RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza jinsi alivyopokea
kwa furaha taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ya kuendelea kukua kwa uchumi
wa Zanzibar.
Dk. Shein aliyasema hayo Ikulu Jijini Zanzibar wakati
alipofanya mazungumzo na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Florens
Luoga ambapo katika mazungumzo hayo Cavana huyo alimueleza Dk. Shein jinsi
uchumi wa Zanzibar unavyoendelea kuimarika.
Katika maelezo hayo Rais Dk. Shein alimueleza
kiongozi huyo kuwa hiyo ni habari njema ambayo inatoa mwanga wa maendeleo ya
uchumi hapa Zanzibar kwani juhudi za makusudi bado zinaendelea kuchukuliwa
katika kuhakikisha uchumi unaimarika.
Rais Dk. Shein aliongeza kuwa hatua hiyo imefikiwa
kutokana na uwepo wa uongozi bora sambamba na mashirikiano mazuri yaliopo kati
ya Serikali, wananchi pamoja na na Benki
kuu ya Tanzania (BoT).
Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika suala
zima la mfumko wa bei pia, amepokea kwa furaha
maelezo ya kuwa mfumko wa bei uko vizuri hapa nchini hali ambayo inaleta
faraja kwa wananchi.
Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza neema
ya chakula iliyopo Zanzibar na kusisitiza kuwa Zanzibar hakuna shida ya chakula
na wananchi wamekuwa wakila chakula wanachokitaka.
Hivyo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania (BoT)
hasa ikizingatiwa kwamba hiyo ni Benki ya wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania.
Pamoja
na hayo, Profesa Luoga alitumia fursa hiyo kumueleza Dk. Shein mashirikiano
mazuri yaliopo kati ya uongozi wa Wizara ya Fedha Zanzibar na Benki hiyo hatua
ambayo imeweza kuleta mafanikio makubwa.
Rais
Dk. Shein alimpongeza Gavana huyo kwa juhudi anazozichukua katika kuhakikisha
Benki hiyo inaimarika na inaendelea kuwa tegemeo kwa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania huku akieleza matumaini yake kwa uongozi mpya wa Profesa Florens
Luoga.
Pamoja
na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa (BoT), ni Benki ya Muungano ambayo imekuwa
ikifanya vyema shughuli zake kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na kuahidi kuendelea kuiunga mkono yeye na Serikali anayoiongoza.
Nae Gavana
wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Florens Luoga alimthibitishia Rais Dk. Shein
kuwa uchumi wa Zanzibar unaendelea kuimarika kila uchao na kumpongeza Rais Dk.
Shein kwa kuendelea kuisimamia hali hiyo.
Gavana
huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), itaendelea
kutoa ushirikiano wake kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa lengo la
kuhakikisha uchumi wa Zanzibar unazidi kuimarika kutoka wastani wa asilimia
saba hivi sasa.
Gavana
wa benki kuu ya Tanzania Florens Luoga amesema kuwa bado benki kuu
haijachapisha wala kuingiza pesa mpya kwenye mzunguko tangu mwaka 2009 na
kwamba pesa iliyopo kwenye mzunguko inatosha kabisa kwa mahitaji ya soko.
Aidha,
Gavana huyo alieleza kuwa Benki kuu ya Tanzania (BoT) inaendelea na mapambano kwa
watengenezaji, wasaambazaji na watumiaji wa Noti bandia na kueleza hatua
inazozichukua katika kutoa elimu kwa wananchi juu ya kufanya utambuzi wa Noti
bandia ili kuepuka utapeli.
Aliongeza
kuwa mashirikiano ya pamoja yanahitajika katika kupambana na hali hiyo ambayo
katika kipindi hichi imeweza kujitokeza na (BoT) kuahidi kuendelea kudhibiti
hali hiyo kwa kupambana na wahalifu wote
Pia,
kiongozi huyo alieleza benki kuu
itaendelea kutekeleza Sera yake ya Sarafu Safi huku akiziomba benki zote
kuhakikisha zinatoa huduma rafiki kwa wananchi ili waweze kutumia vyema huduma
hizo.
Alieleza
haja kwa Benki kufungua Matawi yake nje ya mji hapa Zanzibar ili wananchi
waweze kupata huduma hizo kwa urahisi mkubwa na kusisitiza kuwa azma ya (BoT)
ni kuhakikisha huduma hiyo inapatikana si zaidi ya kilomita tano ya makaazi ya
wananchi.
Profesa
Luoga alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ina fedha za
kutosha katika kuendeleza shughuli zake za kibenki hapa nchini huku akieleza azma
yake ya kuliimarisha Tawi lake la Benki la hapa Zanzibar.
Alimthibitishia
Rais Dk. Shein kwamba mfumko wa bei hapa nchini uko vizuri na (BoT) inaendelea
kuuthibiti ikiwa ni pamoja na kudhibiti kupanda kwa bei ya mazao ya chakula
hiyo ni kutokana na mazao mengi hupatikana kwa miongo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment