Habari za Punde

DKT. MPANGO:WAHASIBU MAFISADI KUKIONA CHA MOTO

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango, akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa  kikao kazi cha kuandaa taarifa za  hesabu za majumuisho za Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/19 katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere  jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya wahasibu kutoka mikoa mbalimbali wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi cha kuandaa taarifa za Hesabu za Majumuisho za Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/19, kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere,  jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya wahasibu kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi cha kuandaa taarifa za hesabu za majumuisho za Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/19, kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Na.Ramadhani Kissimba na Josephine Majura, Dar es Salaam

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.  Dkt. Philip Isdor Mpango, ameiagiza Menejimenti ya Wizara ya Fedha na Mipango kuwachukulia hatua kali za kinidhamu wahasibu wote wanaofanya vitendo vinavyokinzana na maadili ya kitaaluma ya uhasibu kama wizi, ubadhirifu wa mali za umma, ufisadi na rushwa.

Dkt. Mpango alitoa maagizo hayo wakati akifungua Kikako Kazi cha kuandaa Hesabu za Majumuisho za Serikali za mwaka 2018/19 pamoja na kuzindua Mfumo mpya wa uandaaji wa taarifa za fedha za Majumuisho (Government Accounting Consolidation System (GACS), Jijini Dar es Salaam

Dkt. Mpango aliwataka wahasibu wote nchini kuwa wazalendo na kusimamia ipasavyo matumizi ya rasimali za Umma na kuwataka kuhakikisha kuwa usalama katika Mifumo ya Fedha unakuwa madhubuti ili kuondoa uwezekano wa mifumo hiyo kudukuliwa na kuleta hasara kubwa kwa Serikali na Wananchi.

Aidha Dk. Mpango alimpongeza Mhasibu Mkuu wa Serikali CPA Francis Mwakapalila, pamoja na Mkurugenzi wa Mifumo ya Fedha Bw. John Sausi kwa kuonesha dhamira na nia ya kweli ya kuhakikisha wanatengeneza Mifumo bora ya kifedha ili kuleta ufanisi mkubwa katika kukusanya na kuhasibu mapato na matumizi ya Serikali.

Aliongeza kuwa dhamira hiyo  imedhihirika kwa kuanzisha Mifumo ya Kifedha ya kimtandao kama Government e-payment Gateway (GePG), Government Salary Payment Platform (GSPP), na sasa Government Accounting Consolidation System (GACS).

‘’Nimefurahi sana kuona kwamba ndani ya kipindi kifupi cha miaka minne tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, mmeanzisha Mifumo mingi na madhubuti ya kukusanya Mapato na Maduhuli ya Serikali, pamoja na Mifumo ya kuhasibu rasilimali za umma yenye kukidhi viwango vya kimataifa” alisema Dkt. Mpango.

 Aliongeza kuwa ni ushahidi bayana kuwa, watendaji hao wanatafsiri kwa vitendo dhamira na dira ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi shupavu wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli  ya kusimamia rasilimali za nchi kwa manufaa ya Wananchi  hasa Wanyonge.

Pia alieleza kuwa  matarajio ya Serikali ni kwamba mfumo huu ulioanzishwa pamoja na Mifumo iliyokwisha kuanzishwa itaitumika vizuri kwa weledi na uadilifu mkubwa katika kutoa huduma bora kwa Wananchi na ikizingatiwa hilo matarajio ya wananchi na rasimali za umma zitatumika ipasavyo kuboresha Maisha yao.

Awali Mhasibu Mkuu wa Serikali CPA. Fransis Mwakapalila alisema hatua ya kuandaa Hesabu za Majumuisho kwa kutumia Mfumo wa Kielektroniki unaifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza Barani Afrika kutayarisha Hesabu za Majumuisho kwa kutumia mfumo uliandaliwa na wataalamu wake wa ndani kutoka Wizara ya Fedha na Mipango.

CPA. Mwakapalila alisema kwa sasa Tanzania ni nchi inayoongoza kwa ubora wa Taarifa za FeFha za Majumuisho (CFS) zenye kukidhi viwango vya Kimataifa katika sekta ya Umma (IPSAS) Barani Afrika.

Akizungumza katika kikao kazi hicho Mkurugenzi wa Idara ya Mifumo ya Usimamizi wa fedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. John Sausi, amesema Idara yake itaendelea kujenga mifumo ya kielektroniki ya fedha ili kuhakikisha makusanyo ya pesa za Serikali yanapita katika mifumo sahihi.

“Mafanikio yanayopatikana katika uandaaji wa mifumo hii yanatokana na watalaamu kutoka Wizara ya Fedha na Mipango kuwa na uzalendo wa kuitumikia nchi yao, na wataalamu hao wamekuwa wakiandaa mifumo mbalimbali ukiwemo  mfumo wa kukusanya maduhuli ya Serikali kwa njia ya Mtandao (GePG) ambapo  Taasisi zaidi 616 zimeshaunganishwa kwenye mfumo huo.

Bw.Sausi alisema kuwa mfumo mpya wa uandaaji wa taarifa za fedha za majumuisho (GACS) ambao umezinduliwa na Mhe.Dkt. Philip Isdor Mpango utasaidia kupunguza utiriri wa kuwa na mifumo mingi ya uandaaji wa taarifa za fedha.




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.