wengi kupata urahisi wa kusoma shule, lakini kwa wanafunzi wa kike
walioko kwenye mazingira magumu wanapata ugumu wa kwenda shule kwa sababu ya
kukosa vifaa vya shule, sare na mahitaji mengine ambayo mtoto wa kike anapaswa
kuyapata, kwa hiyo elimu bure imepunguza mzigo wa familia duni”, Alisema Bi.Wilbard.
Aliongeza kuwa CAMFED ambayo hasa inawanafunzi wa kike
ambao waliwahi kunufaika na mradi huo wamekuwa wakifanya kazi ya kuelimisha
jamii na kuwapa matumaini wanafunzi walioacha shule hatimaye kurejea mashuleni
ambapo zaidi ya wanafunzi 5,500 wa kike waliweza kurejea shuleni na kuendelea na
masomo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi wa CAMFED, Bi.
Jeane Ndyetabura alisema kuwa Shirika
hilo lililkuwa na mfumo maalumu wa kuwatambua wanafunzi walioko kwenye
mazingira magumu na kwenye hilo iligundulika kuwa watoto wa kike wanapitia
katika hali ngumu Zaidi.
“Tulikuwa na mfumo maalumu ambao ulitutambulisha kuwa
watoto wa kike ambao wako kwenye mazingira hatarishi ikiwemo umasikini, uhitaji
mkubwa wa kiushauri, kukosa wazazi wote na kuwekwa kwenye malezi mengine ambayo
hayaendani na ndoto zao za kupata elimu na sasa CAMFED inafanya kazi kubwa
kuwainua popote pale walipo ilimradi tu imekutana nao”, Alisema Bi.Ndyetabura.
No comments:
Post a Comment