Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Mgeni Rasmin Katika Hafla ya Taarab Maalum ya Sherehe za Miaka 56 ya Mapoinduzi ya Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akimsalimia Msanii Mkongwe wa Taarab Zanzibar.Bi. Mwanajuma Ali Hassan, aliyeimba wimbo wa "Mpunga Kinuni" wakati wa hafla ya Taarab ya Kikundi cha Taifa Zanzibar Kuadhimisha Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar iliofanyika katika ukumbi wa Sheikh. Idrisa Abdulwakili Kikwajuni Zanzibar jana 12-1-2020 usiku. 

RAIS wa Zanzibar na  Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein jana usiku alijumuika na wananchi mbali mbali kwenye taarabu rasmi ya maadhimisho ya miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Katika hafla hiyo iliyofanyika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni, magwiji wa sanaa ya taarab kutoka Kikundi cha Taifa hapa nchini, walimudu vyema kukonga nyoyo za wananchi waliohudhuria kutokana na umahiri wao wa kucharaza ala pamoja kughani nyimbo mbali mbali, ikiwemo zenye kuleta hamasa ya Mapinduzi.

Wasanii nguli, akiwemo Profesa Mohamed Elias, Profesa Gogo, Al-anisa Sada Mohamed, Ustadh Idd Sued, Ustadh Makame Faki (sauti ya zege), Al-anisa Sharia Issa na wengineo, walitawala vyema jukwaa kiasi cha kuwafanya wasikilizaji kushindwa kujizuia na kuibua vifijo na nderemo.

Miongoni mwa nyimbo zilizovuta hisia na kushangiliwa muda wote ni ile ya ‘Tumbili hafugiki’ aliyoimba msanii mahiri Profesa Gogo ambapo kiitikio chake kilisikika, ’hafugiki Tumbili mnyama mkorofi, umpe kile na hiki bado yeye hatosheki, kazoweya Tumbili kuchapiachapia miti’.

Nae, Al-anisa Fatuma Issa, (mwimbaji mualikwa) akadhihirisha thamani ya sauti yake, pale alipoimba wimbo maarufu wa ‘haya maumbile yangu’, wimbo aliouimba miaka kadhaa iliyopita na kumpatia sifa kubwa.

Kwa ujumla, usiku wa Januari 12, ulikuwa ni usiku maalum kwa wapenzi wa sanaa ya taarabu waliohudhuria, nyimbo mbali mbali zilizoghaniwa zilitosha kuwaburudisha na kukonga nyoyo zao.

Nyimbo nyengine zilizoimbwa usiku huo zilikuwa ni pamoja na ‘Mpewa hapokonyeki’ iliyoyoghaniwa na Al-anisa Mariam Juma, Wakwezi na wakulima (Ustadh Makame Faki), Dunia ina fisadi (Al-anisa Sharia Issa), Tarehe 11 (Ust. Iddi Sued), Nnavyokupenda (al-anisa Hilda Mohamed), Anaetowa ni mola (Al-anisa Sada Mohamed) na Waliosema hatuwezi iliyoimbwa na Ustadh Hafidh Abdusalami.

Mapema, Katibu Mkuu Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo Omar Hassan ‘King’ alisema Wizara imetekeleza agizo la Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi , Dk. Ali Mohamed Shein  la kikundi hicho kupatiwa vifaa ili kufanikisha vyema shughuli zake, na kubainisha kuwa  baadhi ya  vifaa hivyo vimeanza kutumika.

Aidha, alisema utekelezaji wa agizo la kuwakumbuka na kuwaalika wasanii wa zamani katika hafla kama hizo limetekelezwa, na kuainisha kuwa baadhi ya wasanii  walioalikwa, kuwa ni pamoja na Mwajuma Ali Hassan ambae alitajika kutokana  na nyimbo ya ‘mpunga na kiwanja’. 

Wengine ni mtunzi/muimbaji  Mariam Hamdani, Salum Kassim aliesifika kwa nyimbo ya ‘macho yake’, Ali Masoud Suleiman anaekumbukwa kwa wimbo wa’kinu’, Fatma Issa alietamba na wimbo wa ‘umewashuka’ pamoja msanii na muigizaji Borafia Silima Juma.
Taarab hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kitaifa, akiwemo Makamo wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na viongozi mbali mbali.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.