Habari za Punde

KIKAO CHA IDARA YA LESENI NA JUMUIYA YA GARI ZA ABIRIA CHA MIKOA MITATU YA UNGUJA

 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji,Zanzibar Mustafa Aboud Jumbe akizungumza na Jumuiya ya Gari za Abiria kwa mikoa mitatu ya unguja  juu ya hatua  zinazohitajika kuchukuliwa ili kudhibiti kuenea janga la maradhi ya Corona,   katika Ukumbi wa Bodi ya Usafiri barabarani Mwanakwerekwe Zanzibar .
Mkuu wa Trafik Zanzibar ambae pia ni Kamishna Msaidizi wa Polisi Robert Hussein akitoa tahadhari kwa Jumuiya ya Gari za Abiria ya mikoa mitatu ya unguja  juu ya hatua zinazohitajika kuchukuliwa ili kudhibiti kuenea kwa virusi vya Corona, Kikao hicho kilifanyika  katika Ukumbi wa Bodi ya Usafiri barabarani Mwanakwerekwe Zanzibar. 
Wanajumuiya ya Gari za Abiria wa Mikoa mitatu ya Unguja wakisikiliza maelezo ya .Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji,zanzibar Mustafa Aboud Jumbe  juu ya hatua zinazohitajika kuchukuliwa ili kudhibiti kuenea janga la maradhi ya Corona, Kikao hicho kilifanyika  katika Ukumbi wa Bodi ya Usafiri barabarani Mwanakwerekwe Zanzibar
Picha zote na Khadija Khamis Maelezo Zanzibar

Na Kijakazi Abdalla - Maelezo            02/04/2020
Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi ,Mawasiliano na Usafirishaji Mustafa Aboud Jumbe amezitaka jumuiya za gari za abiria kufuata  utaratibu  uliowekwa na Wizara ya Afya kwa lengo la  kuepuka  maambukizo ya maradhi ya corona.
Hayo ameyasema katika Ukumbi wa Bodi ya  Usafiri  Barabarani Mwanakwerekwe katika kikao cha Idara ya Leseni na jumuiya za gari za abiria kwa Mikoa mitatu ya Unguja.
Amesema ni vyema kwa madereva na makonda kufuata masharti yaliyowekwa na Wizara ya afya ili kudhibiti kuenea kwa janga la maradhi ya corona.
 “Ni vyema kufuata masharti yaliowekwa na wataalamu kwani maradhi hayo si ya kuyafanyia mzaha hata kidogo”.amesema katibu.
Aidha amewataka viongozi wa jumuiya kushirikiana na Serikali kuhakikisha wanachukua tahadhari kwa  vyombo vya usafiri kwa abiria wanaotumia usafiri wa nchi kavu ili kudhibiti kuenea kwa maradhi ya corona.
Nae Kamishna Msaidizi wa Polisi  ambae pia ni  Mkuu wa Trafik Zanzibar Robert Hussein amewataka madereva na makonda wa gari za abiria kufuata maelekezo yanayotolewa na jeshi la polisi  kwani kwenda kinyume ni kosa  kisheria.
Amesisitiza kuwa Jeshi la Polisi litamchukulia hatua dereva na Konda atakaebainika anavunja sheria na kuwahakikishia kuwa hatua zitachukuliwa hapo kwa hapo.
 “Jeshi la Polisi lipo kwa kulinda mali za raia  na halina nia ya kumkomoa mwananchi, hivyo ni vyema kila mtu kufuata muongozo uliowekwa na jeshi hilo”.Amesema Mkuu huyo.
Miongoni mwa  maazimio ya kikao hicho ni pamoja na  kuwataka wakuu wa jumuiya  kuhakikisha kila gari inachukua abiria kwa idadi walioruhusiwa.
Aidha viongozi wa jumuiya ya gari za abiria wametakiwa kutoa elimu ya uelewa wa maradhi ya corona kwa madereva na makonda ili kuweza kudhibiti  kuenea mambukizo ya maradhi hayo pamoja na kupulizwa dawa gari zote za abiria.
Vilevile mabaguani wametakiwa kusimamia zoezi la abiria kukaa masafa ya kutosha wanapokuwa vituoni pamoja na  gari itayobainika kuchukua abiria kinyume na uwezo iliopewa ishushwe abiria na kuwekwa kituoni.
Aidha  Idara ya Usafiri na Leseni kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kuangalia gari chafu na kuchukuliwa hatua pamoja na jumuiya kuhakikisha gari hazikatishi kutoa huduma mpaka usiku ili kuepusha mrundikano wa abiria vituoni. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.