Habari za Punde

Tume yatembelea TLS, yahimiza ushirikiano

Muwakilishi wa rais wa TLS, Mary Munissi (kushoto) akimkabidhi baadhi ya Machapisho ya TLS Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu. 
Muwakilishi wa rais wa TLS, Mary Munissi akiongea katika kikao hicho kifupi mara baada ya kumkaribisha Mwenyekiti wa THBUB.

Na Mbaraka Kambona,
Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu ametembelea Chama cha Wanasheria (TLS) jijini Dodoma na kuhimiza ushirikiano baina ya taasisi hizo.

Jaji Mwaimu alitoa kauli hiyo Januari 23, 2020 alipofanya ziara katika ofisi za chama hicho kwa lengo la kufahamiana na kujenga mazingira mazuri ya ushirikiano.

Akiongea katika kikao hicho kifupi, Jaji Mwaimu alimueleza Muwakilishi wa Rais wa TLS jijini Dodoma, Mary Munissi kuwa tume inafahamu kuwa TLS imekuwa msaada mkubwa kwa jamii katika  utoaji wa msaada wa kisheria na kuwaelimisha wananchi kuhusu haki zao.

“Majukumu yetu kwa kiasi kikubwa yanafanana, hivyo itakuwa vizuri tukishirikiana katika kuwasaidia wananchi kupata na kufurahia haki zao”, Jaji Mwaimu alieleza

“Ni jukumu letu sisi sote kuwahudumia  na kulinda haki zao wananchi, na kuhakikisha kuwa wakati wote wanaweza kupata haki zao na kufikia kwa urahisi vyombo vinavyohusika na utoaji haki nchini”, aliongeza

“Tumekuja hapa leo kuonesha nia yetu ya kutaka ushirikiano, kushirikiana na wadau kwetu sisi ni moja ya kipaumbele chetu, hivyo niwaeleze kuwa tupo pamoja, tuunganishe nguvu zetu na tufanye kazi kwa dhumuni la kuwahudumia wananchi ”, alisisitiza

Akiongezea aliyoyasema Jaji Mwaimu, Makamu Mwenyekiti wa THBUB, Mhe. Mohamed Hamad alisema kuwa  tume wakati wote imekuwa na ushirikiano mzuri na Asasi za Kiraia nchini na mpaka sasa wameshaingia mkataba wa ushirikiano na Asasi ishirini na moja (21).

“Sisi tume tunaamini haki za binadamu ni suala mtambuka ambalo linahitaji jitihada za pamoja kutekeleza, tume peke yake haiwezi, jambo muhimu ni kuunganisha nguvu zetu ili kutekeleza na kusimamia haki za binadamu nchini” aliongeza Mhe. Hamad

Kwa upande mwingine, Muwakilishi wa rais wa TLS, Mary Munissi alisema kuwa amefurahishwa na ziara hiyo ya viongozi wa juu wa tume kutembelea ofisi hizo na kuahidi kuwa salamu hizo atazifikisha kwa rais, na kuahidi kuwa watatumia vyema ushirikiano huo ambao utasaidia kurahisisha utendaji wa kazi.

Kwa kuongezea, Wakili Isaac Mwaipopo wa TLS alisema kuwa chama hicho kwa wakati wote kimekuwa kikijitahidi kutoa msaada wa sheria kwa wananchi, na pale wanapopata malalamiko ambayo yanakuwa nje ya uwezo wao wanayawasilisha katika mamlaka husika.

Katika hatua nyingine, TLS imeiomba tume kuwapa ushirikiano wa karibu hususan katika eneo la haki za binadamu, na kuangalia uwezekano wa kuwasaidia kuwakwamulia vikwazo wanavyokutana navyo wakati wa utekelezaji wa mradi wao wa upatikanaji wa haki.

Aidha, Wakili Mwaipopo aliishauri Tume kutumia tafiti zao walizofanya katika masuala ya haki za binadamu kwani kwa muda mrefu wamefanya utafiti katika eneo hilo na wana taarifa ambazo zinaweza kuisaidia tume kujua ukubwa wa tatizo na kuweka mikakati ya kupata ufumbuzi.

Mbali na kutekeleza mradi wa upatikanaji wa haki, TLS inaendelea kusaidia kujenga mahusiano baina ya wasaidizi wa sheria na serikali, na mpaka sasa wanafanya kazi kwa karibu na Jeshi la Magereza, Polisi na Wizara ya Katiba na Sheria. Pia, TLS wamekiri kuwa serikali imekuwa ikiwashirikisha katika michakato mbalimbali ya kuandaa miswada ya kisheria na utungwaji wa sheria mpya.

Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu (katikati-mwenye koti la kijivu) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa tume na wa TLS. Kushoto kwake ni Muwakilishi wa rais wa TLS, Mary Munissi

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.